TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 » Sunnah  

'IYD TARATIBU NA SHERIA ZAKE

Imefasiriwa na: Ummu Ummu Ayman

Sifa njema ni za Allah, Bwana wa Ulimwengu, na rehma na amani zimshukie Mtume wetu Muhammad na aali zake na sahaba zake.

“'Iyd” ni neno la kiarabu linalomaanisha jambo la kitabia au ada, lenye kurudi na  kujirejea. 'Iyd au sikukuu ni alama au nembo inayopatikana katika kila taifa, ikiwa ni pamoja na mataifa yale yaliyotajwa katika vitabu vitukufu na yale ya waabudiao masanamu, pamoja na wengineo, kwa sababu kusherehekea sikukuu ni jambo la kimaumbile katika maumbile ya mwanaadamu. Watu wote wanapenda kuwa na matukio  maalumu ya kufanya sherehe, ambapo wanaweza kukukusanyika pamoja na kuonyesha furaha zao.

Sikukuu za mataifa ya makafiri zinaweza kufungamanishwa na mambo ya kidunia, kama kuanza kwa mwaka, kuanza kwa msimu wa kilimo, kubadilika kwa hali ya hewa, kuanzishwa kwa dola, kutawazwa kwa kiongozi, n.k. Zinaweza pia kufungamanishwa na matukio ya kidini, kama ambavyo nyingi ya sikukuu zinazowahusu Mayahudi na Wakiristo tu, mfano Alkhamisi ambayo wanadai kuwa meza maalum iliteremshwa kwa Yesu, Krismas, Mwaka Mpya, Siku ya kushukuriana, na sikukuu ambazo watu hupeana zawadi. Hizi husherehekewa katika nchi zote za Ulaya na Amerika ya Kaskazini hivi sasa, na katika nchi nyengine ambazo ukristo una nguvu, hata kama nchi yenyewe si ya kikiristo kiuhalisi. Baadhi ya wanaoitwa Waislam huweza kujiunga katika sikukuu hizi, kwa sababu ya ujinga au unafiki.

Magians nao pia wana sikukuu zao, kama Mahrajaan, Namrudh n.k.

Ma-baatini (Miongoni mwa Mashia) wana sikukuu zao pia, kama ‘Eid al-Ghadeer”, ambapo wanadai kuwa Mtume (SAW) amempa ukhalifa ‘Ali (RA) na maimamu kumi na moja   baada yake.

Waislamu wanatambulika kwa sikukuu zao.

Maneno ya Mtume (SAW) "Kila Umma una sikukuu yake na hii ni sikukuu yenu"  yanaonyesha kuwa Eid hizi mbili ni maalumu kwa Waislamu tu, na kuwa hairuhusiwi kwa Muislam kuwaiga makafiri na washirikina nao katika jambo lolote ambalo ni maalumu ndani ya sherehe zao, iwapo kama ni chakula, nguo, kuwasha moto au matendo ya ibada.

 Watoto wa Kiislam wasiruhusiwe kucheza katika sikukuu hizo za kikafiri, au kujipamba, au kujumuika na makafiri katika matukio hayo. Sikukuu zote za kikafiri au zilizozushwa ni haraam, mfano kama sherehe za Siku ya Uhuru, maadhimisho ya mapinduzi, miti ya sherehe za sikukuu au kutawazwa kwa kiongozi, siku za kuzaliwa, Sikukuu ya Wafanyakazi, Sikukuu ya Nile, Shimm al-Naseem (sikukuu ya majira ya baridi ya Wamisri), siku ya walimu, na Maulidi ya Mtume (Kuzaliwa kwa Mtume ).

Waislam hawana sikukuu ukiacha ile ya Eid al-Fitr na Eid al-Adh’haa, kwa sababu ya hadiith iliyotolewa na Anas (RA) amesema: "Mjumbe wa Allah (SAW) alikuja Madiynah na watu walikuwa na siku mbili wakicheza na kufurahi.  Akauliza, "Ni siku gani hizi mbili?" Wakasema, "Tulikuwa tukicheza na kufurahi katika siku hizi  zama za ujaahiliyya" (zama za ujinga kabla ya Uislamu).  Mtume  (SAW) akasema, "Allaah Amekupeni siku bora kuliko hizo, nazo ni siku ya 'Eid  Al-Adhaa na siku ya 'Eid Al Fitr".  (sunan Abi Dawuud 1134)

 

Yafuatayo ni maelezo kuhusu sheria na adabu za Eid mbili kwa mujibu wa Sharia ya Kiislam:

 AHKAAM AL-'IYD (Sheria katika 'Iyd)

Kufunga

Ni haram kufunga katika siku za Eid kutokana na hadiith ya Abu Sa’iyd al-Khudri (RA), amesema kuwa Mtume (SAW) amekataza kufunga katika siku ya Fitr na katika siku ya Kuchinja (Adh’haa). (Imeripotiwa na Muslim, 827)

Sheria katika Sala za 'Iyd

Baadhi ya wanavyuoni wanasema kuwa Sala ya Eid ni waajib, huu ni mtizamo wa wanavyuoni wa Kihanafi na Shaykh al-Islam Ibn Taymiyah (RA). Wanasema kuwa Mtume (SAW) alikuwa akisali sala zote za Eid na hakuacha kufanya hivyo hata mara moja. Wamechukua ushahidi katika aya (yenye tafsiri),

"Basi sali na uchinje kwa ajili ya Mola wako Mlezi"

Al-Kawthar: 2

Yaani  Sala ya Eid na kuchinja baada yake, ambayo ni amri, na kwa ukweli kuwa Mtume (SAW) aliwaamrisha wanawake watolewe kuhudhuria sala ya Eid, na kwamba mwanamke aliyekuwa hana jilbaab aazime kutoka kwa ndugu yake

Baadhi ya wanavyuoni wanasema kuwa sala ya Eid ni Fardh Kifaaya (fardhi yenye kutosheleza). Huu ni mtizamo wa Kihambali. Kundi la tatu linasema kuwa sala ya Eid ni sunnah iliyokokotezwa. Huu ni mtizamo wa Kimaalik na Kishaafi. Wanachukua ushahidi ya hadiith ya Bedui inayosema kuwa Allaah (SWT) Hakufaradhisha sala yoyote kwa waja Wake zaidi ya zile sala tano. Kwa hiyo Waislam wafanye hima kuhudhuria sala ya Eid, hususan kwa kuwa maoni ya kuwa ni wajiib yameegemea katika ushahidi wenye nguvu. Neema, baraka na malipo makubwa yanapatikana kwa kuhudhuria sala za Eid, na kwa ukweli kuwa mtu atakuwa anafuata mwendo wa Mtume (SAW) kwa kufanya hivyo, basi inatosha kuwa ni changamoto.

Mambo ya lazima na wakati wa Sala ya 'Iyd

Baadhi ya wanavyuoni wa Kihambali wanasema kuwa sharti za Sala ya Eid ni iqaamah lazima isomwe na ni lazima isaliwe kwa jamaa. Baadhi yao wamesema kuwa sharti za sala ya Eid ni sawa na zile za sala ya Ijumaa, isipokuwa katika khutba, ambapo kuihudhuria si lazima. Wengi miongoni mwa wanavyuoni wanasema wakati wa sala ya Eid unaanza pale jua linapochomoza kwa masafa ya urefu wa mshale, kwa linavyoonekana kwa macho matupu, na unaendelea mpaka jua linapokaribia kuwa sawa sawa

Maelezo ya Sala ya 'Iyd

‘Umar (RA) amesema:  “ Sala ya Eid Fitri na al-Adh’haa ni rakaa mbili zilizotimia, sio fupi fupi. Hii ni kwa mujibu wa maneno ya Mtume, na muongo ni mwenye kulaaniwa.”

Abu Sa’iyd amesema: “Mtume (SAW) amekuwa akija katika pahala pa kusalia katika siku za Fitr na al-Adh’ha, na jambo la mwanzo analofanya ni kusali”.

Takbiira inarejewa mara saba katika rakaa ya mwanzo na mara tano katika rakaa ya pili, Qur’an inasomwa baada yake katika kila rakaa.

Imeripotiwa kutoka kwa A’ishah: Takbira ya al-Fitri na al-Adh’haa ni mara saba katika rakaa ya mwanzo na mara tano katika rakaa ya pili, mbali na Takbiira ya rukuu . (imeripotiwa na Abu Dawuud; imesahihishwa na jumla ya isnaad)

Iwapo mtu amejiunga na sala amemuwahi imaam wakati wa Takbira hizi za ziada, ni juu yake kusema “Allaahu Akbar” pamoja na imaam, na halazimiki kuzilipa Takbira ambazo zimempita, kwa sababu (takbira hizo) ni sunna, sio waajib. Kuhusu nini kinatakiwa kisemwe baina ya Takbiira, Hammaad ibn Salamah ameripoti kutoka kwa Ibraahiim kuwa "Waliid ibn ‘Uqbah aliingia msikitini wakati Ibn Mas’uud, Hudhayfah na Abu Muusa wapo hapo, na akasema, “Eid ipo hapa, nini natakiwa kufanya?” Ibn Mas’uud akasema: “Sema ‘Allaahu Akbar’, msifu na mshukuru Allaah, msalie Mtume (SAW) na omba du’a, kisha sema ‘Allaahu Akbar’, msifu na mshukuru Allaah, msalie Mtume (SAW)….n.k.’ (Imeripotiwa na at-Tabaraani. Ni hadithi sahihi iliyonukuliwa katika al-Irwaa’ na kwengineko).

Kusoma Qur’aan katika Sala za 'Iyd

Imependekezwa (mustahabb) kuwa katika Sala za Eid, imaam asome surat Qaaf (sura ya 50) na surat al-Qamar (sura ya 54), kama ilivyoripotiwa katika Sahiih Muslim kuwa ‘Umar ibn Al-Khattwaab alimuuliza Abu Waaqid al-Laythi, “Nini Mjumbe wa Allaah (SAW) alikuwa akisoma katika [Eid] al-Adh’haa na al-Fitr?” Akasema, “Alikuwa akisoma Qaaf, Wal-Qur’aan al-majiid [Qaaf 50:1] na Iqtarabat as-saa’ah wa’nshaqq al-qamar [al-Qamar 54:1].

Ripoti nyingi zinaonyesha kuwa Mtume (SAW) alikuwa akisoma Suurat al A’laa [87] na Suurat al-Ghaashiyah {88], kama ambavyo alivyokuwa akizisoma katika sala ya Ijumaa. Al-Nu’maan ibn Bishr amesema:

"Mtume (SAW) alikuwa akisoma katika 'Eid mbili na siku ya Ijumaa Sabbih Isma Rabbikal-a'laa (Al-A'alaa 87:1) na Hal Ataaka Hadiythul-Ghaashiyah (Al-Ghaashiyah 88:1)"  Sahiyh Muslim 878

Samura (RA) amesema "Mtume (SAW) alikuwa akisoma katika Eid mbili Sabbih Isma Rabbikal-a'alaa (Al-a'alaa 87:1) na Hal Ataaka Hadiythul-Ghaashiyah (Al-Ghaashiyah 88:1) Imesimuliwa na Ahmad na wengine   ni Sahiyh [ Al-Irwaa 3/116]

Sala inasaliwa kabla ya khutbah

Moja ya sheria za Eid ni kuwa sala ni lazima iwe kabla ya khutbah, kama ilivyoripotiwa katika Musnad Ahmad kutoka katika hadiith ya Ibn ‘Abbaas, ambaye ameshuhudia kwamba Mtume (SAW) alisali kabla ya khutba siku ya Eid kisha akatoa khutba (Musnad Ahmad 1905.  Hadiythi hii pia iko katika Sahihi mbili)   

Yeyote anayetaka kuondoka wakati wa khutbah ameruhusiwa kufanya hivyo

‘Abd- Allaah ibn al-Saab amesema: "Nilihudhuria 'Eid pamoja na Mtume (SAW) na alipomaliza alisema, tutatoa khutba, kwa hiyo anayetaka kukaa (na kusikiliza) khutba basi akae na anayetaka kuondoka basi aondoke (Irwaa al Ghaliyl 3/96)  

Sala isicheleweshwe kwa muda mrefu:

‘Abd-Allaah ibn Bishr, sahaba wa Mtume (SAW), alitoka pamoja na watu siku ya Fitr au al-Adh’haa, na akaonyesha kutopendezwa kwa kuwa imaam alikuja akiwa amechelewa sana. Akasema " Wakati wa Mtume (SAW) tungelikuwa tumeshamaliza wakati wa sasa" na huo ulikuwa wakati wa Tasbiyh (Imesimuliwa na na Bukhaari).

 Sala za sunna, pahala pa Sala (ya 'Iyd)

Hakuna sala za sunna ambazo zinasaliwa kabla au baada ya sala ya Eid, kama alivyoripoti Ibn ‘Abbaas kuwa "Mtume (SAW) alikuwa akitoka katika siku ya Eid na akasali rakaa mbili, bila ya chochote (sala yoyote) kabla au baada yake". Hali hii ni iwapo sala itasaliwa pahala pa kusaliwa au sehemu ya wazi. Hata hivyo, iwapo watu watasali Eid msikitini, basi watatakiwa wasali rakaa mbili za Tahiyat al-Masjid (sala ya kiamkizi cha msikiti) kabla hawajakaa kitako.

Iwapo watu hawatokuwa na habari ya 'Iyd mpaka siku ya pili

Abu ‘Umayr ibn Anas ameripoti kutoka kwa ami yake miongoni mwa Ansaar kuwa alisema: "Kulikuwa na mawingu na hatukuweza kuuona mwezi wa Shawwaal, kwa hiyo tukaanza sikukwa kufunga, kisha ukaja msafara mwisho wa siku na wakamwabia Mtume (SAW) kuwa wameona mwezi wa Shawwaal siku moja kabla, akawaambia watu waache kufunga na wakaenda kuswali Eid siku ya pili"  Imeripotiwa na watano, ni Sahiyhi; Al-Irwaa' 3/102

Iwapo mtu amekosa sala ya Eid, mtazamo ulio sahihi kuliko yote ni kuwa anaweza kuilipa kwa kusali rakaa mbili.

Kuhudhuria kwa Wanawake katika Sala za 'Iyd

Hafsah amesema:  "Tulikuwa tukiwazuwia wasichana wenye hedhi kuhudhuria Sala za Eid.  Kisha akaja mwanamke kukaa katika ngome  ya Banu Khalaf na akatumambia kuhusu dada yake.  Mume wa dada yake alihudhuria  vita kumi na mbili  pamoja na   Mtume  (na akasema) ,  Dada yangu alikuwa naye katika vita sita.  Akasema tulikuwa tukiwatendea walioumia na tukiwashughulikia wagonjwa.  Dada yangu alimuuliza Mtume kama kuna ubaya wowote kutokwenda kusali Eid ikiwa hana jilbaab.  Akasema "mwache rafiki yake ampe moja wa jilbaab lake ili aweze kushuhudia  baraka za Eid na aone kujumuika kwa Waislamu"  Umm 'Atiya alipokuja nilimuuliza umemiskia Mtume (SAW) akisema hivyo? " Akasema "Baba yangu achinjwe kwa ajili yake" Na alikuwa hamtaji ila baada ya kusema "baba yangu achinjwe kwa ajili yake" . "Nimemsikia akisema kuwa wasichana na wale wanaotawishwa  au wasichana waliotawishwa na wanawake wenye hedhi  ili washuhudie baraka za Eid na kujumuika kwa waumini.  Lakini wale wenye hedhi wakae mbali na sehemu ya kusali" (Sahiyh Al Bukhaari)

Vijana wa kike (‘awaatik, mmoja ‘aatiq) ni wale waliokwisha vunja ungo au wako karibu na kufanya hivyo, au wamefikia umri wa kuolewa, au walio na thamani katika familia zao, au wasiofanyishwa kazi zisizo na heshima. Inaonekana kuwa wamekuwa wakizuiwa vijana hawa kutoka nje kwa sababu ya uovu uliojitokeza baada ya kizazi cha kwanza cha Uislam; lakini Sahaabah hawakukubaliana na hilo na wakaona kuwa sheria ya wakati wao lazima ibaki kama ilivyokuwa wakati wa Mtume (SAW).

 “Jilbaab lake”- ametakiwa kuazima baadhi ya nguo ambazo hakuwa akizihitajia.

Wanaotengwa/Wanaotawishwa”- ambao wanaowekewa paazia kipembeni mwa nyumba ambamo wari hukaa nyuma yake.

“Wanawake walio katika hedhi”- huyyadh, mmoja haa’idh– hii inaweza kurejea kwa vijana wa kike waliofikia umri wa kukua, au wanawake waliomo katika siku zao na wasio tohara.

“Wanawake walio katika hedhi wanatakiwa wajitenge na sala – pahala penyewe” – Ibn al-Munayyir amesema:   "Sababu ya kujitenga na sehemu ya kuswali ni kuwa wakisimama pamoja na wanawake wanaosali japokuwa hawasali, itaonekana kuwa hawana heshima na sala au hawajali kwa hiyo ni bora kwao kuepuka kufanya hivyo"

Imesemekana kuwa sababu ya kutakiwa wanawake walio katika hedhi kujitenga na sehemu ya kusalia ni tahadhari, kuwa wanawake wasije karibu ya wanaume bila ya sababu iwapo wao hawasali, au wasiwaudhi wengine kwa damu au harufu yake.

Hadiith hii inamtaka kila mmoja kuhudhuria sala ya Eid, na kushirikiana baina yao katika wema na ucha Mungu. Wanawake walio katika hedhi wasiachwe nyuma katika  kumtaja Allaah au sehemu njema kama mikusanyiko yenye madhumuni ya kutafuta elimu na kumtaja Allaah – ukiachia misikitini. Hadithi hii pia inaonyesha kuwa wanawake wasitoke nje bila ya jilbaab.

Hadithi hii inatuambia kuwa sio sawa kwa vijana wa kike na wanawake wanaotawishwa kutoka nje bila ya sababu inayokubalika. Inasema kuwa imependekezwa (mustahabb) kwa wanawake kuvaa jilbaab, na kuwa imeruhusiwa kuazimana nguo. Pia imeonyesha kuwa sala ya Eid ni wajibu.

Ibn Abi Shaybah pia ameeleza kuwa Ibn ‘Umar alikuwa akenda nae yeyote anaeweza kwenda nae katika wanawake wa nyumbani kwake katika sala za Eid.

Hadithi ya Umm ‘Atiyah pia inaeleza sababu ya sheria hii, ni kuwa ili wanawake waweze kushuhudia baraka ya Eid, waone mkusanyiko wa Waislam, na wapate nao baraka na utukufu wa siku hii.

At-Tirmidhi (Mwenyeezi Mungu Amrehemu) alisema katina Sunan yake, baada ya kutaja Hadiyth ya Umm 'Atiya, "baadhi ya 'ulamaa wamechukulia Hadiythi hii na kuwaruhusu wanawake waende katika Sala za Eid na wengineo hawakupendezewa.  Imeripotiwa kuwa 'Abdullah Ibn Al Mubaarak alisema, 'Sipendi  wanawake waende katika Sala  za Eid siku hizi.  Na mwanamke akishikilia kwenda basi mumewe amwachilie kwenda  lakini anapokwenda avae nguo zake kukuuu kabisa  na asijipambe.   Na akishikilia kujipamba basi asitoke nje.   Na hali hii mume anayo haki kumzuwia kutoka nje.  Imeripotiwa  kuwa bibi 'Aishah (RA) alisema, "Kama Mtume (SAW) angeliona hali za wanawake walivyo hivi sasa angeliwazuwia kwenda misikitini kama vile wanawake wa Bani Israaiyl walivyozuiliwa"  Imeripotiwa kwamba Sufyaan Al Thawriy hakupendezewa wanawake kwenda kuswali Swalah za Eid.   (At-Tirmidhiy 495)

Umm ‘Atiyah ametoa fatwa yake katika hadithi iliyotajwa hapo juu, muda baada ya kufa Mtume (SAW) kufariki, na haikuripotiwa kuwa yeyote miongoni mwa Masahaba amepingana na fatwa hii. Maneno ya ‘Aa’ishah, “Iwapo Mtume (SAW) angeona yanayofanyika kwa wanawake, angewazuilia kwenda misikitini”, hayapingi hii fatwa (alimradi tu wanawake wanatimiza masharti ya Kiislamu ya kutoka kwao nje)  Ni vizuri zaidi iwapo ruhusa itatolewa kwa wale wanawake wasiotoka kwa ajili ya kuwaangalia wanaume au kuangaliwa wao, ambao kuhudhuria kwao hakutopelekea uovu wowote na wasiokwenda kusongamana na wanaume mitaani au msikitini (yaani wanawake ambao kutoka kwao hakutosababisha fitna au kishawishi kwake au kwa wanaume).

Wanaume wawakague wanawake wao wanapotoka nje kwa ajili ya sala kuhakikisha kuwa hijabu zao ziko kamili, kwa sababu wao ndio “wachungaji” wenye jukumu kwa “machunga” wao. Wanawake wanatakiwa watoke wakiwa katika nguo zisizovutia, wasiwe wamejipamba au kujitia manukato. Wanawake walio katika hedhi wasiingie msikitini au sehemu ya kusalia; wanaweza kungojea ndani ya gari, kwa mfano, ambapo wanaweza kusikia khutbah.

ADAAB ZA 'IYD

Kukoga

Moja ya heshima za Eid ni kukoga kabla ya kwenda katika sala. Imeripotiwa katika ripoti sahihi katika al-Muwatta’ na kwengineko kuwa ‘Abd-Allaah ibn ‘Umar alikuwa akikoga siku ya al-Fitr kabla ya kuja pahala pa kusalia. (al-Muwatta’428)

Imeripotiwa kuwa Sa'iyd ibn Jubayr alisema "Mambo matatu ni Sunnah siku ya Eid;  kwenda kwa miguu   katika uwanja wa kusali (Mswallah), kukoga, na kula kabla ya kutoka nje"  . Hivi ndivyo alivyosema Sa'id ibn Jubayr na labda amejifunza haya kutoka kwa baadhi ya maswahaaba.

An-Nawawi (RA) ametaja kuwa wanavyuoni wamekubaliana kuwa imependekezwa (mustahaab) kukoga kabla ya sala ya Eid.

Sababu ya kuwa ni mustahaab kukoga kabla ya sala ya Ijumaa na mikusanyiko mengine pia inahusika katika suala la Eid vilevile.

Kula kabla ya kutoka

Mtu asitoke kwenda pahala pa kusalia Eid al-Fitr kabla ya kula tende, kwa sababu ya hadiith iliyosimuliwa na al-Bukhari kutoka kwa Anas ibn Maalik ambaye amesema:

"Mtume (SAW) alikuwa hatoki asubuhi ya Eid Al Fitr mpaka ale tende na alikuwa kila kwa hesabu ya witri. (odd)

  (al-Bukhaari, 953)

Imependekezwa (mustahaab) kula kabla ya kutoka kwa sababu hii inahakikisha kuwa hatukuruhusiwa kufunga katika siku hiyo, na ni onyesho kuwa saumu sasa imemalizika. Inb Hajar (RA) ameeleza kuwa hii ni kwa ajili ya kuwakinga watu kuendeleza saumu na pia inamaanisha utii kwa Allaah (SWT).(Fath, 2/446).

Iwapo mtu hatakuwa na tende, anaweza kufutari kwa chochote kilichoruhusiwa. Kwa upande mwengine, katika Eid al-Adh’haa, imependekezwa mtu asile mpaka baada ya sala, ambapo mtu anatakiwa kula nyama ya mnyama mmojawapo aliyechinjwa (kwa ajili ya siku hii).

Takbira (Allaahu Akbar) katika siku ya 'Iyd

Hii ni moja ya sunnah kubwa kabisa ya siku hii, kwa sababu ya maneno ya Allaah (yenye tafsiri):

"......Mwenyezi Mungu anakutakieni yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo mazito, na mtimize hiyo hisabu, na mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa kuwa amekuongoeni ili mpate kushukuru"

 al-Baqarah 2:185].

Ad-Daaraqutni na wengine wameripoti kuwa wakati Ibn ‘Umar alipokuwa akitoka katika Eid al-Fitr na al-Adh’haa, huwa anajitahidi kutoa Takbiir mpaka anapofika pahala pa kusalia, kisha kuendelea na Takbiir mpaka aje imaam.

Tendo la kutoa Takbiira kutoka nyumbani hadi pahala pa kusalia, na mpaka imaam aingie, ni maarufu miongoni mwa salaf na limeripotiwa na waandishi wengi kama Ibn Abi Shaybah, ‘Abd al-Razzaaq na al-Firyaabi katika kitabu chake Ahkaam al-‘Eidayn kutoka katika kundi la salaf. Moja ya mfano wake ni ripoti kuwa Naafi’ ibn Jubayr alikuwa akitoa Takbiira na alikuwa akishangaa kwa nini watu hawafanyi hivyo. Alikuwa akiwaambia watu, "Kwa nini hamfanyi Takbiir? Ibn Shihaab Al Zuhri kasema, "Watu walikuwa wakifanya takbiir kuanzia wakati wanapotoka majumbani mwao hadi anapoingia imaam".  

Wakati wa kutoa Takbiira katika Eid al-Fitr unaanza usiku wa kuamkia Eid mpaka wakati imaam anapofika kuongoza sala.

Maneno ya Takbiira

Ibn Abi Shaybah ameripoti katika al-Musannaf kuwa Ibn Mas’uud (RA) alikuwa akitamka takbira katika siku za Tashriiq kama ifuatavyo: “Allaahu akbar, Allaahu akbar, laa ilaaha ill-Allaah, wa Allaahu akbar, Allaahu akbar wa Lillaahi’l-hamd (Allaah ni Mkubwa kabisa ….hakuna Mungu isipokuwa Allaah, Allaah ni Mkubwa kabisa, na sifa zote njema ni za Allaah)’. Ibn Abi Shaybah aliripoti haya mahala pengine katika isnaad hiyo hiyo, lakini ikiwa na pamoja na maneno “Allaahu Akbar” ikirejewa mara tatu.

Al-Muhaamili pia ameripoti kuwa Ibn Mas’uud alikuwa akisema : “Allaahu akbar kabiiran, Allaahu akbar kabiiran, Allaahu Akbar wa ajall, Allaahu Akbar wa Lillaahi’l-hamd (Allaah ni Mkumbwa kabisa, Allaah ni Mkubwa kabisa, Allaah ni Mkubwa kabisa, Allaah ni Mkubwa kabisa na Mtukufu, na sifa zote njema ni za Allaah)”. (al-Irwaa’, 3/126).

Kupongezana

Watu wanaweza kupeana pongezi na salaam njema za Eid, bila ya kujali aina ya maneno. Mfano wanaweza wakaambizana, “Taqabbal Allaah Minnaa Wa Minkum (Allaah azikubali [ saumu na ibada] zetu na zenu” au “Eid mubarak” na mfano wa hayo katika salaam zilizoruhusiwa.

Tendo la kupeana salamu limekuwa maarufu wakati wa Masahaaba na wanavyuoni kama Imaam Ahmad na wengine wameruhusu hilo. Kuna ripoti zinazoonyesha imeruhusiwa kuwapongeza watu katika matukio maalum. Masahaaba walikuwa wakipongezana wakati linapotokea jambo zuri, mfano pale Allaah alipokubali toba ya mtu n.k.

Hakuna shaka kuwa kumpongeza mtu kwa namna hii ni moja kati ya namna ya heshima zaidi katika tabia njema na ni moja kati ya muamala mzuri sana wa jamii ya Waislam.

Kuvaa vizuri zaidi siku ya 'Iyd

'Abdullah ibn 'Umar (RA) amesema, 'Umar alichagua jubbah (nguo refu inayovaliwa juu ya kanzu) ambayo ilitengenezwa kwa hariri na ilikuwa ikiuzwa kwa bei ya takhfifu sokoni, aliileta kwa Mtume (SAW) na akasema, "ewe Mtume nunua hii na uvae kwa ajili ya Eid na watakapokuja wageni"  Mtume (SAW) akasema "Hizi ni nguo za yule ambaye hana sehemu akhera (imeripotiwa na Al-Bukhaari 948)

Mtume (SAW) alikubaliana na mawazo ya ‘Umar ya mtu kuvaa vizuri zaidi, lakini alikataa na kupingana na mawazo ya kununua jubbah hilo kwa sababu lilikuwa limetengenezwa kwa hariri.  

Al-Bayhaqi ameripoti kuwa Ibn Umar alikuwa akivaa nguo zake nzuri siku ya Eid, kwa hivyo wanaume wanatakiwa wavae nguo nzuri zaidi walizokuwa nazo wanapotoka kwa ajili ya Eid.

Kwa upande mwengine, wanawake, wajiepushe na mapambo wanapotoka kwa ajili ya Eid, kwa sababu wao wamekatazwa kuonyesha mapambo yao mbele ya wanaume wasio mahrim zao. Mwanamke anayetaka kutoka ameharamishiwa kujitia manukato au kujionyesha kwa njia ya kushawishi mbele ya wanaume, kwa sababu yeye ametoka kwa ajili ya ibada tu. Je, unafikiria kuwa ni sahihi kwa mwanamke muumini kumuasi Yule Ambae yeye (mwanamke) anatoka kwenda kumuabudu, na kwenda kinyume na amri Zake kwa kuvaa nguo za kuvutia zenye kumbana na za rangi zinazong’ara au kujitia manukano n.k?

Sheria katika kusikiliza khutba za 'Iyd

Ibn Qudaamah (RA) amesema katika kitabu chake cha al-Kaafi (p.234):

Imaam anapotoa salaam (mwisho wa Swalah) atoe khutba sehemu mbili kama khutba ya Ijumaa kwa sababu Mtume (SAW) alifanya hivyo.  Khutba ya Eid ni tofauti  na khutba ya Ijumaa kwa mambo manne, jambo la nne ambali ni Sunnah na sio fardhi kusikiliza kwa sababu imeripotiwa kwamba 'Abdulla bin Al-Saa'ib alisema, "Nilihudhuria Eid na Mtume (SAW)  na alipomaliza kuswali, alisema "tutatoa khutba sasa kwa hiyo anayependa kukaa (na kusikiliza) akae na yeyote anayetaka kuondoka basi na aondoke".   

Katika al-Sharh al-Mumti’  ‘ala Zaad al-Mustanfi’ cha Ibn ‘Uthahymiin, 5/192, kinasema:

“Maneno [ya Ibn Qudaamah], ‘kama khutbah mbili za Ijumaa’ inamaanisha kuwa anatakiwa atoe khutbah mbili, hata kama kuna kutokubaliana katika jambo hili, kama ambavyo tumetaja hapo juu. Khutba ya Eid, imeegemea katika  sheria zilizo sawa na za Ijumaa, hata katika nukta ya kuzumgumza wakati wa khutba hiyo ni haraam, lakini sio wajibu kuhudhuria, hali ya kuwa kuhudhuria khutba ya Ijumaa ni wajibu, kwa sababu Allaah (SWT) Amesema

(maana ya maneno hayo):

"Enyi mlio amini! Ikiadhiniwa Sala siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu, na wacheni biashara"

Al-Jumu'aa :9

 Kuhudhuria khutba ya Eid sio wajibu, na mtu anaruhusiwa kuondoka, bali iwapo atabakia, ni lazima asizungumze na yeyote. Hivi ndivyo muandishi alivyokusudia aliposema ‘kama khutba mbili za Ijumaa’. “

Mmoja wa wanavyuoni amesema: “Si wajibu kusikiliza khutba za Eid, kwa sababu kama ingelikuwa ni wajibu kuzihudhuria na kuzisikiliza basi ingekuwa ni haraam kuondoka. Lakini kwa kuwa imeruhusiwa kuondoka, basi si wajibu kusikiliza”.

Hata hivyo, iwapo mazungumzo yatawakera wale wanaosikiliza, ni haraam kuzungumza kwa sababu ya kero hizo, sio kwa sababu ya kutokusikiliza. Kwa msingi huu, iwapo mtu atakuwa na kitabu wakati imaam anakhutubia, basi ameruhusiwa kukisoma, kwa sababu kufanya hivyo hakutomkera yeyote. Lakini kwa mujibu wa madh’hab anayofuata muandishi huyu, ni wajibu kusikiliza khutba hiyo iwapo utakuwepo (hapo pahala pa kusalia).

Mtu kutoka kwa  njia moja na kurudi kwa kutumia njia nyengine

Jabir ibn ‘Abd-Allah (RA) ameripoti kuwa Mtume (SAW) alikuwa akibadilisha njia siku ya Eid. (imeripotiwa na al-Bukhari, 986)

Imeripotiwa kuwa Mtume (SAW) alikuwa akitoka kwa miguu, na alikuwa akisali bila ya adhana wala iqaamah, kisha hurudi kwa kutumia njia nyengine tofauti. Inasemekana kuwa njia hizi mbili zitamtolea ushahidi siku ya Kiyama, kwa sababu siku hiyo ardhi itasema juu ya kila kitu kilichofanywa juu yake, zuri na baya. Vile vile inasemekana kuwa imefanywa hivi ili kuonyesha alama na utamaduni wa Kiislam katika njia zote mbili; kutoa ukumbusho wa Allah; kuwavunja moyo wanafiki na  Mayahudi na kuwaogopesha kwa wingi wa watu walio pamoja nae; kutimiza mahitaji wa watu kwa kuwapa fatwa, kuwasomesha na kuwawekea mifano ya kuifuata; kuwapa sadaka wale wanaohitajia; au kuwatembelea jamaa zake na kukuza mahusiano yao.

Tahadhari juu ya kufanya maovu

1.     Baadhi ya watu wanadhani kuwa Uislam unatuambia kukesha na kusali usiku wa Eid, kwa kunakili hadithi ya uongo inayosema "Yeyote atakayekesha usiku wa Eid moyo wake hautokufa siku ya kufa moyo wake"  Hadithi hii imeripotiwa katika isnaad mbili moja ambayo ni dhaifu na ya pili ni dhaifu sana.  

     Uislam hautuambii kuutenga usiku wa Eid kwa kukesha na kusali; hata hivyo, iwapo mtu ana tabia ya kuamka na kusali usiku (qiyaam), hakuna ubaya wa kufanya hivyo katika usiku wa Eid pia.

2.      Mchanganyiko wa wanawake na wanaume katika maeneo ya sala, mitaani, n.k. Inasikitisha kuwa haya yanatokea sio misikitini tu, bali hata katika sehemu tukufu zaidi, al-Masjid al-Haram [Makkah]. Wanawake wengi, Allaah Awaongoze  wanatoka wakiwa hawajajisitiri, wamejipamba na kujitia manukato, wanaonyesha mapambo yao, wakati kuna mkusanyiko mkubwa katika msikiti huo. Hatari ya hali hii iko wazi kabisa. Kwa hiyo wale wahusika ni lazima wapange sala za Eid vizuri, kwa kuweka milango tofauti na njia tofauti kwa wanawake na wawacheleweshe wanaume kutoka mpaka wanawake wawe wameshatoka.

3.      Baadhi ya watu wanajikusanya siku ya Eid kwa ajili ya kuimba na kufanya aina nyengine za ….burudani, na hii haikuruhusiwa.

4.      Baadhi ya watu wanashereheka katika Eid kwa sababu Ramadhani imemalizika na kuwa hawahitajiki tena kufunga. Haya ni makosa, waumini wanasherehekea Eid kwa sababu Allaah Amewasaidia wao kumaliza mwezi wa saumu, sio kwa sababu ya kumalizika kwa saumu ambayo watu wengine wanaichukulia kuwa ni mzigo.

Tunamuomba Allaah azikubali ibada zetu na toba zetu. Allaah Ampe rehma Mtume wetu Muhammad.