Mtume (SAW) ameifanya kazi yake kwa ukamilifu
na ameufikisha ujumbe kwa watu kama alivyotakiwa.
Wakati mwingine alikuwa akiwaendea watu maalum au
huwaalika watu chakula, na mara nyengine hujitolea kuyaendea makabila mbali
mbali huku akiwa na subira juu ya yale yanayomkuta, na kabila moja baada ya moja
humkatalia. Wakati mwingine huwaita watu ili akutane nao au huwaendea pale
walipo, na mara nyingine huwatuma walinganiaji katika sahaba zake, na mara
nyingine hutuma wajumbe kwa wafalme na ma gavana, mara nyingine hupigana Jihadi
dhidi ya wale wanaowazuia watu kuilingania njia ya MwenyeziMungu.
Makafiri walipambana na uenezi huu pamoja na
waenezaji kwa kila namna ya ukatili, nguvu na udhia.
Maqureish wakati mwingine walikuwa wakiwafanyia
mzaha Mtume (SAW) na sahaba zake (RA), kisha ghafla wanawavamia baadhi ya
Waislamu na kuwaunguza kwa moto, kuwauwa au kuwaadhibisha. Waliwapiga pande
Waislamu na kuwazunguka wakiwemo katika nyumba za Abu Talib kwa muda wa miaka
mitatu, hata iliwabidi Waislamu wale ngozi na miti. Udhia ukazidi na Masahaba wa
Mtume(SAW) ikawabidi wahame na kukimbilia Uhabeshi (Ethiopia) mara mbili, kisha
wakahamia Madina.
Maqureish wakafanya njama ili wamuuwe Mtume wa
MwenyeziMungu(SAW), lakini MwenyeziMugu akamwamrisha ahame ili aokoke na hila
zao.
Alikuwa akiwaelezea watu yote aliyotakiwa na
MwenyeziMungu ayaeleze. Alitujulisha hata yale yaliyo na makatazo kwake yeye
binafsi kutoka kwa MwenyeziMungu:
Mfano wa kauli ya MwenyeziMungu:
"Alikunja (Mtume ) paji na akageuza uso.
Kwa sababu alimjia kipofu.
Na nini kilichokujulisha (ya kuwa huyo Sahaba pofu
hahitaji mawaidha mapya?) Labda yeye atatakasika (kwa kusikia mawaidha mapya).
Au atakumbuka (aliyoyasahau). Ukukmbusho huo upate
kumfaa.
Ama ajionaye hana haja (ya dini).
Wewe ndie unayemshughulikia?
Na si juu yako kama hakutakasika.
lakini anayekukimbilia.
Naye anaogopa.
Wewe unampuuza (Usifanye hivyo)".
(Abasa -1-10).
Aliambiwa haya kwa sababu Mtume(SAW) alipokuwa
akiwalingania baadhi ya viongozi wa makafiri alijiwa na kipofu Mwislamu aitwae
Ibn Ummi Maktoum akimuuliza masuali, na Mtume (SAW) alichukizwa kwa kuulizwa
masuali wakati alipokuwa akijaribu kuwasilimisha wakubwa wa makabila ambao
wangelisilimu wao pamoja na wafuasi wao ingepatikana kheri kwa Waislamu.
Mtume (SAW) hakumfanyia lolote la zaidi kipofu
huyo isipokuwa alikunja uso wake tu. Na Ibn Ummi Maktoum kwa vile ni kipofu,
hawezi kuuona uso wa Mtume (SAW) ulokunjwa na kwa hivyo hakuudhika.
Lakini MwenyeziMungu akamteremshia Mtume(SAW)
makatazo, na akayafikisha makatazo hayo kama yalivyoteremshwa.
Lengo la Mtume (SAW) katika maisha yake yote
lilikuwa ni kuyafikisha yale aliyoamrishwa na Mola wake bila ya kujali ukubwa wa
taabu au vikwazo atakavyopambana navyo.
Katika Hijja yake ya mwisho (Hijjatul Wadaa)
aliwauliza Waislamu;
"Je! nimefikisha?"
Wakashuhudia kuwa amewafikishia kikamilifu dini ya
MwenyeziMungu;
Kisha akasema:-
"MwenyeziMungu shuhudia".
Hakika ya hali
yake ilivyokuwa katika kila nyanja ya maisha yake inashuhudia kuwa sifa kama
hizi hawezi kuwa za mtu wa aina nyingine isipokuwa ni sifa za Mtume wa
MwenyeziMungu (SAW) na mjumbe Wake.