|
Sifa zote njema anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa
walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu
Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)
na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema
mpaka Siku ya Mwisho.
Kutokana na Hadithi ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa
aalihi wa sallam):
(( من صام رمضان ثم أتبعه ستًّا من شوال كان كصيام الدهر))
أرجه مسلم في صحيحه،
((Atakayefunga Ramadhaan kisha
akafuatiliza na siku sita za mwezi wa Shawwaal' itakuwa kama
ni funga ya mwaka)) [Muslim]
Inavyompasa Muislamu ni
kwamba anatakiwa kwanza alipe deni lake la Ramadhaan kisha
ndio afunge 'sitatu Shawwaal' ili aweze kupata
thawabu za kama kafunga mwaka mzima. Na maulamaa wameona
hivyo ni kutokana na dalili zifuatazo katika Qur-aan
na Sunnah:
Katika Qur-aan:
Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((مَن جَاء بِالْحَسَنَةِ فَلَهُ عَشْرُ أَمْثَالِهَا وَمَن
جَاء بِالسَّيِّئَةِ فَلاَ يُجْزَى إِلاَّ مِثْلَهَا وَهُمْ
لاَ يُظْلَمُون))
((Afanyae wema atalipwa mfano wake
mara kumi. na afanyae ubaya hatalipwa ila sawa nao tu. Na
wao hawatadhulumiwa))
[Al-An'aam:160]
Katika Sunnah:
Kuna Hadiyth mbali mbali
zinazothibitisha kauli hiyo ya Allaah (Subhaanahu Wa
Ta'ala), tutazitaja hapa mbili:
Ya kwanza ambayo kutokana na Imaam At-Tirmidhiy kuwa ni
sababu ya kuteremshwa Aayah hiyo:
((من
صام ثلاث أيام من كل شهر فقد صام الدهر كله))
((Atakayefunga siku tatu katika
mwezi atakuwa amefunga mwaka mzima)) [Ahmad,
An-Nasaaiy, Ibn Maajah, At-Tirmidhiy]
Hadiyth ya pili:
((إن الله كتب الحسنات والسيئات , ثم بين ذلك , فمن هم بحسنة
فلم يعملها كتبها الله له عنده حسنة كاملة فإن هو هم بها
فعملها كتبها الله له عنده عشر حسنات , إلى سبعمائة ضعف , إلى
أضعاف كثيرة , ومن هم بسيئة فلم يعملها , كتبها الله عنده حسنة
كاملة , فإن هو هم بها فعملها كتبها الله له سيئة واحدة ))
متفق عليه ،
((Allah Ameandika mema na mabaya.
Kisha Akayabainisha. Basi atakayetia nia kutenda jema kisha
asilifanye, ataandikiwa jema moja kamili. Atakapofanya hima
na akalitenda, ataandikiwa mema kumi hadi kuzidi mia saba na
ziada nyingi. Na atakayetia nia kufanya kitendo kibaya kisha
asikifanye, ataandikiwa jema moja kamili. Atakapokifanya
ataandikiwa dhambi moja)) [Al-Bukhaariy
ya Muslim]
Kutokana na dalili hizo, kwamba kila jema mtu anapata mara
kumi, hivyo Swawm ya Ramadhaan itakuwa ni hivi:
30 x 10 = 300
Na funga ya 'sitatu
Shawwaal' itakuwa ni 6 x 10 = 60
300 + 60 = 360
Hivyo siku 360 ni sawa taqriban na mwaka mzima.
Na Allah Anajua zaidi
|