TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 » Makala na Mengineyo  

DALILI ZA KUKARIBIA KWA SIKU YA KIAMA

Mwenyezi Mungu amemleta Mtume wake Muhammad (SAW) akiwa kama ni mletaji habari njema na muonyaji ambaye hakuacha jambo lolote la kheri isipokuwa ametujulisha nalo na kutuhimiza kulikimbilia, na hakuacha jambo lolote la shari isipokuwa ametutahadharisha nalo.

Na kwa vile umma huu ni umma wa mwisho, basi Mtume huyu mtukufu (SAW) ametuletea kutoka kwa Mola wake dalili za kutosha zilizo wazi zenye kutujulisha juu ya kukaribia kwa Siku ya Kiama na yeye akatubainishia kwa ulimi wake tena kwa ufasaha kabisa juu ya baadhi ya yatakayotokea katika mwisho wa zama na akatuhakikishia kuwa yote hayo lazima yatatokea, haya yote yakiwa ni dalili juu ya ukweli wa utume wake (SAW) utakayowafanya watu wajitayarishe vizuri na Siku hiyo, siku ambayo mtu hatovuna isipokuwa kile alichochuma, na hatokuwa na wakumlaumu isipokuwa nafsi yake.

Mwenyezi Mungu anasema;

“Isije ikasema nafsi (asije akasema mtu); “Eee majuto yangu kwa yale niliyopunguza upande wa Mwenyezi Mungu, na hakika nilikuwa miongoni mwa wanaoyafanyia mzaha (mambo ya dini)”.

Au ikasema; “Kama Mwenyezi Mungu angeniongoa bila shaka ningekuwa miongoni mwa wenye kumcha Mwenyezi Mungu”.

Au ikasema ionapo adhabu; “Kama ningepata marejeo  (ya kurejea tena duniani) ningekuwa miongoni mwa wafanyao mema”.

(Ataambiwa)’ “Kwa yakini! Bila shaka zilikujia Aya (dalili) zangu ukazikadhibisha na ukajivuna na ukawa miongoni mwa wanaotakabari”.

Az Zumar – 56-59

 

Katika kuzijuwa dalili hizo kisha kuziona zikitendeka hapa duniani kunampatia mtu faida nyinigi sana zikiwemo zifuatazo;

·        Kuwa na uhakika juu ya ukweli wa utume wake Muhammad (SAW).

·        Kujitayarisha vizuri na Siku ya Kiama. Kwani mtu kwa mfano anapopewa habari juu ya meli inayokaribia kuwasili bandarini, huingoja meli hiyo huku akiwa na wasi wasi mwingi, lakini anapoisika sauti ya selo ya meli hiyo anakuwa na uhakika usio na shaka kuwa meli sasa imekaribia kweli kuwasili.

Mfano huu ni sawa na mtu aliyejulishwa juu ya dalili ya kukaribia kwa Siku ya Kiama, kisha akaziona dalili hizo zikitendeka mbele ya macho yake kama zilivyoelezwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW). Mtu huyo anakuwa na uhakika usio na shaka wa kuwepo kwa siku ya Kiama.

·        Kwa ajili hiyo, kuzijuwa na kuziona dalili za kukaribia kwa Siku ya Kiama kunaongeza pia yakini juu ya ukweli wa kukaribia kwa Siku hiyo.

·        Kunamsaidia mtu kutoyumbishwa na masaibu, mitihani na machafuko yanayotekea kila siku, kwani akirudi katika mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) ataona kuwa yoote hayo yamekwishatajwa kuwa yatakuja kutokea.

·        Kunamsaidia mtu aliyejisahau akawa anaikimbilia dunia, anapoziona dalili hizo zikitokea kikweli humkumbusha mtu huyo akawa anaifanyia kazi akhera yake badala ya kuikimbilia dunia.

Kutokana na haya na mengi mengineyo, Mwenyezi Mungu akamfunulia Mtume wake (SAW) baadhi ya dalili ya yale yatakayotokea kabla ya kuja kwa Siku ya Kiama.

 

Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) alikuwa anapozungumza juu ya dalili za kukaribia kwa Siku ya Kiama, mashavu yake yanageuka kuwa mekundu huku akiipaza sauti yake juu kwa ghadhabu mfano wa amri jeshi mwenye kulipa amri jeshi lake.

Alikuwa pia akisema;

“Nimeletwa baina yangu na Kiama kiasi kama hiki”, huku akiashiria kwa kidole chake cha shahada na cha pili yake.

Zipo dalili zinazoitwa ‘dalili ndogo’ na zipo pia ‘dalili kubwa’ za Siku ya Kiama. Nyingi katika dalili ndogo zimekwisha tokea na kuonekana, jambo lililowafanya Waislamu waongezeke imani na kumsadiki zaidi Mtume wao (SAW), na zitakapoanza kuonekana dalili kubwa, basi zitatunga na kufuatana moja baada ya nyingine mpaka Kiama kitakaposimama. Lakini sisi tutazitaja hapa baadhi chache sana za ‘dalili ndogo’ tu.

 

FITAN

Neno ‘Fitan’ ambalo ni wingi wa (plural ya) Fitna, maana yake ni Mitihani. Lakini neno hili linaongezeka maana yake kila linapozidi kutumika, kwani neno hili linaweza kumaanisha misiba, madhambi, kufru, mauaji, kuchomwa moto nk.

Neno ‘Fitan’ pia linamaanisha vita vya wenyewe kwa wenyewe (civil war)

Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) ametujulisha juu ya Fitna nyingi sana zitakazotokea baada yake zikiwa kama ni dalili ya kukaribia kwa Siku ya Kiama. Fitna zitakazomfanya mtu asiweze kutambua ipi haki na ipi batil. Fitna zitakazozitetemesha nyoyo na kuiyumbisha imani hata mtu anaweza akaamka asubuhi akiwa ni Muislamu na jioni yake akageuka kuwa kafiri, au anaweza kuamka asubuhi akiwa kafiri na jioni yake akawa Muislamu.

Kila inapotokea fitna, mtu hudhani kuwa hii ndiyo itakayoangamiza, kisha humalizika na kutokea nyingine kubwa kuliko ile. Na hali itaendelea hivyo mpaka kitakaposimama Kiama.

Anasema Abu Musa Al Ashary (RA) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Kinapokaribia Kiama zitatokea Fitna nyingi mfano wa vipande vya usiku wenye kiza kizito, mtu ataamka ndani yake akiwa Muislamu na jioni yake anakuwa kafiri, au anakuwa wakati wa jioni Muislamu na asubuhi anakuwa kafiri. Aliyekaa katika mtihani huo anakuwa bora kuliko aliyesimama na aliyesimama anakuwa bora kuliko mwenye kutembea taratibu na mwenye kutembea anakuwa bora kuliko anayekwenda mwendo wa kukazana”.

Imam Ahmed na Ibni Majah na Al Hakim na wengineo.

 

Imetolewa na Muslim pia kutoka kwa Abu Huraira (RA) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Kimbilieni kufanya amali njema kabla ya kuja kwa Fitna mfano wa vipande vya usiku wenye kiza kizito, mtu ndani yake anaamka akiwa Muislamu na jioni yake anakuwa kafiri, au jioni anakuwa kafiri na asubuhi anakuwa Muislamu. Mtu ndani ya fitna hizo anaiuza dini yake kwa thamani ndogo ya dunia.”

Muslim

 

Na maana ya neno ‘vipande vya usiku wenye kiza kizito’, ni ule ubaya wa Fitna hizo utakaomfanya mtu achanganyikiwe asiweze kutambua baina ya haki na batil.

 

Kutoka kwa Ummu Salamah (RA) amesema kuwa usiku mmoja Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) aliamka akiwa na hofu nyingi huku akisema;

“Subhana llah! Hazina ngapi aloteremsha Mwenyezi Mungu, na mitihani mingapi aloteremsha Mwenyezi Mungu? Nani atakayewaamsha waliolala vyumbani mwao (akimaanisha wake zake) huenda mtu akawa amevaa duniani akenda uchi akhera”.

Maulamaa wamelitafsiri neno ‘amevaa duniani akenda uchi akhera’, tafsiri nyingi sana zikiwemo zifuatazo;

·        Mtu tajiri mwenye nguo nyingi hapa duniani lakini hana amali njema za kumsitiri huko akhera.

·        Wengine wakasema kuwa maana yake ni mtu mwenye kuvaa nguo

zisizomsitiri hapa duniani na huko akhera hatokuwa na cha kumsitiri.

 

KUVUNJWA KWA MLANGO

Nitaanza kwa kutaja baadhi ya hadithi alizozungumzia ndani yake Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) fitna za mwanzo katika Uislamu, fitna zilizotokea miaka michache baada ya kufariki kwake, mara baada ya kuuliwa kwa Khalifa wa pili wa Waislamu Omar bin Khattab (RA).

Katika Bukhari na Muslim na Attirmidhiy kutoka kwa Hudhaifa (RA) amesema kuwa Omar bin Khattab (RA) aliuliza siku moja;

“Yupi kati yenu aliyehifadhi kauli ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) juu ya Fitna?”

Hudhaifa akasema;

“Mimi nimehifadhi kama alivyosema”.

Omar (RA) akamwambia;

“Tuhadithie, kwani wewe ni jasiri”.

Hudhaifa (RA) akasema;

“Fitna ya mtu katika ahli yake (watu wa nyumba yake) na mali yake na jirani zake zinaondoka kwa kusali na kutoa sadaka na kwa kuamrisha mema na kukataza mabaya”.

Omar akasema;

“La, mimi sikusudii (fitna) hizi, bali zile zinazorusha mawimbi (makubwa) kama mawimbi ya bahari’.

Akasema;

“Ewe Amiri wa Waislamu! Wewe umeepukana nazo fitna hizo, kwani baina yako na baina yake (fitna hizo) upo mlango uliofungwa”.

Omar akauliza;

“Mlango huo utafunguliwa au utavunjwa?”

Akasema;

“La, bali utavunjwa”.

Omar (RA) akasema;

“Kwa hivyo hautofungika tena….”

Na katika riwaya nyingine akasema;

“Kwa hivyo hautofungika mpaka Siku ya Kiama?”

Wakamuuliza (waliokuwa wakimsikiliza Hudhaifa baada ya kufa kwa Omar);

“Aliujuwa?”

Na katika riwaya nyingine;

“Omar alikuwa akiujuwa mlango huo?”

Hudhaifa (RA) akawaambia;

“Naam kama (anavyojuwa kuwa) usiku wa leo unakuja kabla ya usiku wa kesho).”

Masruq bin Al Ajda-a alipomuuliza Hudhaifa(RA);

“Nani mlango huo”.

Akasema;

“(Mlango huo ni) Omar.”

Kisha Hudhaifa (RA) akawaambia;

“Mimi nilimuhadithia Omar hadithi (hii) kama nilivyomsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) bila makosa.”

 

Ikawa kama alivyotujulisha Msemakweli Muhammad (SAW), kwani mlango huo ulivunjwa mara baada ya kuuliwa Khalifa wa pili wa Waislamu Omar bin Khattab (RA) na kuanzia hapo fitna zikafunguka na kuenea na kukithiri, na fitna ya mwanzo ilikuwa kuuliwa kwa Khalifa wa tatu wa Kiislamu Mwenye Nuru mbili Othman bin Affan (RA).

 

KUULIWA KWA OTHMAN (RA)

Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) aliwahi kumbashiria Othman bin Affan (RA) kuwa atakumbwa na mtihani mkubwa.

Kisa chenyewe ni kama ifuatavyo;

Katika hadithii iliyosimuliwa na Bukhari, anasema Abu Musa Al Ash ary(RA) kuwa siku moja alimuona Mtume(SAW) akielekea katika kisima kilichozungushiwa ukuta.

Abu Musa Al Asha-ary anasema;

“Nikasema; Leo mimi nitakuwa mlinzi wa Mtume(SAW). Nikamuona Mtume(SAW) akielekea kisimani, akakidhi haja yake kisha akakaa juu ya kisima huku akining’iniza miguu yake.

Akaja Abubakar akataka ruhusa ya kuingia ndani, nikamwambia; “Hapo hapo ulipo, ngoja kwanza usiingie mpaka nikakuombee ruhusa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW)”.

Nikamwendea Mtume(SAW) na kumwambia;

“Abubakar anataka ruhusa ya kuingia”,

Akanambia;

“Mruhusu aingie, na mbashirie Pepo”.

Nikafanya hivyo, akaingia na kukaa juu ya kisima kuliani kwa Mtume(SAW) na kuining’iniza miguu yake kama alivyofanya Mtume(SAW).

Mlango ukagongwa tena. Nikatamani mgongaji awe ndugu yangu.

Nikauliza;

“Nani?”

“Omar bin Khattab”,

Nikamwambia;

“Hapo hapo ulipo, usiingie mpaka kwanza nimjulisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW)”.

Mtume(SAW) akanambia;

“Mruhusu aingie, na mbashirie Pepo”.

Nikafanya hivyo, na Omar naye akaingia na kukaa juu ya kisima kushotoni kwa Mtume(SAW) na kuining’iniza miguu yake kama walivyofanya wenzake.

Haujapita muda mlango ukagongwa tena; Nikatamani mgongaji awe ndugu yangu.

“Nani?”

“Othman bin Affan”.

Nikamwambia; “Hapo hapo ulipo, usiingie mpaka kwanza nimjulishe Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW)”.

Nilipomjulisha, Mtume (SAW) akanyamaza muda kidogo, kisha akanambia;

“Mruhusu aingie na mbashirie Pepo baada ya kupambana na mtihani mkubwa”.

Nilipomwambia hivyo, Othman akasema;

“Allahu l Mustaan”, (na katika riwaya nyingine alisema ; “Tutakuwa na subira Inshaallah”), kisha akaingia, lakini Othman hakupata pa kukaa, akenda upande wa pili akakaa akiwa amekabiliana nao.

Anasema Abi Musa(RA);

“Nikahisi kama hivi ndivyo makaburi yao yatakavyokuwa, na nikatamani ndugu yangu naye aje”.

Bukhari

Ingawaje Omar bin Khattab (RA) aliuliwa kama alivyouliwa Othman (RA), lakini Omar aliyeuliwa na kafiri anayeabudu moto wakati akisalisha Sala ya Alfajiri hakupata misukosuko kama aliyopata Othman (RA) kabla ya kuuliwa kwake.

Baada ya kuuliwa Othman (RA) fitna zikawa nyingi, khitilafu zikaongezeka, hata Masahaba (RA) walishiriki katika vita vya wenyewe kwa wenyewe.

 

MNAYAONA NINAYOYAONA MIMI?

Siku moja alipokuwa akisimamia ujenzi wa ngome katika mji wa Madina Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) aliyekuwa akiyajuwa yote hayo kuwa yatatokea, aliwauliza Masahaba wake;

“Mnaona ninayoyaona?”

Masahaba (RA) wakasema;

“Hatuoni (kitu) ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu.”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) akasema;

“Mimi naona mapigano mengi yakitokea baina ya nyumba zenu, wingi wa   

nyumba kubwa kubwa (zinazowakusanya watu wengi ndani yake).”

 

FITNA ZITOKAZO UPANDE WA MASHARIKI

Fitna nyingi zilizowakumba Waislamu zilitokea upande wa Mashariki ya dunia, na fitna ya mwanzo iliyoleta mfarakano baina ya Waislamu ilitokea upande huo wa Mashariki, jambo ambalo bila shaka lilimfurahisha sana shetani.

Na haya yanakubaliana na maneno ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) aliyetujulisha kuwa huko ndiko kwenye pembe ya Shetani.

Kutoka kwa Ibni Omar (RA) amesema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema huku akiashiria upande wa Mashariki;

“Fitna ipo huku, Fitna ipo huku, kutakapotokeza pembe  ya shetani”.

Bukhari na Muslim

Habari hizi alizotujulisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) zilianza kuonekana tokea mwanzo wakati yalipotokea mapigano ya wenyewe kwa wenyewe jambo ambalo bila shaka yoyote lilimfurahisha sana shetani.

Anasema Sheikh Yusuf bin Abdullah Al Wabil kuwa;

“Kutoka upande wa mashariki Fitna nyingi sana zilitokea, kwani huko ndiko yalipoanza mapigano ya wenyewe kwa wenyewe baina ya Waislamu, kutoka huko umekuja ukadiani, ukoministi. Tataar pia wametokea huko katika karne ya saba ya Hijri wakaangamiza na kueneza shari kubwa sana”.

“Hadi hii leo”, anaendela kusema Sheikh Yusuf; “Fitna zinaendelea kutujia kutokea upande huo wa Mashariki ya dunia na hata Yajuju wa Majuju watatokea upande huo huo”.

 

KUPOTEA KWA AMANA

Kutoka kwa Abu Hurairah (RA) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Uaminifu utakapoondoka basi isubirini saa (kingojeeni Kiama)”.

Akaulizwa;

“Vipi unapotea (uaminifu) ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?”

Akasema;

“Mambo yakiegemezwa kwa wasiostahiki, basi isubirini saa”.

Bukhari – Kitabul Riqaaq

 

Mtume (SAW) akatubainishia pia kuwa uaminifu utatoweka katika nyoyo na kubaki athari yake tu.

Imepokelewa kutoka kwa Hudhaifa (RA) kuwa amesema;

“Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amenihadithia mambo mawili, na mojawapo katika hayo nimekwishaliona likitokea na ninalisubiri la pili (nilione pia). Amenihadithia kuwa uaminifu utatoweka. Amenihadithia kuwa amana (ilipoteremshwa), iliteremshwa ndani ya mizizi ya nyoyo za watu, kisha iilipoteremshwa Qurani wakaijuwa zaidi, kisha wakaijuwa (vizuri zaidi) kupitia katika Sunnah (Mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW)).

Kisha akatuhadithia juu ya kunyanyuliwa (kupotea) kwa amana akasema;

“Mtu analala usingizi huku amana inafutwa moyoni mwake na kubaki athari yake tu, mfano wa doa lisilokuwa na rangi. Kisha analala usingizi (mwingine) na amana inafutwa (‘tena’ - yaani hilo doa lililobaki) kisha itabaki amana mfano wa alama (ya ngozi iliyokunjika) inayobaki mkononi  baada ya mtu kunyanyua kitu”. (inayotoweka baada ya kupita muda mdogo).(au) maumivu yanayobaki mguuni baada ya kukanyaga kijinga kidogo cha moto (pakafanya lenge lenge kisha likakauka)”.

Kisha Mtume (SAW) akasema;

“Kisha watu watakuwa wanafanya biashara na hapana hata mmoja katika yao atakayekuwa muaminifu, itafika hadi kusemwa; “Katika watu wa kabila Fulaanii yupo mtu moja muaminifu. Na hata itafika hadi watu watakuwa wakimsifia mtu huku wakisema; ‘Mwanamume kweli huyu, mkarimu kweli huyu, ana akili kweli huyu’, (atapewa sifa zote hizo) wakati mtu huyo hata imani (wala uaminifu) hata yenye uzito wa hardali ”.

Hudhaifa (RA) akaendela kusema;

“Nimekwishaiona zama ambayo ndani yake uaminifu baina ya watu ulikuwepo. Na sikuwa nikijali ninafanya biashara na nani (kwa sababu watu wote waaminifu), akiwa mtu huyo ni Muislamu basi Uislamu wake utamfanya asiipoteze amana yake. Na kama mtu huyo ni Mkristo au Myahudi, basi atakuwa anafanya kama anavyotakiwa (kutonidhulumu haki yangu). Ama wakati huu wa leo, Uaminifu umeondoka, na khiyana imedhihiri na sitofanya biashara isipokuwa na Fulani au Fulani (tu)”.

Yaani alikuwa akifanya biashara na baadhi ya watu wachache tu alokuwa akiwaamini.

Hudhaifa (RA) aliishi muda baada ya kuuliwa kwa Othman  bin Affan (RA).

Bukhari na Muslim

Anasema Sheikh Yusuf Al Wabil aliyeandika kitabu cha ‘Ashraat al Saa-a’ kuwa;

“Miongoni mwa dalili za kupotea kwa Amana ni kule kupewa ufalme, uongozi au uhakimu watu wasiokuwa waadilifu wala waaminifu, kwani viongozi wanapotengenea, raia nao hutengenea. Ama huko juu kukiharibika, basi chini nako kutaharibika pia.

Na Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amekwishatujulisha kuwa utafika wakati wa hadaa, mambo yatakapokwenda kinyume. Wakati huo, muongo ndiye atakayesadikiwa na mkweli atakadhibishwa, na muaminifu ataitwa haini na haini ndiye atakayeaminiwa”.

Kubebeshwa mzigo wa uongozi watu wasioijali dini yao, ni dalili ya watu kutojali maamrisho ya dini yao, na dalili ya upungufu wa maulamaa na kuongezeka kwa ujinga, na hizi pia ni katika dalili za kukaribia kwa Kiama alizozitaja Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW).

Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Katika dalili za kukaribia kwa Kiama ni kupotea kwa elimu na kuongezeka ujinga.’

Bukhari

 

KUSHINDANA NA KUJISIFIA KATIKA KUIPAMBA MISIKITI

Imepokelewa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Katika dalili za kukaribia kwa Kiama; ni watu kushindana na kujisifia katika kuipamba misikiti”.

Annasai

 

Anasema Bukhari;

“Amesema Anas (RA) kuwa; ‘Watu wataipamba lakini hawendi kusali ndani yake isipokuwa wachache”.

 

Omar bin Khattab (RA) alikataza watu kuipamba sana misikiti kwa sababu mapambo yanawababaisha watu ndani ya Sala zao, na alipokuwa akisimamia utengenezaji wa msikiti wa Mtume (SAW) alikuwa akiwaambia wajenzi;

“Wakingeni watu na mvua na msitie rangi nyekundu wala manjano mkawababaisha watu”.

Bukhari

“Mwenyezi Mungu amrehemu Omar bin Khattab (RA)”, anasema Sheikh Yusuf Wabil, “kwani watu hawakutoshelezeka na kuwakinga watu na mvua wala hawakutoshelezeka na rangi za manjano na nyekundu, bali misikiti siku hizi inapambwa na kujazwa nakhshi mfano wa nguo inavyonakshiwa”.

 

MAUAJI

Kutoka kwa Abu Hurairah (RA) amesema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Kiama hakitosimama mpaka ‘Haraj’ ikithiri”.

Wakamuuliza;

“Ni nini hii ‘Haraj’ ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?’

Akasema;

“Mauaji, mauaji!.”

Muslim

Na katika riwaya nyingine iliyosimuliwa na Abu Musa (RA) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Kabla ya Kiama kusimama kutatokea ‘Haraj’.”

Wakamuuliza;

“Ni nini hii ‘Haraj’ ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?”

Akasema;

“Mauaji”.

Wakamuuliza;

“Kuliko tunavyouwa? Tunauwa (vitani) katika mwaka mmoja zaidi ya elfu sabini?”

Akasema;

“Si kama kuuwa kwenu washirikina, bali huko ni kuuwana nyinyi wenyewe kwa wenyewe.”

Wakasema;

“Tutakuwa na akili zetu siku hiyo?”

Akasema;

“Zitaondolewa akili za wengi wa watu wa zama hizo. Watakuwa na wafuasi wengi kama vumbi, wengi wao watadhani kuwa wameshika chochote (katika haki), lakini (ukweli ni kuwa) hawana chochote”.

Imam Ahmed – Ibni Majah

 

Kutoka kwa Abu Hurairah kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Naapa kwa Yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, haitotoweka dunia mpaka iwajie watu siku ambayo ndani yake muuaji hatojuwa kwa ajili gani ameuwa na wala aliyeuliwa kwa ajili gani ameuliwa.”

Akaulizwa;

“Yatakuwaje hayo?”

Akasema;

“Al Haraj! aliyeuwa na aliyeuliwa (wataingia) Motoni.”

 

Haya yote yashatokea kweli katika zama zilizopita na tuanayaona yakitokea katika zama zetu hizi pia, hasa baada ya kuvumbuliwa kwa silaha zinazoangamiza.

Na katika hadithi sahihi iliyomo katika Mustadrak ya Al Hakim, Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Umma wangu ni umma utakaohurumiwa, hawatokuwa na adhabu huko Akhera, kwani adhabu zao ni za dunia, mauaji na mashaka na mitetemeko”.

 

MTU ATATAMANI KUFA

Imepokelewa kuwa Abu Hurairah (RA) amesema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Hakitosimama Kiama mpaka mtu atakapopita penye kaburi la mtu akasema;

“Yareti mimi ndiye ningelikuwa mahali pake”.

Bukhari

Na kutoka kwa Abu Hurairah pia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, dunia haitotoweka mpaka mtu atakapopita penye kaburi akasimama na kusema; ‘Yareti ningelikuwa mimi ndani ya kaburi hili’. Si kwa ajili ya dini, bali kwa ajili ya mitihani.”

Bukhari

 

Amesema Ibni Masaud (RA);

“Utakupitikieni wakati, mtu akiyakuta mauti yanauzwa, basi atayanunua”.

 

Wanasema maulamaa kuwa mambo kama haya si lazima yatokee katika kila nchi, lakini yanaweza kutokea katika zama mbali mbali kutokana na mitihani mizito mbali mbali, na mtu anapokumbwa na mitihani hiyo atakapopita makaburini atahisi kama kwamba yule aliyelala ndani mle ndiye aliyestarehe, ama yeye anajiona yumo katika adhabu, misukosuko mashaka na mitihani mikubwa isiyomalizika.

 

KUPIGANA NA WARUMI (WAKRISTO)

Kutoka kwa Auf bin Malik Al Ashjaiy (RA) amesema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Hesabu mambo sita, lazima yatatokea kabla ya kusimama Kiama”,

(miongoni mwa mambo sita hayo akasema; “Kisha vita vitasimamishwa baina yenu na watu wa manjano (Wakristo), kisha watakufanyieni khiana, watakujieni chini ya bendera themanini, chini ya kila bendera (watu) elfu kumi na mbili.”

Bukhari

 

Siku moja alikuja mtu kwa Abdillahi bin Masaud (RA) akamwambia;

“Ewe Abdallah! Kiama kitasimama (karibu sana)”.

Abdillahi bin Masaud (RA) aliyekuwa amekaa akiwa ameegemea, akakaa vizuri kisha akamwambia;

“Hakika ya Kiama hakitosimama mpaka kwanza mirathi isigawiwe na ngawira isifurahiwe”.

Kisha akasema huku akiashiria upande wa Sham (upande wa Mashariki);

“Maadui watajikusanya kuwapiga vita Waislam, na Waislam watajikusanya kwa ajili ya kupambana nao”.

Nikamuuliza;

“Warumi? (Wakristo?)”

Akasema;

“Ndiyo, na katika vita hivyo wengi watartaddi, na Waislamu watatayarisha jeshi litakalokuwa tayari kufa lisilokubali kurudi nyuma bila ushindi, watapigana vita mpaka usiku utakapoingia, kisha watarudi nyuma hawa na wale, hapana mshindi kati yao, kisha jeshi litaangamia, kisha Waislamu watatanguliza jeshi (lingine) litakalokuwa tayari kufa, watapigana vita mpaka wakati wa jioni, kisha watarudi nyuma hawa na wale, hapana mshindi kati yao, kisha litaangamia jeshi. Itakapoingia siku ya nne, Waislamu waliobaki watakuja kuwasaidia, na Mwenyezi Mungu atawajaalia ushindi uwe upande wao, watapigana vita visivyopata kuonekana namna yake, hata ndege akipita juu yao, basi ataanguka akiwa amekufa”.

Muslim

 

KUJA KWA QAHTANIY

Imepokelewa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) amesema;

“Hakitosimama Kiama mpaka kwanza aje mtu kutoka kabila la Qahtaniy (kabila la watu wa Yemen), atawaongoza watu kwa bakora (yaani atawaongoza na wataongoka vizuri na wote watampenda)”.

Imam Ahmed – Bukhari na Muslim

 

MUHAMMAD FARAJ SALEM AL SAIY