TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 » Sunnah  

FADHILA ZA MWEZI WA RAMADHAAN  

Imeandikwa na: Ukht Muznah Faraj

ASSALAMU ALAYKUM!

Ndugu yangu katika imaan:

Sifa njema zote Anastahiki Allah Mola wa viumbe vyote na Swalah na salamu zimfikie Mtume wetu na kipenzi chetu Muhammad (s.a.w.) na aali zake na sahaba zake wote.

Ama kwa hakika katika mwezi wa Ramadhaan kuna fadhila nyingi ambazo mimi nitazitaja kwa uchache namuomba Allah Aniwafiqishe 'asaa yawe na manufaa katika duniya na akhera Insha-Allahu  Aamiin.

1)     NI MWEZI WA QUR'AN

Kama Alivyosema  Mwenyeezi Mungu Mtukufu katika kitabu Chake:

"Mwezi wa Ramadhani ni mwezi ambao imeteremshwa Qur'an ili iwe uongozi kwa watu na hoja na upambanuzi (Baina ya haki na batil) Qur'an 2:185

Na imekua makusudio yake  nikuteremshwa Qur'an kutoka katika Lauhim-Mahfudh ilaa samai dduniya (Kutoka Lawhim-Mahfuudh mpaka mbingu ya kwanza). 

Vilevile kama ilivyo pokewa na ibni 'Abbaas kuwa  makusudiyo yake   kwa hakika kuteremshiwa Mtume (s.a.w.) Qur'an mwanzo ni katika mwezi wa Ramadhani na vilevile Qur'an mwanzo wa kateremka ni usiku wa Laylatul Qadir na Laylatul Qadir iko katika mwezi wa Ramadhaan.

Hivyo basi ni juu yetu kufanya juhudi katika mwezi huu kukithirisha sana kusoma Qur'an.  Walikua Salaf Swaalih (Wema Waliotangulia) wakikilinda kitabu cha Allah kwa kukisoma na kuyafanyia kazi yaliyokuwemo kwa mazingatiyo. Pia Tunaambiwa kuwa Sayyidnaa Jibriil (a.s.) akimfundisha Mtume (s.a.w.) Qur'an katika mwezi wa Ramadhaan, na alikuwa 'Uthmaan bin 'Afaan (r.a.) kila siku akisoma Qur'an yote yaani anakhitimisha mara moja kwa siku,  kwa maana,  msahafu mzima anausoma kwa siku moja. Na walikuwa baadhi yao katika wema wakisoma Qur'an yote kwa siku tatu, wengine kwa wiki moja na wengine kwa siku kumi. Walikuwa wakisoma Qur'an ndani ya Swalah na nje ya Swalah.

Mwenyeezi Mungu Atuwafiqishe mimi na wewe tuisome Qur'an na kwa mazingatiyo khassa katika mwezi huu tufanye juhudi sana ili tuweze kupata fadhila za mwezi huu mtukufu.

2)     NI MWEZI WA SUBIRA:

 Subira ni katika jambo gumu na halipati ila kwa mtu mcha Mungu na mnyenyekevu kwa Allah. Na katika kufunga kunatakiwa subira pale mtu anapo jizuilia kutokana na kutokula, kunywa, matamanio na mengineyo. na imekua saumu ni nusu ya subira na subira malipo yake ni pepo kama alivyosema Mwenyeezi Mungu mtukufu:

"Kwa hakika (Mwenyeezi Mungu) Atawapa wenye kusubiri malipo bila ya hisabu" Qur'an 39:10:

 

3)     MILANGO YA MOTO INAFUNGWA, MILANGO YA PEPO INAFUNGULIWA NA MASHETANI WANAFUNGWA:

Kama ilivyokuja katika hadithi iliyopokelewa na Maimamu wawili:

 Mtume (s.a.w.) amesema,  "Pindi inapo kuja Ramadhaan inafunguliwa milango ya pepo, na hufungwa milango ya moto, na masheytwaani wanafungwa kwa Minyororo"

(imesimuliwa na Al-Bukhaariy na Muslim)

 Kwa hakika utaona katika mwezi huu watu wengi wanajitahidi kujiepusha na maasi, watu wanajaa misikitini kwa kufanya ibada ya mwezi huu hii ni kwasababu mashettaani wamefungwa na sheytaani juu ya uasi wake lakini anauogopa mwezi wa Ramadhaan na vitimbi vyake vinakuwa dhaifu ndio mana wengi nyoyo zina badilika wanaswali  na kujitahidi kufanya kheri.  Lakini ikimalizika Ramadhaan  tu basi Swalah imekwisha kama vile Allah yupo Ramadhaan tu.  Huu ni msiba ndugu zangu waislamu Allah Asitujaalie katika hao.

4)     LAYLATUL QADR:

Katika mwezi huu kuna siku ya Laylatul Qadr siku ambayo ni bora kuliko miezi elfu kama  Alivyosema Mwenyeezi Mungu:

" Huo ni usiku wa hishima ni bora kuliko miezi elfu.

  Huteremka Malaika na roho (za viumbe watakatifu) katika (usiku) huo  

   kwa idhini ya Mola kwa kila jambo.

  Ni amani (usiku) huo mpaka mapambazuko ya alfajiri"

Qur'an 97:3-5

Imehisabiwa mtu atakapo fanya ibada katika usiku huo mmoja nikama amefanya ibada sawa na miaka 83 na hii ni katika fadhila kubwa kabisa. Na katika Muwat'aa Imamu Maalik kwa isnadi iliyotumwa amesema.

Mtume (s.a.w.) ameona umri wa umma za mwanzo ni mrefu, na umri wa umati wake ni mfupi akapewa usiku wa Laylatul Qadr uwe ni bora kuliko miezi elfu.

(Muwattah1/321(Muhammad Fuad 'Abdul Baaqy)

Hakuna siku tukufu na kubwa kama siku hii ni wajibu kwetu kuutafuta usiku huu katika kumi la mwisho kufanya ibada ili tupate fadhila hizo.  Ninamuomba Allah atuwezeshe kwa hilo AMIIN.

 

5)     DUA NI ZENYE KUKUBALIWA:

Katika hadithi iliyopokewa na imam Ahmad:

Kutoka kwa Jaabir (r.a) kwa isnadi iliyo nzuri.

 Mtume (s.a.w.) Amesema "kila Muislamu dua zake ni zenye kukubaliwa atapo muomba katika mwezi wa Ramadhaan"

Na imepokewa katika hadithi kuwa du'aa ya mwenye kufunga pia ni yenye kukubaliwa.  Basi mtu ajipinde katika kumuelekea Allah kumuomba mambo ya kheri ya dunia na akhera aombe pepo ya Jannaatul Firdaus  na alete maombi mengine Insha Allah Mwenyeezi Mungu Atayapokea maombi yetu AMIIN.

Lamwisho ambalo nitakua nimekamilisha maudhui yangu:

 

HAKIKA MWEZI HUU NI MWEZI WA KUTOA:

Na alikua Mtume (s.a.w.) akizidisha kheri nyingi katika mwezi wa Ramadhaan.

Imepokewa na tirmidh kutoka kwa Anas (r.a.) Kasema Mtume (s.a.w.) "Bora ya kutoa sadaqa ni kutoa katika mwezi wa Ramadhaan"

Na imepokewa na Zaid bin Aslam kutoka kwa babake, amesema nimemsikia 'Umar bin Khattwaab (r.a.) anasema, "ametuamrisha Mtume (s.a.w.) tutoe sadaqa nikatoa mali yangu nikasema leo nimemtangulia Abu Bakkar nimekwenda na nusu ya mali,  akasema Mtume (s.a.w.) kunambia umewabakishia nini watu wako? nikasema nusu kama hii, na akaja Abu  Bakkar na kila mali yake Mtume (s.a.w.) akamuuliza umewabakishia nini watu wako? Akasema nimewabakishia Mwenyeezi Mungu na Mtume wake. Nikasema huyu Abu  Bakkar hapitiki na kitu chochote abadan"

Kuonyesha wema waliotangulia walikua wakishindana katika kheri lakini  tofauti kubwa katika zama zetu hizi watu wanashindana katika mambo ya kidunia. 

Insha Allah Atujalie mema tuyafuate na mabaya tuyawache na tushindane katika kila kheri ili tuwe ni wenye kufuzu na kupata daraja ya juu ya Pepo.

 

 ALLAHUMMA AAMIIN.