|
Ndugu yangu katika imaan:
Sifa njema zote Anastahiki Allah
(s.w.t.) Mola wa viumbe wote Mwingi wa Rehma
na Mwingi wa Kusamehe na rehma na
amani zimfikie kipenzi Chake Allah Mtume wetu Muhammad
(S.A.W.) Jamaa na sahaba wake wote.
Amma Baad:
Ndugu
yangu muislamu ama kwahakika umetufikia mwezi ulio mtukufu
na wenye fadhila kubwa na mavuno kwa wenye mazingatiyo kwa
hayo nao ni mwezi wa Ramadhan ambao Allah Ameufaradhisha kwa
Waislam kwa kauli yake
Jalla
Wa 'Alaa Alipo sema:
"Enyi mlioamini mmefaradhishiwa (mmelazimishwa) kufunga
(Saumu mwezi wa ramadhani) kama walivyofaradhishiwa kabla
yenu ili mpate kumcha Allah.
Qur'an
2-183
Na hili la kumcha Allah ndio lengo kabwa la ibada hii ya
funga kwani ni ibada ya siri baina yako na
Mola wako. Na wengi wanaliona
gumu jambo hili la kufunga wakati linafadhila kubwa kabisa
wengi wanapitwa na fadhila za kufunga kwa kupenda kula na
kunywa. Majuto yatawajia pale watakapo kutana na Mola wao
hali hawana kitu.
Na nisiku maalum, siku chache katika mwaka mzima zilizowekwa
watu hawamuonei haya Mwenyeezi
Mungu wanakula mchana bila ya udhuru wowote wa kisheria.
Allah Anatwambia katika kitabu chake kitukufu:
"Siku chache tu (kufunga huko) Na atakaekuwa mgonjwa katika
nyinyi au katika safari (akafungua baadhi ya siku), basi
(atimize) hisabu katika siku nyingine.
Qur'an 2-184
Amaa kwahakika tumeona umuhimu na wajibu wa kufunga. hivyo
basi napenda kuchukua fursa hii adhimu kuwafahamisha ndugu
zangu katika imaan fadhila za kufunga namuomba Allah
Aniwezeshe.
Miongoni mwa fadhila hizo ni:
1- Hakika ya funga
inamuokoa mtu kutokana na moto
kama ilvyopokewa na Imam Ahmad katika hadithi sahihi.
Kutoka kwa Jaabir (r.a) hakika ya Mtume (s.a.w) amesema: "
saumu nikinga itamukoa mja kutokana na moto"
(siku ya qiyama)
(imepokewa na tabraniy kutoka kwa othman bin abil aass)
Na katika hadithi iliopokewa na muttafaqun alayhi
Kutoka kwa Abiy Saidi lkhudhriyy (r.a) hakika Mtume (s.a.w.)
amesema: " Mwenye kufunga siku kwa
ajili ya Allah Mwenyeez Mungu Atamuokoa
uso wake kutokana na moto kwa umbali wa miaka sabini"
Ndugu yangu muislam ikiwa unafunga siku moja Allah Atakuokoa
na moto wa jahannam je, Ukifunga ramadhani yote! hakika hii
ni fadhila kubwa.
Na fadhila hizi zinaingia katika funga za lazima yaani
fardhi na Sunnah.
2- Saumu ni kinga kutokana na matamanio:
Imekuja
katika hadithi.
Kutoka kwa Ibni Masoud (r.a) amesema Mtume (s.a.w.)
"Enyi kundi la vijana miongoni
mwenu atakaekuwa na uwezo wa kuowa basi na aowe (kufanya
hivyo) kutampelekea kuinamisha macho yake na kuhifadhi tupu
yake. Ikiwa hana uwezo wa kuowa
basi na afunge kwani hiyo ni kinga kwake"
(hadithun muttafaqun alayhi)
Hakika vijana wengi wanashtakia kutokana na matamanio khasa
katika zama zetu hizi za wanawake wanavyotembea wazi katika
masoko kwenye magazeti wanajitoa katika matangazo katika
televisheni hii ndio sababu kubwa inayo leta athari ya
uchafu na ufisadi mkubwa katika ardhi.
Allah Atuhifadhi! Na kwa
sababu hiyo Mtume (s.a.w.) akawanasihi vijana ikiwa mtu hana
uwezo wa kuowa basi na afunge.
3- Hakika saumu ni njia ya kumpelekea mtu peponi:
Kutoka kwa Abiy Umamah (r.a) amesema kumwambia Mtume
(s.a.w.) "Ewe Mtume wa Allah
Niamrishe mimi jambo litakalonifaa mbele ya Allah. "akasema
Mtume (s.a.w.) Ni juu yako kufunga kwa hakika hakuna mfano
wake"
(sunanu nnisaai)
Akabainisha alayhi ssalatu wassalam hakuna kitu
kitakachomkurubisha mja kwa Allah, na kumuweka mbali na
adhabu
kama kufunga.
Bali ametupa khabari Mtume (s.a.w.) katika pepo kuna
mlango khassah wa wenye kufunga.
Kutoka kwa Sahal bin Sa'ad (r.a) hakika Mtume (s.a.w.)
amesema "Hakika katika pepo kuna mlango unaitwa Rayyaan,
wataingia humo siku ya qiyama wenye kufunga tu. hatoingia
yeyote mwingine, utasema wako wapi wenye kufunga?
Watasimama kuingia hatoingia yeyote mwingine, wakisha
kuingia utafugwa, basi hatoingia mwengine"
(imepokewa na Bukhar)
Na
umepewa jina hilo inanasibiana na sifa ya saumu ambayo
inampata mtu kiu kutokana na athari ya kufunga.
Mara nyingi mtu anapofunga
hatamani chakula
kama anavyotamani maji.
4- Hakika ya funga itamuombea mtu siku ya qiyama:
Kutoka kwa Abdullahi bin Amru bin Aassi (r.a) amesema Mtume
(s.a.w.) " Funga na
Qur'an zitamuombea mja siku ya
qiyama, itasema funga ewe mola amejizuilia kutokana na
chakula chake na matamanio yake wakati wa mchana, basi
namuombea msamaha, na itasema Qur'an,
amejizuilia kutokana na usingizi wake wakati wa usiku
ninamuombea msamaha. akasema wamesamehewa.
(imepokewa na Ahmad na Haakim biisnadis sahihi)
5- Hakika ya saumu ni kafara na msamaha kutokana na
madhambi:
Kwahakika mema huondosha maovu na saumu ni katika jambo jema
sana. Na Amesema Allah (s.w.)
"Hakika ya mema huyaondosha maovu"
Qur'an 11-114.
Na katika hadithi iliyopokewa na maimamu sita.
Kutoka
kwa Hudhayfah (r.a.) amesema Mtume (s.a.w.) "
Fitna ya mtu kwa mkewake (watu
wake)
mali
yake na jirani yake itamfidiya kutokana na sala, funga na
sadaqa"
Mara
nyingi kunakua na upungufu ima katika haki za mkeo kwa njia
ya maneno au kuudhi na upungufu mdogodogo na katika makosa
ya haki za jirani iwe kwa matendo au qauli na katika
kuitakasa mali. Vyote hivyo
hutakaswa na sala, funga na sadaqa. Iwapo mtu
atajilazimisha na haya basi atasamehewa madhambi yake
madogo.
Na kutoka kwa Abiy Hurayrah (r.a.) hakika Mtume (s.a.w.)
amesema "Mwenye kufunga Ramadhani
kwa imani na akatarajia malipo atasamehewa madhambi yake
aliyoyatanguliza"
Imaani
ni kumuamini Allah na funga ukamkusudia Allah
Aliyetukuka
na ukataraji malipo ambayo Allah Ameyatolea ahadi kwa wenye
kufunga.
Kwani kuna baadhi ya watu
bado wanamshirikisha Mwenyeezi
Mungu katika ibada Zake, wafunga, wasali kwa ajili ya
majini, ni makosa makubwa
sana.
Na
katika hadithi nyingine:
Kutoka kwa Abiy Harayrah (r.a) amesema Mtume (s.a.w.)
" Sala tano, na
Ijumaa mpaka Ijumaa,
na Ramadhani mpaka Ramadhani, zitamfidia hizo baina yake
madamu atakua ni mwenye kujiepusha na madhambi makubwa"
(imepokewa na muslim)
Kufunga
mwezi wa Ramadhani ni sababu ya kusamehewa madhambi ambayo
umeyatanguliza katika kipindi cha mwaka mzima uliopita
lakini basi imewekewa sharti nikwamba ujiepushe na madhambi
makubwa kwani madhambi makubwa hayafutiki mpaka ulete tawbah
na hili wamekubaliana wanavyuoni wote. Na vilevile Allah
Amesema katika kitabu chake kitukufu:
Ikiwa
mtajiepusha na (madhambi) Makubwa yaliyo katazwa
Atakufutieni (Mwenyeez Mungu) maovu yenu na Atakuingizeni
katika maingizo matukufu.
Qur'an 4-31.
6-
Hakika ya saumu ni sababu ya kupata furaha ya nyumba mbili:
Kama ilivyokuja katika hadithi iliyopokewa na muttafuqun
alayhi.
Kutoka kwa Abiy Hurayrah (r.a) Amesema Mtume (s.a.w.)
"Mwenye kufunga ana furaha mbili;
furaha ya kwanza anapofungua na furaha ya pili atakapokutana
na Mola wake".
Amma kwa hakika katika furaha ya kwanza ni pale Allah
Alipotuhalalishia wakati wa jioni kula na kunywa kwani ni
vitu ambavyo tunavipenda kwa hivyo tukamuabudu Mwenyeezi
Mungu kwa kujizuilia kula, kunywa na matamanio wakati wa
mchana.
Amma furaha ya pili nipale Allah alipo tuwafiqisha kuitimiza
saumu hadi jioni kwani mara nyingine unakua taabani mpaka
ikifika jioni unamshukuru Allah Alhumdulillahi nimeifikisha
saumu hadi jioni na nimeikamilisha ibada.
7- Hakika ya harufu
ya mdomo wa mwenye kufunga mbele ya Allah ni nzuri kuliko
harufu ya miski:
Harufu ya mdomo ambayo inatoka ni kutokana na kutokula
chakula. Nayo ni harufu
iwachukizayo watu lakini mbele ya Allah Anaipenda.
Hadithi iliyopokelewa na
muttafuqun alayhi:
Amesema Mtume (s.a.w.) "Naapa kwa yule ambae nafsi ya
Muhammad iko mikononi mwake; harufu ya mdomo wa mfungaji ni
nzuri mbele ya Allah kuliko harufu ya miski".
Kwa
dalili hii inafaa mtu kupiga msuaki wakati jua
limeshachomoza bali ni jambo linalo pendeza sana katika kila
hali unaweza ukasafisha mdomo wako kwa kupiga msuaki wakati
wa sala, wakati wa udhu, wakati unapo amka kutoka usingizini
na pindi unapoona mdomo wako umebadilika ladha unapiga
msuaki maadamu utachunga kitu kisipenye katika koo ambacho
itabatilisha saumu yako. Isiwe
kwamba Allah anapenda harufu hiyo basi ikawa hupigi msuaki. Hiyo harufu
hata ukipiga msuaki Amesema
Allah Anaipenda
sana na itakuja kutokana na kutopita kitu tumboni.
Ninamuomba Mwenyeez Mungu aniwafiqishe mimi na ndugu zangu
katika imaani ajalie yawe na manufaa na faida kwa wasomaji
INSHAALLAH.
|