TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 »  Makala  

IKH-LAASWI

Na: Swaleh Mwanjia Kaima

UTANGULIZI:

 

Mwenyezi Mungu (SWT) amesema:

“Sikuwaumba Majini na wanaadamu ila wapate kuniabudu”. (Qur’an 51: 56)

 

Ibada ni neno linalokusanya mambo meengi. Ujumla wake ni kufungamana na kila analolipenda na kuliridhia Mwenyezi Mungu na kuacha kila alilolikataza Mwenyezi Mungu katika maneno na matendo.

 

Aya nyingi katika Qur’an zinazozungumzia ibada zimeambatanishwa na neno ikhlaaswi. Hebu turejee aya zifuatazo kwa mifano michache:

v     “Wala hawakuamrishwa ila kumuabudu Allah (SWT) kwa kumtakasia dini…..” Qur’an (98:5).

v     “Kwa yakini sisi tumekuteremshia kitabu hiki (Qur’an) kwa haki, basi muabudu mwenyezi Mungu kwa kumfanya mola yeye tu………” (Qur’an 39: 2-3).

 

Hii ni kusema kwamba ibada yoyote ile ambayo itafanywa pasi na ikhlaaswi, basi hiyo haitokubaliwa.

 

Mada yetu hii ya ikhlaaswi tutaizungumzia katika sehemu sita kama ifuatavyo:

1.      Maana ya ikhlaaswi.

2.      Umuhimu wa ikhlaaswi.

3.      Matunda na faida ya ikhlaaswi.

4.      Mifano ya watu waliokuwa na ikhlaaswi.

5.      Madhara/hatari ya kukosa ikhlaaswi katika ibada.

6.      Jinsi ya kuipata ikhlaaswi katika amali (ibada) zetu.

 

MAANA YA IKHLAASWI

Maana ya ikhlaaswi tunaweza kuiangalia katika mtazamo wa kilugha na kisheria.

Lugha:            Maana ya ikhlaaswi ni kitu safi au utakaso.

Sheria:            Ni kukusudia kwa kauli zako na matendo yako na ibada zako zote kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (SWT).

 

Ushahidi tunaupata katika Qur’an 6: 162-163., Mwenyezi Mungu (SWT) anaposema:

                        “Sema: Hakika swala yangu, na ibada zangu (nyingine zote) ……ni kwaajili ya Mwenyezi Mungu (SWT) mola wa viumbe vyote……..”

 

Mema tunayoyatenda na maovu tunayoyaepuka iwe ni kwa ajili ya kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (SWT).

 

Mifano michache ifuatayo ya ibada itatuwekea sawa nini tunakusudia tukisema ibada inatakiwa kufanywa na ikhlaaswi:

 

1.      Swala:

Mwenyezi Mungu anasema katika Qur’an 6: 162:

      “Sema: Hakika swala yangu, na ibada zangu (nyingine zote) ……ni kwaajili ya Mwenyezi Mungu (SWT) mola wa viumbe vyote……..” 

Tunaona katika sehemu nyingine Mwenyezi Mungu amewaonya wale wenye kuswali, si kwa kutaka radhi zake, bali kwa kutaka kuonekana, pale aliposema:

“Basi adhabu itawashukia wanaosali, ambao wanapuuza sala zao, ambao hufanya amali zao ili watu wawaone tu/riya” (Qur’an 107: 4-6).

 

2.      Zaka na sadaka:

Itakuwa ni batili kama sadaka au zaka itatolewa kwa ajili ya mtoaji kutaka kuonekana kuwa ametoa.

Allah (SWT) anasema:

“Enyi mlioamini, msibatilishe sadaka zenu kwa masimbulizi na udhia kama wale ambao hutoa mali zao kwaajili ya kutaka kuonekana na watu…” (Qur’an 2:264).

 

3.      Kutafuta elimu:

Aya ya ya kwanza kumshukia mwanadamu imesisitiza umuhimu wa elimu.

      “Soma kwa jina la Mola wako aliyekuumba.” (Qur’an 96:1).

 

Tunaona kuwa aya hii zaidi imesisitiza kuwa elimu lazima iwe ni kwa jina la Mola aliyetuumba. Kinyume na hivi mtu hatopata malipo bali ajiandalie makazi ya motoni. Mtume (SAW) anasema:

“Mwenye kutafuta elimu kwa lengo la kutaka kuonekana kuwa amesoma au ili abishane na wajinga, basi mtu huyo ataingizwa motoni na Mwenyezi Mungu” TIRMIDHIY.

 

Na katika riwaya nyingine amesema Mtume (SAW):

“Mwenye kutafuta elimu kwa lengo la kutaka kuonekana kuwa amesoma au ili abishane na wajinga, basi mtu huyo ajiandalie makazi yake yake motoni.” TIRMIDHIY.

 

Kwahiyo, ibada zetu zote tunazozifanya ni lazima ziwe ni kwaajili ya Allah (SWT) tu, vinginevyo hatutaambulia thawabu/malipo yoyote katika ibada hizo.

 

Kwa mfano alikuja mtu mmoja kwa mtume (SAW) akasema: “Mimi ninatoa sadaka kwaajili ya kutaka radhi za Allah na vilevile ninapenda niambiwe mkarimu.” Palepale Allah akateremsha aya isemayo:

…. anaependa kukutana na (jaza ya) mola wake (siku ya kiama) basi na afanye (atende) vitendo vizuri, na wala asimshirikishe kwa ibada ya Mola wake na (mtu) yeyote.” (Qur’an 18:110).

 

 

 

UMUHIMU WA IKHLAASWI

Yafuatayo ni maelezo kwa ufupi juu ya umuhimu wa ikhlaaswi katika maisha yetu ya kila siku:

i-                    Ni sharti la kukubaliwa amali zetu:

Ili amali ikubaliwe, lazima ifanywe kwa nia ya kutaka radhi za Allah (SWT).

Mtume (SAW) anasema:

“Hakika amali zote huzingatiwa kwa nia na hakika kila mtu atalipwa kulingana na nia aliyonuia. Yule ambaye amehama (kutoka Maka kwenda Madina)kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na mtume wake, basi hijra yake hiyo (ndiyo hasa) kwa ajili ya Allah na Mtume, Na ambaye amehama kwa malengo ya kidunia au kwaajili ya mwanamke anayetaka kumuoa, basi hijra (kuhama) kwake huko ni kwaajili ya hilo alilohamia.” BUKHARI & MUSLIM.

 

ii-                  Dawa ya unafiki:

Ibada zetu zikifanywa kwa ikhlaaswi zinatupelekea kuondokana na unafiki.

Miongoni mwa dalili za wanafiki zilizotajwa katika Qur’an ni (4: 142):

-         Kusimama katika swala kivivu,

-         kuzionyesha swala zetu, na

-         kutomtaja Mwenyezi Mungu.

 

Basi aya zifuatazo zinatoa maelezo ni namna gani mtu atatoka katika unafiki kwa kuwa na ikhlaaswi katika ibada zake:

“Hakika wanafiki watakuwa katika tabaka la chini kabisa la moto na wala hawatopata wa kuwanusuru. Isipokuwa wale waliotubia, na wakafanya vitendo vizuri, na wakashikamana na dini ya Mwenyezi Mungu, na wakawa na ikhlaaswi katika dini yao kwa ajili ya Allah (SWT) basi hao watakuwa pamoja na waumini (Watatoka katika unafiki)….” Qur’an 4:145-146.

iii-                Dawa ya Riya:

Riya maana yake ni kutaka kila amali yako ya kheri ionekane au ijulikane. Kwa hivyo, ili uondokane na riya, basi ni lazima ufanye ibada zako kwa ikhlaaswi.

 

MATUNDA/FAIDA ZA IKHLAASWI

Miongoni mwa faida za ikhlaswi ni:

i-                    Kuweza kumshinda shetani.

ii-                  Kuweza kutenda mema na kuyaepuka maovu mahali popote pasi na kumuogopa mtu yeyote au kutaraji malipo kutoka kwa mtu yeyote.

iii-                 Amali iliyofanywa kwa ikhlaaswi inaweza kumnusuru mtu wakati anapofikwa na matatizo.

 

Kwa ufafanuzi zaidi wa faida hizo hapo juu tunanukuu kisa kifuatacho kutoka katika hadithi ya mtume iliyopo katika kitabu cha Imamu Bukhari na Muslimu. Hadithi hii inapatikana pia katika kitabu cha riyadhu swalihina, katika mada ya ikhlaswi. Ni hadithi No. 12. Ifuatilize hadithi hii kwa makini:

 

Imepokelewa kutoka kwa Abdallah bin Umar bin al-Khattab (radhi za Allah ziwe juu yake) akisema: Nimemsikia mtume (SAW) akisema:

“Waliondoka watu watatu katika watu waliokuwepo kabla yenu (masahaba), mpaka ukawaingilia usiku wakaingia katika pango (ili wapate kulala). Jiwe likaanguka kutoka mlimani na kuziba mlango wa lile pango”.

 

Watu hawa watatu wakawa hawana njia ya kutokea. Wakasema:

“Hakuna kitakacho tuokoa kutokana na hili jiwe isipokuwa ni kumuomba Allah (SWT) kwa vitendo vvyetu vizuri (ambavyo tumekwisha wahi fanya).”

 

Wa kwanza wao akasema: “ Eeeeh Mola wangu!, mimi nilikuwa na wazee wangu wawili, watu wazima, nilikuwa nikiwapa maziwa kabla ya kumpa yeyote katika watoto wangu, watumishi au wangu au mtu yeyote wa nje. Siku moja nilikwenda mbali kutafuta kuni, sikuweza kurudi (mapema) mpaka walipokuwa wamelala. Nikakamua maziwa, na kama kawaida yangu nikaenda kuwapelekea yale maziwa. Kwa bahati mbaya nikawakuta wamelala. Nikachukia kuwaamsha, na pia sikupenda kumpa mtuyeyote maziwa yale kabla yao. Watoto wangu walikuwa wakilia kutokana na njaa chini ya miguu yangu, lakini nilisubiri na bakuli la maziwa mpaka ilipoingia alfajiri. Walipoamka alfajiri, nikawapa yale maziwa, wakanywa.

Eeeh Mola wangu wa haki!, ikiwa mimi nilifanya hivyo kwaajili ya kutafuta radhi zako, basi tupe faraja katika hili (jambo)”…… JIWE LOKASOGEA LAKINI HAWAKUWEZA KUTOKA.

 

Wa pili wao akasema: “Eeeh Mola wangu wa haki!, hakika mimi nilikuwa na binti wa baba yangu mdogo, ambaye alikuwa ni mtu anayependeza sana kwangu. Nilikuwa nikitaka kufanya naye mapenzi, lakini alikataa. Mpaka ikapita miaka akanijia na shida yake, nikampa dinari 120 kwa sharti kuwa akubali nimuingilie. Yule binti akakubali. Lakini nilipokuwa nimekaa baina ya miguu yake (tayari kumuingilia) akasema: ‘mche Mwenyezi Mungu, na wala usiivue pete isipokuwa kwa haki yake.’ Nikaondoka na kumuacha yule mwanamke na hali ya kuwa bado ninampenda sana. Na nikamwachia zile pesa ambazo nilimpa.

Eeeh Mola wangu wa haki, ikiwa mimi nilifanya hivyo kwaajili ya kutafuta radhi zako, basi tupe faraja kutokana na jambo hili tulilonalo.” JIWE LIKASOGEA TENA KIDOGO, LAKINI BADO HAWAKUWEZA KUTOKA KWA KUWA UWAZI ULIKUWA BADO NI MDOGO.

 

Na akasema yule wa tatu: “Eeh Mola wangu wa haki, hakika mimi nilikuwa nimeajiri watu, na nikawapa ujira wao (baada ya kumaliza kazi) isipokuwa mtu mmoja ambaye aliondoka bila ya kuchukua mshahara wake. Nilimuendelezea kile kiasi cha mshahara wake na kuwa mali nyingi.

 

Baada ya muda fulani yule mtu (aliyekuwa mwajiriwa) akanijia na kutaka ujira wake alouacha siku za nyuma. Nikamwambia kuwa kila alichokiona pale kilikuwa ni kutokana na ujira wake ambao niliuendeleza. Hivyo achukue kila kitu (Ngamia, ng’ombe, kondoo, mbuzi n.k.) Mtu yule alifikiri ninamtania. Lakini nilipomuhakikishia kuwa nilikuwa ninasema kweli, alichukua kila kilichokuwepo bila ya kuniachia chochote.

Eeeh Mola wangu wa haki!, ikiwa mimi nilifanya hivi kuzitaka radhi zako, basi tupe faraja katika jambo hili.” JIWE LIKAFUNGUKA WAKATOKA KATIKA PANGO NA KWENDA ZAO.

 

MAELEZO:

Hadithi hii ina mafunzo mengi sana, mojawapo ni kuwa ibada au amali inayofanywa kwa ikhlaaswi inaweza kumuokoa mja anapopatwa na matatizo/janga.

 

 

MIFANO YA WATU WALOKUWA NA IKHLAASWI

Iko mifano mingi, mwiongoni mwayo ni hii tutakayoielezea hapa chini:

 

Mfano wa kwanza ni wa Khalid Bin Walid (R.A) ambaye aliondolewa kwenye uongozi wa jeshi na Umar Bin Khattab kabla ya fat-hu (kukombolewa) Shaam (Syria). Baada ya kuondolewa Khalid Bin Walid kwenye uongozi, Umar (R.A) alimteua Abuu Ubaida Aamir Bin Jarrah kuwa kiongozi mpya wa jeshi.

 

Pamoja na kuondolewa kwenye uongozi wa jeshi, Khalid alionekana kupigana kwa nguvu zote katika kuikomboa Shaam. Baadhi ya maswahaba wakamwambia ‘mbona bado uko mstari wa mbele, una pigana kama kawaida ili hali wewe si kiongozi wa jeshi tena?’ Khalid akawajibu:  “ Ninataka kuikomboa Shaam kwa ajili ya Allah (SWT) na wala siyo kwaajili ya Ummar Bin Khattab.

 

Hii ndiyo ikhlaaswi. Pamoja na kuwa Khalid Bin Walid aliuzuliwa u amiri jeshi, bado alikuwa katika mstari wa mbele ili kuikomboa Shaam kwaajili ya kuzitafuta radhi za Mwenyezi Mungu (SWT) na wala siyo kwa ajili ya kumridhisha Umar, au kwa sababu alikuwa ni kiongozi, au Imam.

 

Mfano wa pili tunaupata katika vita nyingine ambayo walipata kupigana waislamu. Katika vita hivi walikutana na ngome ngumu ya makafiri. Takriban miezi saba (7) waislamu walishindwa kuingia katika ngome hii.

 

Mmoja kati ya waislamu alikuwa akiamka usiku na kuchimba shimo chini kwa chini (kwa siri) na ifikapo asubuhi, alikuwa akiliziba na kujiunga na wenzake. Baada ya muda kadhaa ulipatikana mwanya wa kuwawezesha waislamu kuingia katika ngome ya makafiri. Alipofanikiwa kupata mwanya huu, aliingia kwenye ngome ya makafiri na kupiga takbir ya nguvu kama ishara ya kuwajulisha waislamu kuwa ngome inaingilika. Waislamu waliivamia ngome hii lakini hakujulikana ni nani aliyechimba lile shimo.

 

Kiongozi wa jeshi la waislamu, kwa furaha kubwa alisimama na kutangaza kuwa aliyechimba lile shimo ajitokeze ili apate kumlipa. Siku tatu zilipita baada ya tangazo hili hakuna aliyejitokeza. Siku ya nne (4) kiongozi yule alitoa tangazo jingine kuwa kujitokeza kwa aliyechimba shimo lile ni wajibu, kwani lasivyo atakuwa amemuasi kiongozi wa jeshi.

 

Hapa ndipo yule aliyechimba shimbo akajitokeza mbele ya kiongozi wa jeshi, lakini akiwa amejifunga kitambaa usoni na kusema: “Mimi nimetumwa na aliyechimba shimo, lakini kabla hajajitaja anakupa masharti matatu:

1-     Usimlipe kwa lile alilolifanya,

2-     Usilitaje jina lake kwa amiir Muuminina, na

3-     Usimuulize jina lake.”

 

Alipomaliza kauli hii alikimbia huyu bwana na akajifungua kitambaa, lakini kiongozi wa jeshi hakufanikiwa kumuona na kumtambua kuwa ni nani.

 

Baada ya tukio hili, yule kiongozi wa jeshi alikuwa kila akiingia vitani anaomba dua hii: “Eeeh Mola! Nakuomba unifufue na yule aliyechimba shimo, mimi pamoja na Mtume (SAW).”

 

 

Na mfano wa tatu ni wa Abubakar, ambaye alikuwa akiwaacha huru watumwa kwaajili ya kutafuta radhi za  alla (SWT). Tukio hili limetajwa katika Qur’an tukufu (92: 19-20):

“Na hali ya kuwa hakuna yeyote aliyemfanyia ihsani ili awe anamlipa. Isipokuwa (anafanya haya) kwa kutaka radhi ya Mola wake Mtukufu”

 

MADHARA/HATARI YA KUKOSA IKHLAASWI KATIKA IBADA

 

Kukosekana kwa ikhlaaswi katika ibada zetu husababisha madhara mengi sana. Tutayataja machache hapa chini:

i-                    Hubatilisha amali za mja na kumfanya asipate chochote isipokuwa ghadhabu za Allah (SWT). Allah (SWT) anasema:

“Enyi mlioamini, msibatilishe sadaka zenu kwa masimbulizi na udhia kama wale ambao hutoa mali zao kwaajili ya kutaka kuonekana na watu…” Qur’an 2: 264.

 

            Pia Allah (SWT) anasema:

“Ole wao wenye kuswali ambao huswali kwa ajili ya kuwaonyesha watu swala zao.” Qur’an 107: 4-6.

 

ii-                  Kumtia mtu katika Riya, kisha humtia katika shirki.

Mtume (SAW) anasema:

“Ninachokiogopea sana kwa umma wangu ni shirki ndogo”, wakamuuliza (maswahaba):” Shirki ndogo ni ipi?” Akasema (Mtume): “Ni Riya.”

 

Na katika hadithi nyingine, Mtume (SAW) anasema:

“Mwenye kuswali kwaajili ya kutaka kuonekana atakuwa amefanya shirki, na mwenye kufunga kwaajili ya kutaka kuonekana atakuwa amefanya shirki, na mwenye kutoa sadaka kwaajili ya kutaka kuonekana atakuwa amefanya shirki.” IMAM AHMAD.

 

iii-                 Kwa kuwa ikhlaaswi ndiyo roho ya ibada (amali), ibada yoyote isiyo na ikhlaaswi haiwezi kudumu.

Mifano:

a)      Kuna Binti ambaye alitaka kuolewa na bwana mmoja ili apate makaratasi ya kumuwezesha kuishi katika nchi moja ya ughaibuni. Baada ya kuolewa na kupata hayo makaratasi, alimfanyia vituko mumewe huyo mpaka ndoa yao ikavunjika.

b)      Kuvunjika na kusambaratika kwa taasisi nyingi za kiislamu. Hii ni kwasababu hazikuasisiwa chini ya misingi ya ikhlaaswi, bali kwaajili ya malengo ya kidunia tu.

 

iv-                Aliyefanya ibada kwaajili ya kutaka kuonekana ataingia motoni hata kama alikufa katika jihadi, au alisoma na kufundisha Qur’an au alitoa sadka na zaka.

 

Ushahidi wa hili tunaupata katika hadithi ndefu ya Mtume (SAW) ambayo inapatikana katika kitabu cha Imamu MUSLIM:

 

Mtume (SAW) anasema:

“Katika watu wa mwanzo watakaohukumiwa siku ya kiama ni mtu ambaye alikufa katika jihadi. Ataletwa mbele ya Allah (SWT) kisha atafahamishwa neema aliyopewa, ataifahamu. Kisha Allah (SWT) atamuuliza:

Allah     :‘umeifanyia nini neema hiyo?’

Atajibu   :‘Nimepigana kwaajili yako mpaka nimekufa shahidi’.

Allah     : ‘Muongo, lakini wewe ulipigana ili uitwe shujaa, na umeshaitwa (shujaa duniani).

Kisha ataburutwa uso wake ukiwa chini mpaka atupwe motoni.

 

Na mtu mwingine atakayehukumiwa mwanzo ni yule aliyejifunza elimu, kisha akaifundisha (kwa watu) na akasoma Qur’an. Naye ataletwa mbele ya Allah (SWT) na na kufahamishwa neema aliyopewa na Allah (SWT), naye ataifahamu. Kisha Allah (SWT) atamuuliza:

Allah          : ‘Umeifanyia nini neema hiyo?’

Atajibu   : ‘Nimejifundisha elimu, na nikawafundisha watu, kisha nikasoma Qur’an kwaajili yako.’

Allah     : ‘Muongo, wewe ulisoma elimu ili uitwe mwana chuoni, na ulisoma Qur’an ili uitwe msomaji mzuri. Na umeshaitwa (huko duniani.)

Kisha ataburutwa uso wake ukiwa chini mpaka atupwe motoni.

 

Na mtu mwingine atakayehukumiwa ni yule ambaye Allah (SWT) amemjaalia mali za aina kwa aina. Naye akazitoa sadaka na kuzitolea zaka. Ataletwa mbele ya Allah (SWT) na kufahamishwa neema aliyopewa na Allah (SWT), naye ataifahamu. Kisha Allah (SWT) atamuuliza:

Allah          : ‘Umeifanyia nini neema hiyo?’

Atajibu   : ‘Sikuacha katika njia ambayo wewe unapenda watu watoe katika njia hiyo, isipokuwa nimetoa kwaajili yako.’

Allah     : ‘Muongo, wewe umetoa mali yako ili uitwe mkarim. Na umeshaitwa (huko duniani.)

Kisha ataburutwa uso wake ukiwa chini mpaka atupwe motoni.”

 

Hadithi hii ni ushahidi tosha kuwa kama mtu atakufa katika jihadi, au atatafuta elimu, au atatoa sadaka, zaka, kujenga misikiti, kuwalisha mayatima n.k. kwaajili ya kutaka kuonekana au kupata sifa kutoka kwa watu, basi mtu huyo ataishia motoni.

 

Allah (SWT) aliwaambia watu wote hawa watatu kuwa ni wa waongo kwa kuwa yeye Allah tu ndiye ajuaye yaliyomo katika vifua/mioyo yetu. Allah (SWT) anasema kumwambia Mtume (SAW):

“Sema: Kama mtayaficha au mtayadhihirisha yaliyomo katika nyoyo zenu, basi Allah anayajua, na anajua yaliyomo mbinguni na ardhini. Na Mwenyezi Mungu juu ya kila kitu ni muweza”. Qur’an 3: 29.

           

JINSI YA KUIPATA IKHLAASWI KATIKA AMALI (IBADA) ZETU.

Zipo hatua kubwa tatu za kuzingatia ili kupata ikhlaaswi katika amali zetu. Nazo ni kujichunga kabla, wakati na baada ya kutenda amali.

i-                    Kabla ya amali:

Ni lazima tuzichunge nia zetu. Na tujiulize ni kwanini tunafanya amali hiyo? Je tunafanya amali ile kwaajili ya Allah (SWT) au kuna malengo mengine?

 

ii-                  Wakati wa amali:

Wakati tukiwa ndani ya amali, tujaribu kujikumbusha mara kwa mara, Je? Nia yetu haijabadilika?

 

iii-                Baada ya amali:

Baada ya kumaliza amali yeyote, tujaribu kuleta istighfaar (kuomba msamaha) kwani pengine ndani ya amali ilitupitia kufanya dhambi ya Riya. Pia tuwe wenye kumuomba Allah (SWT) azikubali amali zetu.

 

Tutatolea mfano wa swala jinsi gani mtu anaweza kujitahidi kupata ikhlaaswi katika ibada hii.

 

Mara baada ya mtu kunuwia kuswali ni sunnah kusoma dua ya istiftaahi, yaani dua ya kufungulia swala. Ndani ya dua hii kuna ile aya inayosema: “Inna swalaatii, wanusukii, wa mahyii wa mamatii lillahi rabbi al aalamiin” Kwa maana ya kuwa:

“Sema: Hakika swala yangu, na ibada zangu (nyingine zote) ……ni kwaajili ya Mwenyezi Mungu (SWT) mola wa viumbe vyote……..” Qur’an 6:162:

 

Katikati ya ibada ya swala, kwa mfano imamu akimaliza kusoma surat-al-faatiha, kisha akisoma suratul mauun, yaani “Araita al-ladhii yukadhibu biddiin…. (107: 1-6).” Ndani ya sura hii kuna aya isemayo “Ole wao wenye kuswali kwaajili ya kutaka kuonekana.” Qur’an 107:6. Kwa kusoma aya hii, imamu huwa anajikumbusha yeye na sisi kuwa tuwe ndani ya mstari wa ikhlaaswi katika ibada zetu. Ndiyo maana Allah (SWT) akasema: “Inaposomwa Qur’an, isikilizeni na mnyamaze kimya….”

 

Mara baada ya kumaliza kuswali, ni sunnah kusema astaghfirullah mara tatu (x3). Hapa tunapata funzo kuwa tunalizapo ibada zetu, tujaribu kuomba msamaha, pengine ndani ya ibada ile tulifanya jambo la kumuudhi Allah (SWT).

 

MWENYEZI MUNGU NDIYE MJUZI ZAIDI.

 

Swaleh Mwanjia Kaima,

Coventry,

U.K