TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 » Sunnah  

INGIA KATIKA MILANGO MINGI YA KHERI YA RAMADHAAN

Mwezi huu mtukufu umejaa fursa ya kujichumia mengi ya kheri ambayo thawabu zake huanzia tokea kumi hadi zaidi ya mia saba pamoja na malipo maalum yatokayo kwa Allaah kwa Mfungaji, kama alivyosema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم

((قال صلى الله عليه وسلم :   كل عمل ابن آدم له الحسنة بعشر أمثالها إلى سبعمائة ضعف . يقول الله عز وجل : إلا الصيام فإنه لي وأنا أجزي به ، ترك شهوته وطعامه وشرابه من أجلي،  للصائم فرحتان ؛ فرحة عند فطره ، وفرحة عند لقاء ربه، و لخلوف فم الصائم أطيب عند الله من ريح المسك))    أخرجه البخاري ومسلم

((Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم, kila amali njema ya mwanaadamu inalipwa mara kumi na inaongezewa thawabu kutoka kumi hadi mia saba, na Allaah سبحانه وتعالى Anasema isipokuwa Swawm, kwani hiyo ni kwa ajili  Yangu na Mimi Ndiye nitakayemlipa.  Ameacha matamanio yake na chakula chake na maji yake kwa ajili Yangu.  Kwa aliyefunga atapata furaha mbili; furaha anapofuturu na furaha atakapoonana na Mola wake, harufu inayotoka kinywani mwa aliyefunga ni nzuri mbele ya Allaah سبحانه وتعالى kuliko harufu ya misk)) Al-Bukhariy na Muslim  

Kwanza kabisa inatupasa tuanze mwezi huu mtukufu kwa kutia Nia moyoni (si kuitamka) yenye Ikhlaas ambayo ndio msingi wa kutaqabaliwa amali ya ibada yoyote, na ili kupata Ridhaa ya Allaah سبحانه وتعالى  kama Anavyosema:

}}وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاء وَيُقِيمُوا الصَّلَاةَ وَيُؤْتُوا الزَّكَاةَ وَذَلِكَ دِينُ الْقَيِّمَةِ {{

{{Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu, na washike Swalah, na watoe Zakah. Na hiyo ndiyo Dini madhubuti}} Al-Bayyinah: 5

Ifuatayo ni baadhi ya milango ya kheri ambayo inampasa kila Muislamu ajitahidi kuiingia na kutekeleza hizo amali njema katika mwezi huu mtukufu wenye kheri na baraka nyingi ili kujichumia mema mengi yatakayomfaa mtu akhera. 

1)     Swawm kwa imani ili Kufutiwa madhambi

قال صلى الله عليه وسلم : (( من صام رمضان إيماناً و احتساباً غفر له ما تقدم من ذنبه ))  أخرجه البخاري ومسلم

Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ((Atakayefunga Ramadhaan kwa imaan na kutegemea malipo ataghufuriwa madhambi yake yaliotangulia )) Al Bukhariy na Muslim.

2)     Qiyaamul-Layl (Kusimama Usiku katika Swalah) Tarawiyh na Tahajjud 

((قال صلى الله عليه وسلم : من قام رمضان إيماناً واحتساباً ، غفر له ما تقدم من ذنبه )) أخرجه البخاري ومسلم

((Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  Atakayesimama (kwa Swalah ya usiku) kwa imani na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia)) Al-Bukhariy na Muslim.

3)      Sadaka

((قال صلى الله عليه وسلم:  أفضل الصدقة صدقة في رمضان ))   أخرجه الترمذي عن أنس

((Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  Sadaka bora kabisa ni ile inayotolewa katika mwezi wa Ramadhaan)) At-Tirmidhy kutoka kwa Anas

4)     Kumfuturisha aliyefunga

((قال صلى الله عليه وسلم :  من فطر صائماً كان له مثل أجره غير أنه لا ينقص من  أجر الصائم شيء )) 

أخرجه أحمد والنسائي وصححه الألبان

((Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم "Atakayemfuturisha aliyefunga, atapata ujira kama ujira wake bila ya kupungua chochote katika ujira wa yule aliyefunga)) Ahmad, An-Nasaaiy na kasahihisha Sh Albani

Na Allaah سبحانه وتعالى Anasema:

}}وَيُطْعِمُونَ الطَّعَامَ عَلَى حُبِّهِ مِسْكِينًا وَيَتِيمًا وَأَسِيرًا{{  

}} إِنَّمَا نُطْعِمُكُمْ لِوَجْهِ اللَّهِ لَا نُرِيدُ مِنكُمْ جَزَاء وَلَا شُكُورًا{{

 }} إِنَّا نَخَافُ مِن رَّبِّنَا يَوْمًا عَبُوسًا قَمْطَرِيرًا{{

 }} فَوَقَاهُمُ اللَّهُ شَرَّ ذَلِكَ الْيَوْمِ وَلَقَّاهُمْ نَضْرَةً وَسُرُورًا{{   

}}وَجَزَاهُم بِمَا صَبَرُوا جَنَّةً وَحَرِيرًا{{                           

{{Na huwalisha chakula, juu ya kukipenda kwake, masikini, na yatima, na wafungwa}}

{{Hakika sisi tunakulisheni kwa wajihi wa Mwenyezi Mungu. Hatutaki kwenu malipo wala shukrani}}

{{Hakika sisi tunaiogopa kwa Mola wetu Mlezi hiyo siku yenye shida na taabu}}

{{Basi Mwenyezi Mungu Atawalinda na shari ya siku hiyo na Kuwakutanisha na neema na furaha}} 

{{Na Atawajazi Bustani za Peponi na maguo ya hariri kwa vile walivyosubiri}} Al-Insaan: 8-12

Vile vile kasema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم :

  (( أيما مؤمن أطعم مؤمناً على جوع أطعمه الله من ثمارالجنة ومن سقى مؤمناً على

ظمأ سقاه الله من الرحيق المختوم ))  رواه الترمذي بسند حسن

((Muumin yeyote atakayemlisha Muumin mwenzake mwenye njaa, Allaah Atamlisha katika matunda ya Peponi, na atakayemnywisha mu'min mwenye kiu Allaah Atamnywesha kutoka 'Rahiyqul-Makhtuum' [Kinywaji safi kilichofunikwa kwa kizibo madhubuti] )) At-Tirmidhiy kwa Sanad nzuri.

5)     Kusoma Qur'aan sana na kujua maana  yake

Mwezi wa Ramadhaan ni mwezi ulioteremshwa Qur'aan kama Anavyosema Allaah سبحانه وتعالى:

}} شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِيَ أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَى وَالْفُرْقَان{{

{{Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur'aan kuwa ni uongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi}} Al-Baqarah: 185

 

Kwa hiyo inampasa Muislamu azidishe kusoma Qur'aan na ajitahidi kukhitimisha japo mara moja katika mwezi huu kama alivyokuwa akifanya Jibriyl عليه السلام wakati akimfundisha Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Qur'aan kila Ramadhaan. Vile vile Maswahaba na Salaf Swaalih (Wema Waliopita) walikuwa wakijihimiza sana kusoma Qur'aan mwezi huu. 'Uthmaan bin 'Affaan رضي الله عنه alikuwa akikhitimisha Qur'aan kila siku mara moja. Na baadhi ya Salaf wakikhitimisha katika Kisimamo cha usiku kila baada ya siku tatu. Na wengineo kila siku saba, na wengine kila siku kumi. Na walikuwa wakiisoma katika Swalah na nje ya Swalah.

 

6)    Kukaa kwa kumkumbuka Allaah baada Swalah ya Alfajiri hadi jua litoke

((عن أنس عن النبي صلى الله عليه وسلم ، أنه قال : من صلى الفجر في جماعة ثم قعد يذكر الله

 حتى تطلع الشمس ثم صلى ركعتين كانت له كأجر حجة وعمرة تامة تامة تامة) )

أخرج الترمذي  صححه الألباني  .

((Imetoka kwa Anas kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema, Atakayeswali Alfajiri katika Jama'ah kisha akakaa anamkumbuka Allaah mpaka likachomoza jua kisha akaswali Raka'a mbili, atapata ujira kama ujira wa kwenda Hajj na 'Umrah ulio kamili kamili kamili)) Imetolewa na At-Tirmidhy na kaisahihisha Albani

(Kuswali Jama'ah imesisitizwa kwa wanaume, ama mwanamke anaweza naye kupata thawabu hizi sawa akiswali nyumbani kwake)

Thawabu hizo ni katika siku za kawaida ndugu Muislamu, seuze mwezi wa Ramadhaan?  Nayo ni fadhila ya siku moja tu, na ikiwa atatimiza kila wiki mara moja, atakuwa ana thawabu za Hajj na 'Umrah mara nne kwa mwezi, na akiendelea hivyo miezi yote kumi na mbili basi atakuwa na thawabu za Hajj na 'Umrah mara 48 kwa mwaka. Yatakuwaje malipo yake akitimiza kila siku? Na hii ni mojawapo ya neema na uadilifu wa Allaah سبحانه وتعالى kwamba hata maskini asiyeweza kujilipia kwenda Hajj au 'Umrah aweze kupata thawabu hizi akiwa nyumbani kwake, tena chumo lenyewe hilo, lenye thawabu nyingi zenye kumshinda hata yule mwenye uwezo wa mali, ni kwa muda wa usiozidi masaa mawili; tokea Alfajiri hadi kuchomoza jua. Hizi ni neema za Allaah ambazo hazipatikani tu katika mwezi huu mtukufu bali zinapatika siku zote.

7)     I'itikaaf

((Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alikuwa akikaa I'itikaaf kila Ramadhaan katika siku kumi za mwisho, na mwaka ambao aliondoka duniani alikaa I'itkaaf siku ishirini)) Al- Bukhariy

I'itikaaf ni ibada ambayo inajumuisha Twa'a nyingi kama tilawat (kusoma) Qur'aan, Swalah, Dhikr na Dua'a, na wala haina tabu. Na fadhila zake ni kubwa mno khaswa katika zile siku kumi za mwisho ndio imo siku ya Laylatul-Qadr. Ni fursa kubwa ya mtu kuweza kuupata usiku huo mtukufu kwa kujiepusha na mambo yanayomshughulisha kila siku ya kidunia na kuulekeza moyo na nafsi yake katika Twa'a kamili kwa Mola wake akiwa msikitini. 

 

8)     'Umrah katika mwezi wa Ramadhaan

Imethibiti katika hadithi kwamba thawaabu za kwenda 'Umrah katika Ramadhaan ni sawa sawa na Hija.

   (( عمرة في رمضان تعدل حجة ))  أخرجه البخاري و مسلم

(('Umrah katika Ramadhaan ni sawa (kwa thawabu) na Hija))  Al-Bukhariy na Muslim

 

9)      Baraka za Suhuur (Daku)

  Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم

 (( تسحروا فإن في السحور بركة ))   رواه البخاري ومسلم  

((Kuleni daku kwani katika huko kula daku, kuna  baraka)) Al-Bukhariy na Muslim  

 

10)    Du'aa

Ramadhaan ni mwezi wa Du'aa pia kwani baada ya Allaah سبحانه وتعالى Kutaja aya za kufunga amendeleza kusema:

}}وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ فَلْيَسْتَجِيبُواْ لِي

 وَلْيُؤْمِنُواْ بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ{{

{{Na waja Wangu watakapokuuliza khabari zangu, waambie kuwa Mimi nipo karibu. Naitikia maombi ya mwombaji anaponiomba. Basi na waniitikie Mimi, na waniamini Mimi, ili wapate kuongoka}}. Al-Baqarah:186

 

11)   Kuomba Maghfirah na Tawbah

Ramadhaan ni mwezi wa Maghfirah na Tawbah na ni fursa kubwa kutumia wakati wa Suhuur (kukesha kwa ajili ya kula daku) kuomba Tawbah na Maghfira kwani Allaah سبحانه وتعالى  ni katika sifa za wenye kupata Pepo.

}}وَبِالأََسْحَارِ هُمْ يَسْتَغْفِرُونَ{{

{{Na kabla ya alfajiri wakiomba maghfira}} Adh-Dhaariyaat 18

Vile vile Allaah سبحانه وتعالى  Huteremka nyakati hizo katika mbingu ya kwanza  :

((عن أبي هريرة رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال:  ينزل ربنا تبارك وتعالى كل ليلة

 إلى السماء الدنيا حين يبقى ثلث الليل الآخر فيقول: من يدعوني فأستجيب له؟ من يسألني فأعطيه؟

من يستغفرني فأغفر له ))

 ((Imetoka kwa Abu Hurayrah رضي الله عنه kwamba Mtume صلى الله عليه وسلم  amesema:  Allaah سبحانه وتعالى Huteremka kila siku katika mbingu ya dunia (mbingu ya kwanza) inapobakia   thuluthi ya mwisho ya  usiku   na Husema:  Nani ananiomba Nimtakabalie? Nani Ana shida Nimtekelezee? Nani ananiomba maghfira  Nimghufurie? ))

 

12)      Kuunga udugu na ujamaa

))  الرحم معلقة بالعرش ، تقول : من وصلني وصله الله ،  ومن قطعني قطعه الله ))  رواه البخاري ومسلم

((Fuko la uzazi linaning'inia katika 'Arshi linasema, atakayeniunga Allaah Atamuunga, na atakayenitenga  Naye Allaah Atamtenga [Atamkatia]))

 

13)   Laylatul-Qadr  

Ni usiku ambao ibada yake ni bora kuliko ibada utakayoifanya miezi alfu.

 }}إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْرِ  {{

 }}وَمَا أَدْرَاكَ مَا لَيْلَةُ الْقَدْرِ  {{

 }}  لَيْلَةُ الْقَدْرِ خَيْرٌ مِّنْ أَلْفِ شَهْرٍ{{

{{Hakika Sisi tumeiteremsha Qur'ani katika Laylatul Qadri, Usiku wa Cheo Kitukufu}}

{{Na nini kitacho kujuulisha nini Laylatul Qadri}}

{{Laylatul Qadri ni bora kuliko miezi elfu}} Al-Qadr 1-3

 

Basi na tujitahidi ndugu zetu tusipoteze fursa kubwa ya kuingia katika milango hiyo mingi ya kheri ili tutoke katika mwezi huu Allaah سبحانه وتعالى Akiwa Radhi na sisi na sisi turidhike Naye. 

 

Tutaendelea Inshaa-Allaah  Ijumaa ijayo. Tumuombe Allaah سبحانه وتعالى   Atunufaishe kwa yale tunayojifunza na Atuajaalie miongoni mwa wale wanaosikiliza kauli (nyingi) wakafuata zile zilizo njema.

Tunawaombea wote Ijumaa hii iwe ya kheri na baraka nyingi. Aamiyn