Waislamu amkeni!
Shukrani
zote ni zake Allah, tunamshukuru, tunategemea msaada kutoka kwake, tunafuata
uongozi wake, tunajilinda kwake kutokana na shari za nafsi zetu na amali zetu
zilizo ovu. Atakayeongozwa na Mwenyezi Mungu
hapana wa kumpotosha, na atakayeachwa kupotea (kwa sababu
ya kukataa kwake kufuata uongofu), hatapata mwengine wa kumuongoza.
Nashuhudia kuwa Hapana Mola anayestahiki kuabudiwa isipokuwa Allah, na kwamba
Muhammad (SAW) ni Mja wake, Mtume wake na mbora wa viumbe vyake. Ameifikisha
amana, amewanasihi Umma, amewatoa watu kutoka katika kiza cha kufru na
kuwaingiza katika Nuru ya Uislamu na amepigana Jihadi katika njia ya Mwenyezi
Mungu kama inavyostahiki. Kwa hivyo tunakuomba Mola wetu umsalie na kumsalimia
Mtume huyu mtukufu pamoja na Aali yake na Masahaba wake wema.
Amma
baad,
Waislamu
wanaanza kupoteza mwamko wa dini yao, na hii inatokana na mazingara mbali mbali
wanayofaridhishiwa na nchi za kikafiri, kama vile kuenezwa kwa filamu chafu,
madishi ya televisheni yasiyosimamiwa yanayotuletea picha zenye utovu wa adabu,
kuenezwa kwa vitabu mbali mbali vilivyojaa kufru na maasia, michezo isiyokuwa na
asili ya Kiislamu, utumiaji wa madawa ya kulevya pamoja na kushughulishwa
Waislamu na kuhifadhi majina na historia za maisha ya wanamichezo mbali mbali,
waigizaji wa sinema, waimbaji, na kila aina ya watu mafasiki badala ya kuhifadhi
majina ya viongozi wao wema walioisimamia dini hii na kuieneza kila pembe ya
dunia tokea siku za mwanzo..
Kwa
ajili hiyo nikaona bora niandike juu ya maisha ya Makhalifa wa Mtume wa Mwenyezi
Mungu (SAW) ili tukumbushane jinsi Masahaba hawa watukufu walivyomuamini Mtume
wao (SAW) tokea siku zile za mwanzo, wakaishi pamoja naye, wakapata tabu na
kuteswa pamoja, wakahama pamoja, na kwa juhudi na ushirikianao mkubwa baina yao
wakaweza kuianzisha dola kubwa ya Kiislamu katika mji wa Madina, dola
iliyofanikiwa kuieneza nuru ya Kiislamu mashariki ya ardhi na magharibi yake,
kueneza uadilifu baina ya watu na kuwatoa watu kutoka katika kiza cha kufru ya
kuabudu masanamu, kuabudu viumbe, kuabudu mizimu, kuabudu wanyama, kuabudu moto
nk. na kuwaingiza katika nuru ya kumuabudu Mungu mmoja Subhanahu wa Taala asiye
na mshirika.
Rudi
Juu
Ikiwa
kila umma unajivunia historia yake, basi sisi Waislamu tuna haki zaidi ya
kujivunia historia yetu iliyojaa uadilifu, huruma, ushujaa, pamoja na uongozi
mwema wenye hekima.
Abubakar,
Omar, Othman na Ali pamoja na masahaba wengine (Radhiyallahu Anhum), na baadaye
akafuata Omar bin Abdul Aziz (RA), wote hawa waliweza kuibeba bendera ya Tawhidi
mara tu baada ya kuondoka duniani kwa kipenzi chao, mwalimu wao na mwalimu wa
ulimwengu mzima, Muhammad (SAW), na kuifanya ipepee bendera hiyo katika kila
pembe ya dunia, hata wakastahiki kupewa sifa ya kuwa umma bora kupita umma zote
zilizodhihirishiwa watu.
Mwenyezi
Mungu Subhanahau wa Taala anasema;
"Nyinyi
ndio umma bora kuliko umma zote zilizodhihirishiwa watu."
Aali
Imran - 110
Na
akasema:
"Na
kumbukeni (enyi Waislamu) mlipokuwa wachache, mkionekana madhaifu katika ardhi;
akakupeni mahala pazuri pa kukaa (Napo ni hapa Madina) na akakutieni nguvu kwa
nusura yake, na akakupeni riziki nzuri ili mupate kumshukuru."
Al Anfal
– 26
Na
akasema;
"Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na walio pamoja naye ni wenye nyoyo thabiti
mbele ya makafiri na wenye kuhurumiana wao kwa wao. Utawaona wakirukuu na
kusujudu pamoja wakitafuta fadhila za Mwenyezi Mungu na radhi yake. Alama zao zi
katika nyuso zao kwa taathira ya kusujudu" .
Al Fat-
h 29
Rudi
Juu
Hawa ndio
mfano bora wa kuigwa
Katika
hadithi sahihi iliyopokelewa na Abu Daud, Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) anasema:
·
"Anayejifananisha na kundi, yuko pamoja nalo".
Na
Mwenyezi Mungu amekwisha tufahamisha kuwa siku ya kiama kutakuwa na makundi
mawili tu:
Kundi la
watu wa Peponi na jingine la watu wa Motoni.
Mwenyezi
Mungu anasema;
·
"Kundi moja litakuwa Peponi na kundi jingine Motoni".
Ashu ura
-7
Kwa
hivyo ndugu zangu Waislamu tujitahidi kusoma juu ya maisha ya Makhalifa wa Mtume
(SAW) na juu ya Masahaba wake waliokwisha bashiriwa Pepo, kisha tuwaige na
kufuata nyayo zao, kwani hawa ni wanafunzi waliohitimu katika chuo cha Mtume wa
Mwenyezi Mungu (SAW) ambao Mwenyezi Mungu Subahanhau wa Taala anatujulisha
katika kitabu chake kitukufu kuwa kesharidhika nao.
Mwenyezi
Mungu anasema:
·
"Na wale walio tangulia wa kwanza, katika Wahajiri (watu wa
Makkah waliohamia Madina) na Ansari (watu wa Madina ambao ndio
waliowakaribisha na kuwapokea waliohama kutoka Makkah), na walio wafuata kwa
wema, Mwenyezi Mungu
ameridhika nao,
na wao wameridhika naye;
na amewaandalia Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele. Huko ndiko
kufuzu kukubwa".
At Tawba
100
Ikiwa
Mwenyezi Mungu kesharidhika nao, bila shaka na Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW)
naye pia kesharidhika nao.
Amma
kuhusu wale wanaopenda kuwaigiza makafiri, basi Mwenyezi Mungu anasema:
·
"Hawatakuwa radhi juu yako Mayahudi wala Wakristo mpaka
ufuate mila
yao, Sema: "Hakika uongozi wa Mwenyezi Mungu ndio uongozi
(khasa). "Na kama ukifuata matamanio yao baada ya yale yaliyokufikia ya ujuzi
(wa kweli) hutapata msaidizi yoyote wala mlinzi kwa Mwenyezi Mungu".
Al
Baqarah - 120
Katika
aya hii Mwenyezi Mungu anawaambia wale wanaojifanya kama vikaragosi kwa kufuata
na kuwaiga Mayahudi na Wakristo kuwa wasifikiri kuiga kwao huko kutawafanya
makafiri hao wawapende, bali kinyume cha hivyo; wanajidharaulisha mbele yao na
wamo katika hatari ya kutopata mlinzi wala msaada wowote mbele ya Mwenyezi Mungu
siku ya Kiama.
Katika
kuyadurusu maisha ya masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW), tutapata
mafundisho mengi ndani yake yakiwemo ucha Mungu wao, jihadi yao, uadilifu wao,
kupendana kwao, namna walivyoishi na kustahamili kila aina ya taabu, mateso, na
kuvumiliana wao kwa wao, na mafunzo haya yatatuwezesha kutuangazia njia
walioipitia ili nasi tujaribu kufuata hatua zao.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu atujulishe nini haki ili tuifuate na atujulishe nini
batili ili tujiepushe nayo - Aamin .
Muhammad Faraj Salem Al Saiy
Rudi
Juu
Nabii
Ibrahim, ndiye aliyejulishwa na Mola wake mahali pa kuujenga msikiti mtukufu wa
Al Kaaba hapo Makkah. Akazinyanyua nguzo zake akisaidiana na mwanawe Ismail -
Sala na Salaam za Mwenyezi Mungu ziwafikie wao pamoja na Mtume wetu mtukufu
Muhammad (SAW).
Baada ya
kulikamilisha jengo la msikiti, Mwenyezi Mungu akamtaka Nabii Ibrahimu
awatangazie watu habari za Hija, awafundishe namna ya kuhiji na namna ya
kumuabudu Mwenyezi Mungu wa Haki asiye na mshirika.
Mwenyezi
Mungu anasema:
"Na
(kumbuka) tulipomkalisha Ibrahimu mahali penye ile Nyumba (Na kumwambia)
"Usinishirikishe na chochote na isafishe Nyumba yangu kwa ajili ya waizungukao
na wanaokaa hapo (kufanya Ibada zao) na wanaorukuu na kusujudu (wanaosali)."
Na (tukamwambia)
"Utangaze kwa watu habari za Hija, watakujia (wengine) kwa miguu na (wengine)
juu ya kila mnyama aliyekonda (kwa machofu ya njiani) wakija kutoka katika kila
njia ya mbali."
Al Hajj
- 26-27
Waarabu
wakauitikia mwito huo, wakawa wanakuja kuizuru nyumba kongwe hiyo kama
walivyofundishwa na Nabii Ibrahim hata baada ya kufariki kwake.
Lakini
baada ya miaka mingi kupita na vizazi vipya kuja, mafundisho ya kutomshirikisha
Mwenyezi Mungu yakaanza kutoweka, itikadi sahihi ikaanza kubadilishwa, na
masanamu yaliyoingizwa ndani ya msikiti huo ndiyo yaliyokuwa yakielekewa,
yakiabudiwa, yakiombwa na kutegemewa.
Masanamu
hayo yaliingizwa na mtu mmoja aitwae Amru bin Luhay, aliyekuwa mkuu wa kabila la
Hudhayl, na hili ni kabila lililokuwa likitawala mji wa Makkah wakati huo.
Lata,
Uzza, Manata, Hubal ni miongoni mwa masanamu yaliyokuwa yakiabudiwa huko Sham
(Syria), na Amru bin Luhay alipokuwa huko katika safari zake za kibiashara
akayachukuwa na kuja nayo mpaka Makkah na kuyaingiza ndani ya nyumba ile kongwe,
kisha akawaamrisha watu wake kuyaabudu na kuwaambia kuwa masanamu hayo yalikuwa
ni picha za watu wema waliotangulia waliokuwa wacha Mungu sana, na kwamba kwa
kufanya hivyo Mwenyezi Mungu ataridhika nao na atazikubali amali zao.
Kwa vile
Amru alikuwa mtu mwenye kuheshimika sana, watu wake wakamsadiki na kuanza kuyapa
heshima kubwa masanamu hayo, ikawa hata watoto wanapozaliwa wakiletwa mbele ya
masanamu na kujulishwa nayo, na haukupita muda mrefu karibu waarabu wote wakawa
wanayaabudu masanamu hayo.
Amru
akapendekeza kila kabila liwe na sanamu lake, kila kijiji kiwe na sanamu lake,
kila taifa liwe na sanamu lake, na kwa ajili hiyo masanamu yakaongezeka na
kuanza kujaa msikitini humo, na idadi yake ikafika masanamu
360, yaliyobomolewa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) siku Waislamu
walipouteka mji wa Makkah.
Maqureshi walikuwa wakiheshimiwa sana na mataifa yote ya Kiarabu, kwa sababu wao
ndio walokuwa walinzi wa nyumba hiyo ya Mwenyezi Mungu.
Safari
ndefu zilikuwa zikifungwa kuelekea huko, majangwa yalikatwa kwa ngamia, kwa
farasi, wengine walipanda punda na wengine walitembea kwa miguu kuelekea katika
nyumba kongwe hiyo, kila mmoja alikuwa na sanamu lake, kila kabila lina mungu
wake, na wengine wanapokuwa safarini walikuwa wakifinyanga tende mfano wa sanamu
kisha wanaliabudu, na njaa inapowashika, humuomba msamaha mungu wao huyo, ambaye
ni tende na kumla.
Mila ya
Nabii Ibrahim ikapotea, na Tawhid aliyoitamka, pale aliposema:
"Mimi
nimeuelekeza uso wangu kwa Yule aliyeziumba mbingu na ardhi hali ya kuwa
nimeacha dini za upotevu. Mimi (ni Mwislamu) si miongoni mwa washirikina".
Al An Am
- 79
Tauhidi hii ilipotea
kabisa.