|
Moja katika mambo makuu yanayohusu ndoa na
kusikika kila siku ni jinsi mke anavyopaswa kuishi na mumewe. Makala mengi na
mawaidha hutolewa kuelewesha haki na wajibu wa ndoa ikizingatia zaidi upande wa
mke. Hali hii imejitokeza kutokana khulka ya mwanamke kimaumbile kuwa dhaifu na
kwa wanaume kupewa
jukumu la kuwa walinzi kwa wanawake na kwa hivyo kasoro nyingi katika ndoa
hunasibishwa na kuwepo kwa hali hizi.
Ni mara chache sana kusikia vipi mume, kama upande wa pili wa ndoa, anapaswa au
kuaswa kuishi na mkewe.
Kwa kiasi fulani maelekezo haya yana nia nzuri tu ya kumuongoza mke katika njia
iliyo sahihi ya kuishi pamoja na kumuenzi mume,lakini kwa upande mwengine
yanaweza kuleta taswira mbaya kwa mume kana kwamba yeye huwa hatendi mambo
kinyume na misingi na taratibu za ndoa ambayo pia kwa upande wake ni wajibu.
Moja katika tatizo kubwa la ndoa zetu ni kwamba wanandoa wanaandaliwa au
kujiandaa kuingia katika maisha ya kuishi pamoja kama mume na mke wakiangalia
zaidi upande wa maisha. Sijui tuilaumu jamii au tulaumu mabadiliko ya mifumo ya
maisha yaliyopelekea kujikuta katika hali hii. Au tuwalaumu wadau katika upande
wa dini kwamba jambo hili hawalitilii mkazo unaopaswa.
Ndugu yetu wa kiislam tayari akishajiona keshajijenga kimaisha ya kumwezesha
kumudu maisha ya ndoa hujiunga katika chuo cha ndoa na kuomba nusra.Na kwa
mantiki hii ile misingi ya ndoa ya kiislam haipewi umuhimu unaostahiki.
Zile mila za wazee wetu zamani kumweka kitako kijana wao na kumfundisha maisha
ya ndoa zimeanza kutoweka kwa kasi kubwa kiasi ya kutishia ndoa nyingi kwa
kutokuwa na misingi madhubuti ya kimaadili, khulka na silka za kiislam.
Ninachokusudia ni kwamba ndoa zetu zimekosa mwelekeo halisi hasa hasa
kiutaratibu. Kwani ndugu zetu wanaingia katika chuo hiki muhimu katika maisha
yao ihali ya kuwa wengi wao hawana maarifa ya kutosha kuhusu umuhimu wa ndoa
katika uislam, haki na wajibu wa mume na mke na pia hadhi kubwa ambayo uislam
umeipa ndoa . Na athari zake ni matukio tofauti yanayojitokeza (mengine ya
kusikitisha) katika ndoa zetu na kwa kiasi kikubwa yasingepaswa kutokea kama
wanandoa wangelikuwa wanaelewa fika kuhusu taratibu za ndoa ya kiislamu na haki
na wajibu kwa kila mmoja wao.
Ieleweke kwamba ndoa ni moja katika alama na
miujiza yake Allah Subhaanahu Wataala Arruum/21
وَمِنْ
آيَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَكُمْ مِنْ أَنْفُسِكُمْ أَزْوَاجاً لِتَسْكُنُوا إِلَيْهَا
وَجَعَلَ بَيْنَكُمْ مَوَدَّةً وَرَحْمَةً
إِنَّ فِي
ذَلِكَ لَآياتٍ لِقَوْمٍ يَتَفَكَّرُونَ
Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni
wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao. Naye amejaalia mapenzi
na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu
wanao fikiri.
Katika aya hii Allah Subhaanahu Wataala
katika kuonesha ihsaani kwa waja wake ametaja vitu vitatu muhimu vinavyojenga
ndoa madhubuti. Utulivu katika maisha, mapenzi na kuoneana huruma.Hivyo
kila mume wa kiislamu anatakiwa avizingatie sana vitu hivi ambavyo ametuzawadia
Subhaanahu Wataala na kuhakikisha vinakuwepo katika ndoa yake, pia
anavienzi na kuvitekeleza ipasavyo.
Kwa mtu kuamua kuoa ieleweke kuwa sio kwamba
anapata mke tu bali ni kuelekea katika kukamilisha dini ukijumuisha na
ulimwengu ndani yake kama hadithi ya Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam)
inavyothibitisha kwamba :
من تزوج فقد
استكمل نصف الإيمان فليتق الله في النصف الباقي » [صحيح الجامع:
"Mwenye kufunga ndoa (atakuwa)
amekamilisha nusu ya Imani (dini yake) na amuogope Allah katika nusu
itakayobakia".
Sahihul
Jaami’i
Katika hadithi hii Mtume (Sallallahu
‘alayhi Wasallam) anatufahamisha hadhi na daraja ya ndoa kwa muislam ni kama
mtu kuwa tayari nusu ya dini yake imekamilika sasa iweje leo ghafla mtu anaweza
kuamua kuondoka katika daraja hii ya juu kabisa ya imani katika dini kwa kufanya
matendo yanayokwenda kinyume na maadili ya dini?
Baada ya kufunga ndoa ifahamike kwamba tokea wakati huo watu wawili hukutana
pamoja na sio kama marafiki tu bali kama patna, mwenza sahiba na kushirikana
katika furaha na huzuni, mafanikio na misiba, matarajio na matatizo na pia
kukabiliana na mitihani na majaribu ambayo yanapatikana ndani yake. Mmojawapo
akipatwa na mitihani anajua kama ana mwenzake wa karibu na kuhakikisha
anamsaidia.
Mnapoamka asubuhi macho yenu yanapofumbua macho hukutana na kusabahiana na
mchana mtakuwa pamoja ikiwezekana na kama mmetingwa na shughuli bado huwa pamoja
kwa kila mmoja kumjali mwenzake na kumtakia kila la kheri katika amali zake na
ukifika wakati wa usiku kitu cha mwisho kwa macho yenu kabla ya kulala ni
kutakiana usingizi wa kheri,kwa ufupi ni kama aya ya Suuratul Baqarah /187
ambayo imekhitimisha maana kamili ya ukaribu wa mume na mke kwa kusema:
هُنَّ
لِبَاسٌ لَّكُمْ وَأَنتُمْ لِبَاسٌ لَّهُنَّ
Wao ni mavazi kwenu na nyinyi na mavazi kwao
Mahusiano ya ndoa kati ya mume na mke ni aina ya mahusiano ya ajabu kabisa
kulinganisha na aina nyengine zote za mahusiano ya binadamu.Daraja ya mapenzi na
mahaba,kuenziana, na kuhurumiana ,amani na "raha" inayajaa katika nyoyo za mume
na mke hazina mfano wake.Kwa ufupi ni vigumu kulijua hili isipokuwa kuirudisha
kwa mwenyewe muumba kwamba ni moja katika rehema zake kwa waja wake.
Maisha ambayo waume siku hizi wanaishi ni maisha yaliyojaa pirika na
kuhangaika na maisha kwa kiasi kikubwa na jambo hilo kupewa kipaumbele kwa
sababu nyingi zikiwemo zile "kama mimi nikikaa ndani tutakula nini ?".Kutingwa
huku kwa shughuli za "kimaisha" kwa kiasi kikubwa kumepelekea mume na mke kuwa
na muda mdogo sana wa kukaa pamoja na hivyo kupelekea ile furaha iliopo na
mahaba pia kupungua(ambayo tumetakiwa na Allah tuyaenzi ). Na hasa ukizingatia
mume huyu atakuwa amerudi ilhali ya kuwa amechoka hata kufanya jambo jengine
lolote hawezi isipokuwa kuupumzisha mwili kwa kujiandaa na pirika za siku
inayofuata. Maisha haya ya kileo yamembadilisha binadamu kutoka hali yake na
kuwa mashine kama ya "robot" ambayo haina hisia na wala kujali kitu chengine
zaidi ya vile ilivyosetiwa..
Tuna mifano mingi hai ya aina ya waume ambao wameondoka na kwenda nchi za mbali
kwenda kutafuta maisha na kuwaacha wake zao nyumbani huku wakijitahidi
kuwahudumia kwa kila wanachokipata. Na hudiriki kuwa mbali na familia – aila -
zao kwa muda mrefu tu .Wengine huwepo hapo hapo nyumbani lakini pirika za maisha
kama tulivyozieleza hazimpi muda wa kutosha kustarehe na mke.Na wengine ambao
wamekwenda nchi za nje pamoja na aila zao lakini mfumo tofauti wa maisha
wanaokuta huko huwafanya kuwa mbali na wake zao kama wale wanaoingia kazini
nyakati za usiku tu mfululizo na wengine kufanya kazi za sulubu na kuwachosha
kiasi cha kushindwa kutekeleza majukumu yao muhimu.
Aina ya pili ya waume tulio nao ni ile ya wale waliokuwa wakionesha mapenzi ya
dhati kabla ya ndoa zao na baada ya fungate tu ile huba iliyokuwepo inapungua
kwa daraja ya kutisha kwa dhana ile ya kuwa sasa tayari nimeshamfunga na kumtia
shemere.Badala ya kuwepo mapenzi na huba hugeuka na kuwa mazoea tu ndiyo
yanayowaweka wanandoa wawili na kama wakijaaliwa watoto basi huwa ni watoto.
Ndoa zilitakiwa zikakamae kwa maana ya kwamba kila siku zikipita ndoa zizidi
kuimarika ,lakini kwa bahati mbaya zetu zinakwenda kinyume chake yaani kila siku
kukicha uimara wake unazidi kupungua na lau kama hakuna kitu chengine cha
kuifanya isimame kama watoto au mazoea basi tayari isingelikuwepo.
Na tumuangalie tena ruwaza (kigezo) - Mtume wetu Muhammad (Sallallahu ‘Alayhi
Wasallam) vipi alivyokuwa akitufundisha sisi waume kuenzi ndoa. Anasema
Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) katika hadithi:
خيركم
خيركم لأهله، وأنا خيركم لأهلي
"Mbora miongoni mwenu wenu ni yule aliye
mbora kwa mkewe na mimi ni mbora kuliko nyinyi wote kwavni mimi ni mwema sana
kwa wake zangu."
Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) alikuwa akionesha mapenzi ya hali
ya juu kwa wakeze kwani alikuwa akicheza na kuwa na wasaa wa kutosha kuwa
pamoja nao na yatosha kupigiwa mfano kitendo chake cha kumwekea goti mkewe ili
aweze kupanda ngamia .Mtume (Salla Allahu ‘alayhi Wasallam) anatoa
bishara njema kwa mume na mke wanaoamshana usiku kwa ajili ya kufanya ibada na
kumhimiza yule anayewahi kuamka kumwamsha mwenziwe hata ikiwa kwa kumrushia maji
baridi kwenye uso wake.Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) alikuwa
akitoka "out " na wakeze kama ilivyoripotiwa alipomchukua mmoja wa wakeze kwenda
kuangalia michezo ya wahabeshi.
Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) alikuwa akifanya haya kama ni
kigezo kwetu jinsi ya kuyahuisha mapenzi na mahaba katika ndoa na kuienzi ili
iimarike.
Hakuna sababu nyengine kubwa ya kuweza kuweka
misingi madhubuti katika ndoa kama hapajawekwa misingi madhubuti ya mahusiano ya
mtu na Allah (Subhaanahu Wataala). Ni lazima mume awe na utulivu wa nafsi
na moyo wake kwa Allah(Subhaanahu Wataala) kwanza kwa kutekeleza yale
yote ambayo Allah(Subhaanahu Wataala) ameamrisha na kuacha yale yote
ambayo amekataza na msingi huu moja kwa moja utampelekea mume kuwa na mahusiano
mazuri kati yake na mkewe.Na endapo mume atakuwa mukhlis kwa Allah(Subhaanahu
Wataala) moja kwa moja mume huyo atakuwa mukhlis kwa mkewe pia.
Na kwa kulisisitiza jambo hili Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam)
anatufahamisha misingi ya uchaguaji mke kwamba katika kuoa, kati ya yale mambo
mane ambayo kwa ajili yake mwanamke huolewa (uzuri, nasaba, mali na dini)
tumchague mwenye dini kwani huyo ndiye atakayekusaidia katika kuhakikisha
mahusiano ya mume na Allah (Subhaanahu Wataala) yanakuwepo pale pale hasa
pakitokea ile hali ya imani kuanza kupungua.Kama anavyosema katika hadithi:
أن رسول الله (صلى الله عليه وسلم) قال: تنكح المرأة لأربع لمالها , ولحسبها
,
ولدينها , فاظفر بذات الدين تربت يداك
ولجمالها
روى البخاري
ومسلم
Hakika Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam
amesema :
Mwanamke huolewa kwa mambo mane: Kwa (ajili
ya) mali yake, kwa nasaba yake, kwa uzuri wake na kwa dini yake, basi mtafuteni
mwenye dini (kwani) mikono yako itatakatika na michanga.
Bukhari na
Muslim
Kwa maana hii hali itakuwa tofauti pale
ambapo mke hana msingi wa dini kwani yeye ni mtu pekee wa karibu wa kuweza
kuielewa hali yako na vipi ataweza kuchangia kuweza kukusaidia.
Yaliyobakia uzuri,nasaba na mali kama
yakiwepo basi huwa ni “bonus” lakini la msingi kulitazama ni maadili na msingi
wa kidini. Wanazuoni wanafafanua busara hizi za Mtume Salla Allahu ‘Alayhi
Wassallam kwamba uwezo na mali bila ya kuwa na dini na taqwa ni hasara.
Uzuri usiokuwa na chembe ya dini ni kiburi na ufisadi. Na nasaba (ukoo)
usioambatana na dini pia ni upotevu na ujilabu na si vyenginevyo. Tunaona mifano
hii katika maisha ya waliooa kwa kufuata moja ya mambo haya bila ya kuzingatia
msingi wa kidini yanayowafika katika maisha yao ya ndoa.
Ndugu yangu, mume wa kiislam, jitahidi kadri ya uwezo wako kuwa mukhlis kwa mkeo
kwa maneno na vitendo kwa kuongea nae, kucheka nae, kustarehe nae, kufurahi nae,
kutafuta ushauri wake, kumsikiliza na kumpa umuhimu anaostahili kama mke
wako.Usiwe mbinafsi wala kutokuwa na imani na mkeo .Kuwa mvumilivu kwa mitihani
itakayokukabili katika ndoa na Allah (Subhaanahu Wataala) amekuandalia
malipo mazuri kama hadithi ya Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam)
inavyofahamisha:
"Mume atakayevumilia usumbufu wa mkewe (kwa
ajili ya Allah) basi Allah atamlipa mume huyo malipo sawa na malipo aliyomwahidi
Nabii Ayyub (‘Alayhi Ssalaam)".
Shirikiana nae katika kazi za nyumbani pale inapowezekana.Tokeni pamoja na wala
msione taabu kufanya hilo na wala isiwe kwa ajili ya kwenda hospitali tu au
kuwaangalia wazee bali mtoke "out " kutembelea ndugu, jamaa na marafiki .Wala
watoto wasiwe kizingiti cha kukuzuieni kufanya baadhi ya mambo yenu kwani
mnaweza kuwa na utaratibu wa kuyafanya yote pasipo kuleta athari. Kumbuka ndoa
hii ina mlinzi anaelinda na anaeiangalia Annisaa/1
يَا أَيُّهَا
النَّاسُ اتَّقُواْ رَبَّكُمُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ وَخَلَقَ
مِنْهَا زَوْجَهَا وَبَثَّ مِنْهُمَا رِجَالاً كَثِيراً وَنِسَاء وَاتَّقُواْ
اللّهَ الَّذِي تَسَاءلُونَ بِهِ وَالأَرْحَامَ إِنَّ اللّهَ كَانَ عَلَيْكُمْ
رَقِيبًا
Enyi watu! Mcheni Mola wenu aliye kuumbeni
kutokana na nafsi moja, na akamuumba mkewe kutoka nafsi ile ile. Na akaeneza
kutokana na wawili hao wanaume na wanawake wengi. Na tahadharini na Allah ambaye
kwaye mnaombana, na jamaa zenu. Hakika Allah ni Mwenye kuwaangalieni
Pia ndoa hii ina wa kuisaidia – Allah
Subhaanahu Wataala- kama anavyosema Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam
katika hadithi:
« ثلاثة حق على
الله تعالى عونهم: المجاهد في سبيل الله ، والمكاتب الذي يريد الأداء
والناكح الذي يريد العفاف
»
[صحيح الجامع
Watu watatu ni hake yake Allah kuwasaidia;
mwenye kupigana jihadi kwa ajili ya Allah, mwenye kuandikiana na Mtumwa (Kwa
ajili ya kuachiwa huru) huku akiwa na nia ya kulitekeleza hilo, na mwenye kutaka
kuoa akitaka kupata sitara na kujizuia na maovu.”
Sahihul
Jaami’i
Mhifadhi mkeo na kila jambo ambalo
litapelekea kutiwa motoni siku ya kiama . Hakikisha unatekeleza haki zake na
kutimiza wajibu wako katika ndoa . Usimchukie mkeo kwa ugomvi mdogo tu na wala
usichukue maneno maneno ya nje tu na kuyatolea hukumu bila ya kuwa na ushahidi
kwani maudhi ya mke ni mengi na ni nadra kuweza kukaa na mke bila ya kuudhiana -
ni maumbile. Mtunukie zawadi kwani ni kitu ambacho kinavuta na kuenzi mapenzi
katika ndoa. Pia msitiri mkeo kwani si miongoni mwa tabia za mume wa kiislamu
kumtajia aibu na dosari za mke wake aliekabidhiwa kwa neno lake Allah
Subhaanahu Wata’aala.
Kwa kuhitimisha, ile kauli wanayoitoa watu wa
dini nyengine pale wanapofunga ndoa kwamba wanakula kiapo cha kupenda na kuienzi
ndoa mpaka kifo kitakapowatenganisha haina nafasi katika uislam kwani mapenzi
hayaishi kwa kutenganishwa na kifo kwani sisi waislam tunaamini kuwepo maisha
baada ya kufa na hivyo kukutana na wake zetu.Attuur/21
وَالَّذِينَ آمَنُوا وَاتَّبَعَتْهُمْ ذُرِّيَّتُهُم بِإِيمَانٍ أَلْحَقْنَا بِهِمْ
ذُرِّيَّتَهُمْ وَمَا أَلَتْنَاهُم مِّنْ عَمَلِهِم مِّن
شَيْءٍ كُلُّ
امْرِئٍ بِمَا كَسَبَ رَهِينٌ
Na walio amini na dhuriya zao wakawafuata kwa
Imani tutawakutanisha nao dhuriya zao, na wala hatutawapunja hata kidogo katika
vitendo vyao. Kila mtu lazima atapata alicho kichuma
Ndugu yangu, mume wa kiislam, mpende mkeo na
penda vile ambavyo mkeo anapenda na sio mpaka kifo kitakapokutenganisheni bali
mpaka mtakapokutana tena huko akhera Inshaallah.
Wabillahi Ttawfiq
|