|
بسم الله الرحمن الرحيم الحمد لله رب العالمين
والصلاة و السلام على سيدنا محمد وعلى آله وأصحابه أجمعين وبعد
Tunauaga mwezi wa Ramadhaan Mtukufu, mwezi wa Baraka na
Rahma, tunaziwaga siku zake za mchana tukiwa katika subira
ya Swawm, na siku zake za usiku zenye ladha ya ibaada.
Tunauaga mwezi wa Qur'aan, mwezi wa Taqwa, mwezi wa Jihaad,
mwezi wa Maghfirah na mwezi wa kuepushwa na moto.
Amefaulu aliyetimizia Swawm ilivyopaswa akachuma mema mengi
na akajitahidi kufanya ibaada zaidi na amekhasirika
aliyepuuza Swawm na sheria zake na asichume mengi, na
akafanya uvivu asiyejitahidi kufanya ibaada zaidi.
Kama
Alivyosema Allaah
سبحانه وتعالى
katika aya zilizotufaridhisha kufunga Ramadhaan kuwa lengo
la Swawm ni kuingia katika Taqwa.
))يَا
أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ
كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ
تَتَّقُونَ((
((Enyi
mlioamini! Mmeandikiwa Swawm,
kama waliyoandikiwa waliokuwa kabla yenu ili mpate kumcha
Mungu))
Al-Baqarah:183
Kwa
hiyo kila Muislamu aliyeingia katika mwezi wa Ramadhaan
atakuwa ameingia katika madrasa ya taqwa. Na mtu anapoingia
katika madrasa yoyote hutoka humo akiwa amepata shahada yake
ya lile somo alilolisoma, na baada ya hapo huitumia ile
elimu aliyoisoma aidha kuifanyia kazi au kumsaidia katika
kuendesha maisha yake yamuongoze katika uhusiano wa tabia
yake pamoja na familia yake, mujtamaa wake na watu wote kwa
ujumla.
Na
huendelea kuitumia hiyo elimu katika maisha yake yote hadi
kufa kwake. Na ni hivyo hivyo ndivyo shahada ya taqwa
inayopatikana katika mwezi huu, elimu yake humuongoza
Muislamu katika uhusiano wake pamoja na Mola wake, familia
yake na watu wote kwa ujumla. Kwa hiyo inampasa Muislamu
aendelee kuitumia elimu hii ya taqwa hadi atakapoonana na
Mola wake kama Alivyosema Allaah
سبحانه وتعالى
(( وَاعْبُدْ رَبَّكَ حَتَّى يَأْتِيَكَ الْيَقِينُ))
((Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie Yakini))
Al-Hijr:99
Na hii
ndio maana ya istiqaamah (kunyooka au kuendelea kuthibiti)
kama Anavyosema Allaah
سبحانه وتعالى
.
((فَاسْتَقِمْ كَمَا أُمِرْتَ وَمَن تَابَ مَعَكَ وَلاَ
تَطْغَوْاْ إِنَّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ))
((Basi, simama sawa sawa kama ulivyoamrishwa, wewe na wale
wanaoelekea kwa Mwenyezi Mungu pamoja nawe; wala msikiuke
mipaka. Hakika Yeye anayaona yote myatendayo))
Huud:112
((فَاسْتَقِيمُوا إِلَيْهِ وَاسْتَغْفِرُوهُ))
((Basi nyookeni sawa kumwendea Yeye, na mumtake msamaha))
Fussilat:6
Kunyooka
katika ibaada vile vile ametufundisha Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
katika Hadiythi ifuatayo:
((عن
أبي عَمْرو، وَقِيلَ: أبي عَمْرَةَ، سُفْيَانَ بْنِ عَبْدِ
اللهِ الثّقَفيِّ رَضيَ اللهُ عَنْهُ قَال: قُلْتُ: يا رَسُولَ
الله، قُلْ لي في الإِسْلاَمِ قَوْلاً، لاَ أَسْأَلُ عَنْهُ
أَحَداً غَيْرَكَ. قَال: "قُلْ: آمَنْتُ باللهِ ثُمَّ
اسْتَقِمْ")).
((Kutoka kwa Abu 'Amr, vile vile (anajulikana kama) Abu
'Amra Sufyaan Ibn Abdillah
رضي الله عنه
ambaye amesema:
Nilisema: Ewe Mjumbe wa Mwenyeezi Mungu, niambie kitu kuhusu
Uislamu ambacho siwezi kumuuliza mtu yeyote ila wewe.
Akasema (Mtume
صلى الله عليه وسلم
) : Sema; Namuamini Allaah, kisha kuwa mwenye kunyooka.
(kwa kuendelea kufanya ibada na kuwa na msimamo madhubuti
katika dini))
[Imesimuliwa na Muslim]
Kuthibitika katika ibaada ya Ramadhaan au msimu wowote wa
ibaada ni alama ya kukubaliwa vitendo vya ibaada
alivyovifanya Muislamu humo na kupotoka na kuingia katika
maasi baada ya kutoka kwenye taqwa ni alama ya kuviharibu
vitendo vyake vyema. Na inampasa Muislamu anapotoka katika
mwezi wa Ramadhaan, hali yake ya twa'a na Mola wake iwe bora
zaidi kuliko ilivyokuwa kabla. Na kuhakikisha hali hii,
jiulize na ujibu maswali haya:
1)
Je, Umekufikia mchana mmoja
kama mchana wa Ramadhaan ukiwa
katika
Swam?
2)
Je, Umekufikia usiku mmoja
kama usiku wa Ramadhaan ukiwa katika Qiyaamul-
Layl?
3)
Je, Umeburudika na kusoma Qur'aan kama ulivyoburudika katika
Ramadhaan?
4) Je,
Umeuburudisha moyo wako kwa dhikr, istighfaar du'aa na
kilio kama
ilivyokuwa hali yako katika Ramadhaan?
Allaah
سبحانه وتعالى
Anapenda vitendo vya mwanaadamu anavyoviendeleza japokuwa
kama ni kidogo vipi, kuliko vitendo vingi kisha
asiviendeleze:
قال رسول الله صلى الله عليه وسلم : (
أحب الأعمال إلى الله أدومها وإن قل)
متفق عليه
Amesema Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
((Vitendo Anavyovipenda Allaah
سبحانه وتعالى
zaidi (kuliko vyote) ni vile vinavyodumishwa japokuwa ni
vidogo)).
[Al-Bukhaariy na Muslim]
Kwa hiyo nyooka ewe ndugu Muislamu kwa kujiendeleza kufanya
vitendo vyema na ibada katika miezi mingine yote kama
ulivyokuwa ukifanya katika mwezi wa Ramadhaan nazo ni:
SWAWM
Funga siku sita za mwezi wa Shawwaal ili ujipatie thawabu
za kufunga mwaka mzima kama alivyosema Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
))
من صام رمضان ثم أتبعه ستاً من شوال كان كصيام الدهر))
رواه
مسلم و الترمذي و ابن ماجه , أبو داود و أحمد
((Yeyote atakayefunga mwezi wa Ramadhaan, kisha akafuatia
kwa kufunga siku sita za mwezi wa Shawwaal, basi atapata
ujira wa aliyefunga mwaka mzima)).
[Imepokewa na Maimaam Muslim, At Tirmidhy, Ibn Maajah, Abu
Dawood na Ahmad ]
Vile
vile kuna Swawm za Jumatatu na Alkhamiys, siku tatu katika
mwezi, (Ayyaamul-Baydh), Swawm ya Arafat, swawm ya 'Ashuraa
na zote zimetajwa fadhila zake katika mada inayopatikana
katika TAWHIYD kwenye kiungo hiki kifuatacho:
>>SWAWM ZA
SUNNAH NA UMUHIMU WAKE<<
QIYAAMUL-LAYL (kisimamo cha kuswali usiku)
Ni
Swalah ya Sunnah iliyo bora kabisa baada ya Swalah ya Fardh
kama ilivyo katika Hadiythi ifuatayo:
((أفضل الصلاة بعد الفريضة صلاة الليل))
رواه مسلم.
((Swalah iliyo bora kabisa baada ya Fardh ni Swalah ya
usiku))
[Muslim]
Na
fadhila zake zimetajwa nyingi sana, ingia katika vitengo
vifuatavyo utambue fadhila zake:
>>FADHILA ZA QIYAAMUL-LAYL - 1<<
>>FADHILA
ZA QIYAAMUL-LAYL - 2<<
SADAQAH
Ikiwa
kutoa sadaqa katika Ramadhaan kumekwisha, basi kuna Fardhi
ya Zakaah, na kuna milango mingi ya kutoa sadaqah pamoja na
kutoa katika Jihaad fiy Sabiyli-LLah (Jihaad katika njia ya
Allaah).
KULISHA MASIKINI
Ni
jambo Analolipenda Allaah
سبحانه وتعالى
na Amelisisitiza katika Qur'aan na kuonya asilipuuze mwenye
uwezo wa kufanya hivyo kwani miongoni mwa
watu wa motoni walipoulizwa sababu za kuweko humo
walijibu kuwa baadhi ya sababu ni:
((مَا سَلَكَكُمْ فِي سَقَرَ))
((قَالُوا لَمْ نَكُ مِنَ الْمُصَلِّينَ))
((وَلَمْ نَكُ نُطْعِمُ الْمِسْكِينَ))
((Ni nini kilicho kupelekeni Motoni))
((Waseme: Hatukuwa miongoni waliokuwa wakisali))
((Wala hatukuwa tukiwalisha masikini))
Al-Mudathir: 42-44
KUTENDA WEMA NA UKARIMU
Ikiwa
Ramadhaan ilikubadilisha tabia yako ukawa unatenda wema kwa
wazazi, ndugu, jamaa na jirani, basi kutenda wema huko
kuendelee miezi yote mingine.
Na
vitendo vingi vyenginevyo inampasa Muislamu aendelee navyo
siku zote wakati wote.
Tunatoa
Nasiha za dhati kwa ndugu Waislamu waliofunga Ramadhaan
ipasavyo, kuendelea kuthibiti katika taqwa na kumshukuru na
kumuomba Allaah
سبحانه وتعالى
Akusaidie kuwa katika hali hiyo bila ya kurudi nyuma. Wala
usiwe kama yule aliyeshona nguo yake akaipenda sana kisha
akaiharibu kwa kuivuta uzi bila ya sababu kama mfano wa
mwanamke mmoja aliyekuwa Makkah ambaye alikuwa akifuma uzi
na kuufanya madhubuti kisha kila ukiwa madhubuti huufumua,
naye Amemtaja Allaah
سبحانه وتعالى
:
((وَلاَ تَكُونُواْ كَالَّتِي نَقَضَتْ غَزْلَهَا مِن بَعْدِ
قُوَّةٍ أَنكَاثًا))
((Wala msiwe kama mwanamke anayeuzongoa uzi wake baada ya
kwisha usokota ukawa mgumu))
An-Nahl:92
Hii ni
kama hali ya mwenye kurudia katika ma'asi baada ya kutoka
katika Ramdhaan na akaacha kuwa na twa'a na kufanya mema,
akawa badala ya kuitumia neema ya kuwasiliana na Mola wake
na kuwa karibu Naye, akarudi katika madhambi. Waovu walioje
watu wanaomtambua Allaah
سبحانه وتعالى
katika Ramadhaan pekee.
Alipofariki Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
, Maswahaba walikuwa katika vilio na huzuni kubwa za ajabu
hadi wengine walipigwa na bumbuwazi, na 'Umar
رضي الله عنه
alifika hadi kusema "Atakayesema
Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
Amefariki nitamuua". Walivunjikwa
moyo sana hadi hali ikawa sio ya kupendeza, ndipo Abu Bakar
رضي الله عنه
Akawaambia:
"من كان يعبد محمد فمحمد قد مات
ومن كان
يعبد الله فان الله باقي حي لا يموت"
"Yeyote aliyekuwa anamuabudu Muhammad, basi Muhammad
amefariki na yeyote aliyekuwa anamuabudu Allaah, basi Allaah
Anabakia, Yu hai Hafi"
Hali
kadhalika tunasema
'aliyekuwa anaabudu Ramadhaan, basi Ramadhaan inapita na
aliyekuwa anamuabudu Allaah, basi Allaah Anabakia, Yu hai
Hapiti kuondoka (Hafi)"
Kutokuwa katika istiqaamah baada ya Ramadhaan kunadhihirika
kwa njia kama zifuatazo:
1) Kupuuza
Swalah
Kutokuswali Swalah za Fardhi, au kutokuziswali kwa wakati
wake au kutokuziswali kwa kwa utulivu kama ipasavyo.
2) Kuacha
kuswali Jama'ah misikitini
Swalah
ya Jama'ah ni jambo liliosisitizwa sana na Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
sio Ramadhaan tu, bali siku zote za kawaida. Lakini utaona
misikiti inajaa watu siku za Ramadhaan khaswa katika Swalah
ya Tarawiyh ambayo ni Sunnah, wakati Swalah za fardhi ndizo
muhimu zaidi. Na fadhila nyingi zimetajwa katika Sunnah
anazozipata Muislamu kuswali Jama'ah.
3) Kuacha kusoma Qur'aan na kujua maana yake
Wengine huijua Qur'aan katika Ramadhaan tu, ikimalizika
Ramadhaan, misahafu inarudishwa katika kabati ijae vumbi
hadi Ramadhaan nyingine, wakati Qur'aan ni uongofu kamili
wetu, na ina manufaa makubwa sana katika maisha yetu kwa
kila upande kwani imekusanya neema zote humo zenye manufaa
kwetu kama Anavyosema Allaah
سبحانه وتعالى
((يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءتْكُم مَّوْعِظَةٌ مِّن
رَّبِّكُمْ وَشِفَاء لِّمَا فِي الصُّدُورِ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ
لِّلْمُؤْمِنِينَ))
((قُلْ بِفَضْلِ اللّهِ وَبِرَحْمَتِهِ فَبِذَلِكَ
فَلْيَفْرَحُواْ هُوَ خَيْرٌ مِّمَّا يَجْمَعُونَ))
((Enyi watu! Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu
Mlezi, na poza kuponyesha yaliyomo vifuani, na uongofu, na
rehema kwa Waumini))
((Sema: Kwa fadhila ya Mwenyezi Mungu na rehema yake! Basi
nawafurahi kwa hayo. Haya ni bora kuliko hayo
wanayoyakusanya)
Yunus: 57-58
Vile
vile ni muhimu sana Muislamu ajue maana ya maneno ya Mola
wake ili atambue maamrisho na makatazo yake, sheria zake
anazozihitaji katika maisha yake, na vile vile Qur'aan ni
kipumbazo cha moyo kwani humo kuna visa vya Mitume na watu
wa kale ambavyo vina mafundisho mazito kwetu na masimulizi
ya kuburudisha nyoyo.
4) Kurudia katika mambo ya upuuzi
Inampasa Muislamu aendelee kujiepusha na mambo ya upuuzi
kama kutazama michezo ya televisheni, kusikiliza nyimbo,
kukaa barazani kupiga soga, kusengenya katika simu, kusoma
vitabu visivyo vya elimu na haswa elimu ya dini ya Kiislamu
na kadhalika, na badala yake anatakiwa ajitahidi autumie
wakati wa thamani katika kutafuta elimu ya dini yake tukufu
na kuutumia wakati wake wote katika yale yenye kumridhisha
Mola wake tu. Kujiepusha na mambo ya upuuzi ni moja wa
sababu ya kumrithisisha Muislamu Pepo ya Firdaws kama
Anavyosema Allaah
سبحانه وتعالى
katika aya ifuatayo:
((وَالَّذِينَ هُمْ عَنِ اللَّغْوِ مُعْرِضُونَ))
((Na ambao hujiepusha na mambo ya upuuzi))
Al-Muuminuun:3
Ndugu Muislamu, endelea kunyooka katika taqwa siku zote,
wakati wote, kwani hujui lini Malaika wa kuchukua roho
atakuwa mgeni wako. Jihadhari kukutana naye wakati uko
katika ma'asi na jitayarishe uwe katika wale ambao
wanapofikiwa na Malaika wa roho uambiwe :
((يَا أَيَّتُهَا النَّفْسُ الْمُطْمَئِنَّةُ))
((ارْجِعِي إِلَى رَبِّكِ رَاضِيَةً مَّرْضِيَّةً))
((فَادْخُلِي فِي عِبَادِي))
((وَاد ْخُلِي جَنَّتِي))
((Ewe nafsi iliyo tua))
((Rejea kwa Mola wako Mlezi umeridhika, na umemridhisha))
((Basi ingia miongoni mwa waja wangu))
((Na ingia katika Pepo yangu))
Al-Fajr: 27- 30
Tunamuomba Allaah
سبحانه وتعالى
Atutakabalie 'amali zetu zote tulizozifanya katika Ramadhaan
na Atuhidi kutuendeleza kunyooka katika taqwa na wenye
kuzidisha kufanya vitendo vyema siku zote, wakati wote hadi
tutakapokutana Naye Mola wetu Mtukufu tuwe miongoni mwa wale
walioamini na Atuingize Peponi kama Alivyotuahidi katika
kitabu chake Kitukufu:
((إِنَّ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ
أُوْلَئِكَ هُمْ خَيْرُ الْبَرِيَّةِ))
((جَزَاؤُهُمْ عِندَ رَبِّهِمْ جَنَّاتُ عَدْنٍ تَجْرِي مِن
تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا أَبَدًا رَّضِيَ
اللَّهُ عَنْهُمْ وَرَضُوا عَنْهُ ذَلِكَ لِمَنْ خَشِيَ
رَبَّهُ))
((Hakika
walioamini na wakatenda mema, hao ndio bora wa viumbe))
((Malipo yao kwa Mola Wao Mlezi ni Bustani za daima,
zipitazo mito kati yake. Wakae humo milele. Mwenyezi Mungu
Yu radhi nao, na wao waradhi Naye. Hayo ni kwa anaye mwogopa
Mola wake Mlezi))
Al-Bayyinah: 7-8
Du'aa
ya Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم
ya kututhibitisha nyoyo zetu katika Dini yetu tukufu.
اَللَّهُمَّ يَا مُقَلِّبَ الْقُلُوبِ ثَبِّتْ قَلْبِي عَلَى
دِينِك
Allaahuuma Yaa Muqallibal-Quluub Thabbit Qalbiy 'Alaa Diynik
Allaahuumma, Ewe Mgeuza nyoyo, thibitisha moyo wangu katika
Dini Yako
اّللَّهُمَّ ياَ مُصَرِّفَ الْقُلُوب صَرِّف قُلُوبَناَ عَلَى
طَاعَتِك
Allaahuumma Ya Muswarrifal-quluub Swarrif Quluubana 'Alaa
Twaa'atik
Allaahumma, Ewe Muelekezaji wa nyoyo, Elekeza nyoyo zetu
katika Twa'aa Yako
Na Allaah
Anajua Zaidi
|