TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 » Sunnah  

RAMADHANI HUMALIZIKA/HUISHIA NA EID?

Imefasiriwa na : Ummu Ahmad

Ukimuuliza Muislamu yeyote suala hili bila shaka utapata jawabu la “ndio”, Ramadhani huisha ile siku tunayojumuika pamoja kwa furaha kusheherekea ‘Eid-el-Fitri. Maamrisho ya kujizuwia kula, kunywa  na mashirikiano ya kimwili kati ya mke na mume wakati wa mchana wa Mwezi wa Ramadhani tunayapata moja kwa moja kutoka kwenye Kurani Tukufu na  Hadithi za Bwana Mtume (S.A.W).  Lakini kwa kweli kama tutachunguza kwa undani baraka za Mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani, tutaona kwamba mafunzo yake yanakusudiwa kubakia na kutekelezwa na kila mmoja wetu baada ya kumalizika kwa chuo hichi adhimu kwa muda wote utakaofuatia baada ya Ramadhani.



Kwanza kabisa, suala zima la kujizuwia na kula, kunywa na matamanio ya kiwiliwili kutoka alfajiri hadi magharibi tunapata mafundisho maalumu. Katika mafunzo hayo ni pamoja na:

1)     Utulivu na Upole

2)     Kuwa na tafakur
 
3)     Kuishi ndani ya Qur'ani

4)     Kuwafikiri waja wenzetu na hali ya Umma wa Kiislam kwa ujumla

 5)    Kujiweka mbali na mapambo na matamanio ya vitu vya kidunia
 

Mafunzo haya  na neema nyingi nyingi yatatuwezesha,  kwa uwezo wa Allah, kutupa faida ya hali ya juu ya uvumilivu na ustahamilivu katika nafsi zetu. Mwenye Enzi Mungu Anasema katika Kurani tukufu:

((Enyi mlioamini! Takeni msaada kwa subira na Sala. Hakika Mwenyezi Mungu Yu pamoja na wanaosubiri))
 [Sura Al-Baqarah  153]



Kumpenda Allah (s.w.t) na kumtii kwa maamrisho Yake ndio  msingi wa ibada na ndio lengo hasa la sisi wanaadamu kuwepo hapa ulimwenguni. Kwa ajili hiyo basi tunapojiuliza na kutafakari mafunzo tunayopata ndani ya Ramadhani na umuhimu wake kwa maisha yetu ya kila siku, inatubainikia kuwa lengo hasa la kuingia kwenye chuo hichi adhimu ni kuziweka nyoyo zetu ndani ya taqwa  ya kumtii Allah (s.w.t.) kwa muda wote unaofuatia baada ya Ramadhani karimu.

Mwenyezi Mungu anasema ndani ya Kurani tukufu:

((Enyi watu! Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na poza kuponyesha yaliyomo vifuani, na uwongofu, na rehema kwa Waumini))

((Sema: Kwa fadhila ya Mwenyezi Mungu na rehema Yake! Basi nawafurahi kwa hayo. Haya ni bora kuliko hayo wanayo yakusanya))

[Sura Yunus   57 – 58]


Hivyo basi ni wazi kabisa kuwa ibada ya funga ya Ramadhani ni katika nguzo kubwa  iliyo muhimu ya  dini ya Kiislam iliyokusudiwa kutusaidia kama wanaadamu katika kufanikisha  lengo la kuwepo kwetu duniani kama makhalifa wa Allah  (s.w.t.).



Kwa kuwa Ramadhani ni chuo adhimu cha kutuleta ndani yake taqwa pale tunapokuwa wastahamilivu na wanyenyekevu katika kufuata maamrisho ya Allah ndani ya nafsi zetu tunapata faida ya kuwa waadilifu na kuipigania njia ya Mwenyezi Mungu ndani ya nafsi zetu kwanza. Vita hivi vya kuzilea nafsi kwa ajili ya Allah(s.w.t.), huitwa Jihaad.



Jihad inakusanya yale yote, kuanzia vita dhidi ya makafiri na ushirikina na yale yote yaliyokatazwa na Allah (s.w.t.) ili kupata daraja ya juu kabisa ya mafanikio katika maisha ya Muislamu mbele ya Allah (s.w.t.) Mwenyeezi Mungu Anasema katika kurani tukufu:

((Wale walioamini, na wakahama, na wakapigana Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yao na nafsi zao, hao wanacheo kikubwa zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu. Na hao ndio wenye kufuzu.
 [Sura Taubah 9:20]

Wengi wetu huelewa neno Jihaad kwa maana finyu kabisa, ya kuchukua silaha na kwenda vitani. Kwa mafundisho ya Bwana Mtume (s.a.w) kwenda vitani ni katika jihadi ndogo. Jihadi kubwa haswa ni kupigana na nafsi zetu kwa kuwacha yale yote tuliyokatazwa na Allah (s.w.t.) na
Mtume wake (s.a.w.)  na kufanya yale tuliyoamrishwa ndani ya Uislamu.

 

Kwa kufanya hivyo tu ndio tutafuzu mbele ya Allah (s.w.t.) kwa kuishi maisha bora hapa duniani na kutarajia mema kesho akhera.

 

Hivyo basi kwisha kwa Ramadhani isiwe ndiyo mwisho wa sisi kufanya mema na kuishi nje ya mipaka ya Allah(s.w.t.), bali tubebe tabia zote njema tulizojifunza ndani ya mwezi huu mtukufu na kwa kufanya hivyo tu , ndio tutakuwa Waislamu wa kweli.