TAWHIYD
    Tawhiyd

Qur'aan

Sunnah

Fiqhi

Makala

Nasiha Ya Ijumaa

Dua na Adhkaar

'Aqiyda-Tawhiyd

Vitabu

Darsa za Wanawake

    Sikiliza

Qur'aan

Mawaidha

Dua

Nashiyd

    Tizama

Video

 »  Ramadhan  

Salamu za ‘Iydil-Fittri

 Assalaamu'Alaykum Warahmatu Llahi Wabarakaatuh,

 

Shukrani zote ni zake Subhanah Yule anaye mjibu (muitikia) mwenye shida pale anapo muomba, Maalik yawmid Diyn, Maalik asiye Mpinzani wa Siku isiyo shaka wala wasi wasi kuja kwake, siku ambayo watu watagawika makundi mawili makubwa; kundi moja litakuwa la watu wa Peponi, na kundi jengine ni la watu wa Motoni.

Rehma na Amani za Allah zimfikie Al-Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Aalihi Wasallam) aliyepewa ujumbe kupitia Qur-an kututaka waislamu tujihadhari, tujitayarishe na tujiandae na siku hiyo, kwani kila mmoja wetu atalipwa kwa alichochuma na kuwa mmoja kati ya makundi mawili, Qur-an inasema :

  وَاتَّقُواْ يَوْمًا تُرْجَعُونَ فِيهِ إِلَى اللّهِ ثُمَّ تُوَفَّى كُلُّ نَفْسٍ مَّا كَسَبَتْ وَهُمْ لاَ يُظْلَمُونَ

Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Allah, kisha kila nafsi italipwa ilicho chuma. Nao hawatadhulumiwa” al-Baqarah aya ya 281.

Ayuhal Ahibaa,

Namshukuru Mola wangu na wako, Mola Mlezi anaewabashiria wenye kufaulu na kufuzu rehma zitokazo kwake, na radhi zake, na Jannaatin (mabustani) ambayo humo watapata neema za kudumu.

Namshukuru Mola wangu na wako, Mwenye kutoa hakikisho kuwa wenye kufaulu katika mitihani mingi (ukiwemo huu wa Ramadhan) watadumu humo (katika Jannaatin) milele.

Namshukuru Mola wangu na wako, Mola aliyetoa changamoto kwa kila mwenye kujaaliwa kushinda katika mashindano aliyoyatangaza kuwa kwake Yeye yapo malipo makubwa yenye kuvutia na kufurahisha kwa kila mwenye kumtarajiya, kumkumbuka sana na kuyatekeleza yale yote ayatakayo Yeye Subhanah.

Ndugu yangu katika iman, napenda kutumia nafasi hii kujiusia nafsi yangu kwanza na nafsi zenu kumcha Allah Subhaanahu Wata’ala kwa kumtii, na Ndugu kwa kutekeleza kila aloliamrisha kadiri ya uwezo wetu, na kujikataza na kila alichokikataza mara moja.

                

Ndugu yangu katika iman, kwa munasaba huu mtukufu napenda kusema: ‘Iyd Mubarak kwa nyote na familia zenu na kwa kila aliyejaaliwa kutekeleza ibada ‘adhiymu ya saum kama alivyotakiwa aitekeleze na Dhul Jalaali wal Ikraam.

 

Ndugu yangu katika iman, ‘iyd katika Uislamu ni ibada hivyo tunatakiwa tujiandae na ibada hii, ibada ambayo inaonyesha shukrani zetu kwa Rahmaan kwa kutuwezesha kuishi na Ramadhan na kutuwafikisha kumuaga mgeni wetu, mgeni ambaye tunamtarajia awe amekubaliwa na Mwenye kuwakubalia Muttaqiyn.

Ndugu yangu katika iman, kuondoka kwa mgeni wetu mtukufu kunatupeleka kuwa na siku yenye kueleweka na sote kuwa ni ‘Iydul-Fittri , siku ambayo ni mahafali (sherehe) kwa sisi sote tuliojaaliwa kuhudhuria mafunzo/masomo katika chuo kikuu cha Ramadhan. 

Ndugu yangu katika iman, kwa kuwa sote tulihudhuria darasa katika masiku machache yaliyopita hivyo ni vyema tuelewe kuwa siku ya kuwepa shahada na nishani zetu ndio imefika, kama tulihudhuria darasa na kuwa haadhir katika darasa letu kwa kuiishi na kukaa vyema na mgeni wetu mtukufu (Ramadhan), basi insha Allah tutapata yale wanayoyatarajiwa waliohudhuria darasa (waliofunga na kusimama) katika masiku machache ya mgeni wetu Ramadhan.

Ndugu yangu katika iman, mgeni wetu Ramadhan ameondoka baada ya kuishi na kukaa na sisi na insha Allah amewafikishwa kuifanya kazi ngumu kabisa, kazi ya kutusafisha na kutukosha kwa vyenye kusafisha na kukosha (sala, sadaqaat, saumu, dhikr, visimamo vya usiku, tiwatul Qur-an, kufutarisha, kuhudhuria mihadhara, kusikiliza mawaidha, istighfaar na kadhalika) na kutusuuza kwa maji safi yenye uwezo wa kusuuza na kuondowa kila aina ya uchafu tuliokuwa nao na kuondoka hali ya kuwa tuko katika usafi insha Allah usafi wa mtu aliyezaliwa na mama ake!

 

Ndugu yangu katika iman, Ramadhan imeondoka baada ya kutusafisha na kutuweka safi, itakuwaje tujitose katika uchafu wa matope wa kila aina ya mambo yaliyokatazwa na Mola wangu wa wako siku ya kwanza tu baada ya Ramadhan kuondoka! 

 

Ndugu yangu katika iman, kama tuna uhakika (hakuna wenye uhakika sote tunataraji tu) wa kukubaliwa kwa mgeni wetu (Ramadhan) na Rahmaan, basi siku ya ‘iyd ni siku ya kushukuru na kufurahi kuwa saumu yetu imekubaliwa, na furaha na shukrani za kukubaliwa kwa ‘amali yo yote ile huwa kwa kufanya yenye kuridhiwa na Jabbaar na sio kinyume chake.

Ndugu yangu katika iman, kama tulikuwa hatuna furaha kwa kuwa Ramadhan imekuja kutunyima uhuru wetu (kufanya tuyatakayo) na sasa tumefurahi kwa kuondoka kwake, kwani tumepata uhuru wetu hivyo tutawaonyesha wasio jijuwa na kuelewa demokrasia (mtu kufanya au kusema alitakalo hata kumuasi Mola wake), maendeleo na vipi kuishi katika dunia hii (bila ya kuingiliana kwa kuamrishana mema na kukatazana mabaya), tutawaonyesha kwa kupanga kufanya kila lenye kumuasi Mola na Mjumbe wake, kumuudhi Mola na Mjumbee, kutuondoshea utu wetu, kuthibitisha kuwa sisi hatuna haya wala hatuoni vibaya, tutahakikisha kwa wale waliokuwa wakitutaka tule na tunywe (katika masiku ya Ramadhan) kuwa tulikuwa hatufungi lakini tulikuwa tukitekeleza ada, mila na desturi tulizokuwa tukiwaona wakitekeleza wazee wetu, bali tulikuwa tukiwacheza shere hawa wasiotaka maendeleo au wasioendelea juu ya kuwepo kwao huku ulaya bado wanasali na kufunga kama wajinga wenzao waliotangulia. Hivyo tutapanga kufanya na kuhakikisha tunatoa kila tulichanacho (nafsi zetu na mali zetu) katika kumuasi na kutekeleza yote yale aliyoyakataza Rahmaan (twamuomba Jabbar atuhifadhi na shari za watu hawa na wengine kama hawa hata kama ni ndugu zetu au jamaa zetu na jirani zetu), kama walivyopanga kufanya majahili kama hawa:

(TAARIFA YA MALIKO, BISMILLAAHI RAHMAANI RAHIIM

Kwa kusherehekea kumalizika mwezi mtukufu wa Ramadhan, Bi XXX wa Slough na Bi YYY wa Derby pamoja na wenzao wana furaha ya kuwaalika waislam wote wa kike na wa kiume katika sherehe za Idi zitakazofanyika katika ukumbi wa Britwell, Slough; siku ya Jumatatu tarehe 23/10/06 kuanzia saa nane za mchana hadi saa nne za usiku.  Chakula na vinywaji vya aina zote vitakuwepo, vikifuatiwa na burudani ya Rusha Roho na Disco Toto pamoja na magoma moto moto ya aina zote.  Nyote munakaribishwa pamoja na watoto wenu kuja kufurahia siku kuu.

Kingilio ni £ 5.00 .  Tafadhali muarifu mwenzako.)

Mambo kama haya hayafanywi, hayatangaziwi, hayaenezwi na wala hashiriki au hata kutowa fikra na mawazo wachilia mbali kuhudhuria (hata kama utakodiwa na kulipwa kupeleka watu au vifaa au vyakula au vinywaji) mwenye kutaraji kukubaliwa Ramadhan yao, kutolewa katika moto na kusamehewa majidhambi yao, wachilia mbali wenye kutarajia kukutana na Mola wangu na wako Mlezi.

Ndugu yangu katika iman, kumalizika kwa mwezi tena mtukufu sherehe huwa na heshima na desturi zilizowekwa na Rahmaan.  Ndugu yangu katika iman, fikiria ni wangapi ulisali nao ‘iyd mwaka jana? Wako wapi leo, wamekwenda wapi?

Ndugu yangu katika iman, ni kweli sherehe itakuwa sherehe ya kusheherekea kumalizika funga kwa kukusanyika wake kwa waume na vinywaji vya aina zote!  Ni kweli sherehe itakuwa sherehe yenye kustahiki kuhudhuriwa na waliokuwa wenyeji wa Ramadhan katika masiku machache na matukufu huku wakijigamba (kama inavyothibitisha matendo na mipango yao) na kujisifu kuwa wao hawana khofu wala wasi wasi na moto wa Jahannam!

Ndugu yangu katika iman, roho unairusha, itaangukia wapi kama sio motoni?  Motoni ambako huna uhakika kama ulikuwa miongoni mwa waliotolewa (na kama ulikuwa miongoni mwa waliotolewa –jambo ambalo ni muhali- huoni haya kurudi jela siku ile ile uliotolewa) katika Ramadhan au bado umebakishwa humo humo kwa upotofu wako!  Qur-an inasema:

       أُوْلَـئِكَ الَّذِينَ اشْتَرُوُاْ الضَّلاَلَةَ بِالْهُدَى فَمَا رَبِحَت تِّجَارَتُهُمْ وَمَا كَانُواْ مُهْتَدِينَ

Hao ndio walio nunua upotofu kwa uwongofu; lakini biashara yao haikupata tija, wala hawakuwa wenye kuongoka al-Baqarah aya ya 16.

Ndugu yangu katika iman, muislamu hutarajiwa kununuwa uongofu na sio upotofu (kingilio ni £5.00), Qur-an inasema:

   وَمِنَ النَّاسِ مَن يَشْتَرِي لَهْوَ الْحَدِيثِ لِيُضِلَّ عَن سَبِيلِ اللَّهِ بِغَيْرِ عِلْمٍ وَيَتَّخِذَهَا هُزُوًا

                               أُولَئِكَ لَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ

Na miongoni mwa watu wapo wanao nunua maneno ya upuuzi, ili wawapoteze watu na njia ya Allah pasipo kujua, na wanaichukulia ni maskhara. Hao watapata adhabu ya kuwafedhehesha  al-Luqmaan aya ya 6.

Ndugu yangu katika iman, kiingilio £5.00, vipi kuhusu zakaatul fittri! Magoma ni moto moto, wewe ulikuwa ukiomba katika masiku machache na matukufu utolewe katika moto na baada ya kuondoka Ramadhan unanunua Moto mmoja kwa moto moto!  Tunajilinda na Allah, Moto wa Jahannam haukutoshi unataka zaidi!

 

Ndugu yangu katika iman, hii ndio hali zetu kwa uhakika (Bi XXX wa Slough na Bi YYY wa Derby pamoja na wenzao wana furaha ya kuwaalika), huu ndio uislamu wetu, hii ndio iman, ‘aqidah na matarajio yetu kwa Mola wetu!  Hivyo kweli sisi ni waislamu !  Qur-an inasema:

 

   الْمُنَافِقُونَ وَالْمُنَافِقَاتُ بَعْضُهُم مِّن بَعْضٍ يَأْمُرُونَ بِالْمُنكَرِ وَيَنْهَوْنَ عَنِ الْمَعْرُوفِ وَيَقْبِضُونَ أَيْدِيَهُمْ نَسُواْ اللّهَ فَنَسِيَهُمْ إِنَّ الْمُنَافِقِينَ هُمُ الْفَاسِقُونَ

 

Wanaume wanaafiki na wanawake wanaafiki, wote ni hali moja. Huamrisha maovu na huyakataza mema, na huifumba mikono yao. Wamemsahau Allah, basi na Yeye pia amewasahau. Hakika wanaafiki ndio wapotofu.” At-Tawbah aya ya 67.

 

 Ndugu Waislamu, lengo letu katika maisha yetu ya kila siku hapa duniani liwe ni kumridhisha Jabbar pekee, hivyo kila tunachokisema au kukitenda au kiandika tuwe na ikhlasi ndani yake kwa iman na kusudio la kumridhisha Allah pekee. 

 

Ndugu Waislamu, ni vyema tuelewe kuwa al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) hakutumwa isipokuwa awe ni mwenye kupendwa, kigezo na mfano wa kufuatwa na kila mwenye kumtaraji Allah katika kila nyanja ya maisha yetu ya kila siku, hivyo tuwe na hadhari na familia zetu kwa tunaempenda, kumsikiliza, kumfuata, kumsaidia na kumfanya kuwa rafiki (shoga) au hata kumkaribisha nyumbani kwako au kumchukuwa kama kigezo chetu au kuwa ndio mfano wetu.

 

Ndugu Waislamu, ‘iyd haiwi ‘iyd kama hatutokuwa tayari kusameheyana, kukumbushana, kuwaidhiana, kuusiana na kuamrishana mema na kukatazana maovu (kama hayo waliyoyaandaa wanawake wawili na kundi lao) katika maisha yetu ya kila siku.  Ndugu Waislamu, ni vyema tuelewe kuwa sisi ni waislamu, na hatutokuwa na maendeleo yo yote yale wala heshima wala 'izzah bila ya kurudi katika dini yetu na kujinasibisha nayo katika maisha yetu ya kila siku.

 

Ndugu Waislamu, Uislamu ndio dini pekee ya haki mbele ya Allah, sisi kama Waislamu nini tunafanya katika kuonyesha na kuthibitisha haya (rusha roho, magoma moto moto, vinywaji wa kila aina, wake kwa waume, tafadhali muarifu mwenzako – laiti tungekuwa tuna arifiana mambo ya kheri- )?  Uko wapi utekelezaji wetu wa maamrisho ya Allah na utekelezaji wetu wa makatazo ya Allah, uko wapi ulinganio wetu kwa watu kurudi katika dini ya Allah na kwa wasiokuwa waislamu kuingia na kufuata dini ya Allah, dini ya haki inayokenda sambamba na maumbile yetu. 

 

Ndugu katika iman, fanya kila ulifanyalo lakini hakikisha kuwa litakupelekea kuweza kujihakikishia kuwa siku ya ‘iyd kwako ni ile siku utakayopewa kitabu chako kwa mkono wa kulia, Qur-an inasema:

“Basi ama atakaye pewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, atasema: Haya someni kitabu changu! (tafadhali waarifu wenzako)    Hakika nalijua ya kuwa nitapokea hisabu yangu.   Basi yeye atakuwa katika maisha ya kupendeza.  Katika Bustani ya juu (ukumbi wa Britwell, Slough).  Matunda yake yakaribu.   Waambiwe: Kuleni na mnywe kwa furaha (Chakula na vinywaji vya aina zote vitakuwepo) kwa sababu ya mlivyo tanguliza katika siku zilizo pita (kuanzia saa nane za mchana hadi saa nne za usiku).” Al-Haaqqah aya ya 19-24.

Ndugu yangu katika iman, fanya ulifanyalo litatokuhakikishia kuwa ‘iyd yako na furaha yako ya kweli na sherehe za kusheherekea iwe ile siku utakayo epusha na Jahannam Moto (Rusha Roho, Disco Toto pamoja na magoma moto moto ya aina zote) na kuambiwa kwa heshma na ta’adhima ingia Peponi, Qur-an inasema:

كُلُّ نَفْسٍ ذَآئِقَةُ الْمَوْتِ وَإِنَّمَا تُوَفَّوْنَ أُجُورَكُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ فَمَن زُحْزِحَ عَنِ النَّارِ وَأُدْخِلَ

الْجَنَّةَ فَقَدْ فَازَ وَما الْحَيَاةُ الدُّنْيَا إِلاَّ مَتَاعُ الْغُرُورِ

 

“Kila nafsi itaonja mauti. Na bila ya shaka mtapewa ujira wenu kaamili Siku ya Kiyama. Na atakaye epushwa na Moto na akatiwa Peponi basi huyo amefuzu. Na maisha ya dunia si kitu ila ni starehe ya udanganyifu.” Al ‘Imraan aya ya 185.

 

Hivyo ni vyema kila tunapokutana kuwaombea dua na kuwaombea maghfirah msamaha kwa Ghaffar Mola wetu na Mola wa waliokuwa kabla yetu na watakao kuja baada yetu.

              

Ndugu Waislamu, tumuombe ar-Rahmaan aturejeshe katika dini yake urejesho ulio mzuri, tumuombe ar-Rahmaan atukubalie yetu Ramadhan, atupe uwezo wa kutekeleza ayatakayo Yeye Subhanah Muumba wetu, na kuachana na makatazo yake, atupe uwezo wa kufikisha amana kama ilivyofikisha al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), atutie mapenzi baina yetu mapenzi yatayozaa kuwa tayari kusameheyana, kuhurumiana, kupendana, kustahamiliana, kamrishana mema na kukatazana maovu na kadhalika.

 

Kila mwaka na nyinyi muko katika kheri

Wassalamu'alaykum Warahmatu Llahi Wabarakatuh

Mkusanyaji

Ndugu yenu katika imani

Abu Fatimah