|
UJANJA WA
KUTENGANA (SEPARATION)
Assalaam Alaykum!
Ndugu zangu waislam suala hili limekuwa likijitokeza na
kuulizwa katika sehemu nyingi hapa Uingereza ambazo waislamu
hukusanyika kwa ajili ya mikusanyiko ya kidini na kutafutiwa
hukumu yake. Wengine hujaribu kuvuka bahari na kujaribu
kuwauliza masheikh tofauti sehemu mbali mbali duniani
kujaribu kupata “fatwa” .Hivyo baada ya kukaa na
kulitafakari sana suala hili tumeona tutoe makala juu ya
kadhia hii nzima chimbuko, faida, athari na madhara yake kwa
mfumo mzima wa maisha ya ndoa ya muislam.
Ingawa suala hili ni nyeti
kwa baadhi yetu lakini unyeti wake sidhani kwamba utamzuia
muislamu kulizungumzia huku tukiona mmomonyoko wa kimaadili
ukiendelea na kuharibu jamii zetu huku tukichelea kujaribu
kulizungumzia. Pia kulijitokeza kauli kwamba kwa nini
tunakuwa na hamu sana kuyazungumzia masuala kama haya wakati
kuna mengine ya kimsingi lakini tunakuwa wazito au woga
kuyakemea kwasababu yanatugusa. Binafsi, Wallahu A’alamu,
sidhani kama ni sababu kwani kama tulivyoainisha mwanzoni
kwamba chimbuko la makala hii ni kukithiri kwa masuala
yanayohusiana na kadhia hii .
Lengo la makala hii ni kujaribu kuwazindua na kuwaamsha
waliolala na kuwanufaisha wale watakaowaidhika na kuwa
ukumbusho kwa kila aliyehusika kwa njia moja au nyengine
katika kadhia hii .
Imebidi tuuite ujanja kwani ndiyo hali halisi. Ujanja huu
ambao mke na mume huufanya kwa kudai mbele ya serikali
kutengana na hali halisi ni kwamba si kweli ila ni mbinu tu
ya kupata unafuu wa maisha . Na baada ya kufanyika ujanja
huu baadhi ya waislam hurudi tena nyuma na kujaribu
kuangalia hukmu yake katika uislam je inakubalika? .Suala
jengine ambalo linajitokeza katika kadhia hii ni ile ndoa
iliyokuwepo kabla ya ujanja huu bado itaitwa ndoa au
kitakuwa kitu chengine tukimaanisha mke kaachika ,ndoa ile
bado ipo au imebatilika au…….? Na labda kwa kuwa hawa
wanandoa walikubaliana kufanya ujanja huu kwa pamoja , je
utakuwa na athari yoyote kwenye ndoa yao halali?
Kwanza kabisa kabla ya hata kuingia katika kadhia yenyewe
ambayo tayari imeweza kujipenyeza na kuenea katika jamii
yetu kwa kasi sana na kudiriki kusema asilimia kadhaa ya
zinazoitwa “ndoa” basi zimo katika mfumo huu. Yaani
kiserikali wametengana lakini hali halisi wanaishi pamoja
kiada. Au kiserikali hata hawaishi pamoja kumbe huku pembeni
ni mke na mume. Tunaita kiada kwani kisheria hatuwezi kuwa
na uhakika wa moja kwa moja kwamba ndoa bado ipo au laa.
Hivyo kwa kujaribu kupata ufafanuzi wa kadhia hii ni vyema
tukaangalia kwa hawa wenyewe wazungu ni nini maana ya
kutengana.
Judicial separation (Kutengana
kwa kisheria) ni kule kutengana kwa mke na mume na hivyo
kuondokana na ule wajibu wa kuishi pamoja bila ya
kubatilisha ndoa au kuachana.Sababu zinazoruhusu wanandoa
kutengana kubwa ni mbili nazo ni ukatili(uonevu) na uzinifu
(kutembea nje ya ndoa).Baada ya mwaka 1976 sababu hizi
zilibadilishwa na kuwa: uzinifu (kutembea nje ya ndoa),
tabia isiyoweza kuvumilika, kutoishi nyumba moja kwa muda
mrefu zaidi ya miaka miwili.
Kutengana (Separation) katika utamaduni wa kizungu ni kuwa
haina maana ya talaka. Bali ina maana ya kutengana kweli
kweli, nakusudia kusema kuwa hawa wenye ku-declare
separation huwa hawaishi tena pamoja, na huku kutoishi
pamoja ndipo pahala tunapopataka hasa, na mara nyingi huko
kutengana kwao huwa ndiyo mwanzo wa process ya talaka
,hutengana kwanza na baada ya kupita muda na taratibu za
kisheria mwishowe huachana.
Nayo ni aina mbili:
1.Ya muda (Temporary)
2.Ya kudumu (Permanent)
Sasa turudi kwa hii aina yetu mpya ya kutengana inaingia
katika maana iliyotajwa hapo juu au laa?
Ukiiangalia aina yetu unaikuta haimo
katika zote hizi mbili si ya muda na wala si ya kudumu
lakini kauli ya kwamba tumetengana imetamkwa ila wanandoa
huwa wanaishi kama walivyokuwa, kama kwamba hakuna
kilichotendeka.
Na kuna aina nyengine ambayo si kutengana bali ni kudanganya
na kusema uongo .Kwamba mke na mume wamefanya mambo yao kila
mtu kivyake wakati wakijijua kama ni mume na mke.Hawa
hawajatengana bali mmoja wao huishi kama single/lone parent
kwa mujibu wa serikali na mke na mume, kiadana kikawaida .
Sababu kubwa inayowafanya wanandoa kufanya janja hizi ni kwa
kuyaona “maslahi” yafuatayo:
1. Ujanja wa Mume kutotaka kulipa kodi (rent) na council tax
ya nyumba.
2. Uchu wa mwanamke kutaka kuwa na kipato kila wiki bila ya
jasho.
3. Kuwa na kiakiba cha fedha .
4. Kupata msaada katika suala zima la huduma (nafaqa).
Inawezekana kuwa uchache wa elimu wa hawa watu kuelewa kuwa
jukumu la kuwalisha watoto (nafaqa) ni jukumu lililopewa
umuhimu wa juu katika dini kwa mzazi mwenyewe limewapelekea
kunasa kwenye mtego wa ujanja huu.
Ieleweke kwamba katika Sheria ya ndoa ya kiislam imeeleza
vitu viwili kama ilivyotajwa katika Quraan Al Baqarah/229 ni
kwamba
الطَّلاَقُ
مَرَّتَانِ فَإِمْسَاكٌ بِمَعْرُوفٍ أَوْ تَسْرِيحٌ
بِإِحْسَانٍ
“…. Talaka ni mara mbili ima tukae kwa
wema (na wake zetu ) au kuachana kwa ihsani……...”
Suala la kutengana halikutajwa kabisa. Hivyo suala la
kutengana (separation) si suala la kulitafutia hukmu ya
kiislam ila tutakacho kitafutia hukmu ya kiislam ni ile
kauli iliyotolewa wakati wa kutengana,Kulitamkwa kauli gani,
nimekuacha, nimekutenga, nimekukataa, sikutaki,si mke wangu,
simjui aliko…..
Na hapo kuiangalia kauli hiyo je itakuwa katika hukmu ya
talaka au si talaka? Na hata ikiwa kama ni uongo na si
makusudio ya wanandoa kusema hivyo wakikusudia talaka.
Lakini kisheria ni wajibu kuiangalia kauli hiyo kwa makini
sana na kisha kuipatia hukmu muafaka.
ATHARI ZAKE
Kinachowapelekea watu kuamua kutengana au kutojitambulisha
rasmi kwa wahusika kwamba wao ni wanandoa ( kwa wale ambao
wameoana lakini walipofika hapa wamekwenda kufanya mambo
kila mtu kivyake),kumeleta athari nyingi sana mbaya kwa dini
yetu ya kiislamu kwanza na pia kwa jamii zetu kama hizi
zifuatazo:
1. Kuwatukanisha wanawake wa Kiislamu rasmi – official- kuwa
wanazaa bila ya kuwa na waume, kwani kila wakienda DSS huwa
wanasema hawana waume, lakini kila mara huwa wanazaa au hata
baada ya miaka miwili au mitatu.Wakati inaeleweka vyema
kwamba kuzaa nje ya ndoa kiislamu ni haramu.
2. Kuwadhalilisha wanawake wa Kiislamu mbele ya makafiri
official kuwa wao ni malaya hata kama wanajidai
kuwa hawatendi umalaya.Inayotukanwa hapa ni dini ya Allah
Subhaanahu Wataala.
3 Kubwa kuliko hayo ni kuutukanisha Uislam na kuwa kuzuizi
cha wasiokuwa waislamu kuingia katika dini ya
Allah, kwani wengi hawana nafasi ya kusoma lakini wana
nafasi ya kuona, hivyo da’awah ya vitendo
hapa ndio inafanya kazi zaidi ya da’awah ya maneno au
maandishi kuwa wanawake wa Kiislamu huwa wanautukanisha
Uislam kivitendo wakati wanapokwenda kuomba msaada wakidai
kuwa hawana uwezo!.
4 Wanawake kuwa na nguvu na madaraka juu ya waume zao
wengine kufikia kuwafukuza hao “waume” kwenye majumba na
hapa kugeuza maana halisi ya ile aya ya 34 ya Suuratu
Nnisaai
الرِّجَالُ قَوَّامُونَ عَلَى النِّسَاء بِمَا فَضَّلَ اللّهُ
بَعْضَهُمْ عَلَى بَعْضٍ وَبِمَا أَنفَقُواْ مِنْ
أَمْوَالِهِمْ
“Wanaume ni wasimamizi wa wanawake kwa
kufadhiliwa na Allah baadhi yao juu ya baadhi, na kwa mali
yao wanayo yatoa”
Na kuwa wanawake ni wasimamizi wa wanaume!.Hivyo kwenda
kinyume na maagizo ya Allah (Subhaanahu Wataala) pale
alipomkabidhi mwanamme jukumu na uongozi wa familia.Tumeona
mifano aina kwa aina jinsi mume anavyodhalilishwa na
kudharauliwa na mke ambae ni mume mwenyewe aliemhangaikia
safari mpaka akafika hapa . Na kibaya zaidi mume kukubali
kudhalilishwa huku kwa kuchelea mambo mengi ya kimaslahi
ambayo atakuwa hatarini kuyakosa.
5 Kukosekana uadilifu na kuingiwa na mtafaruku katika nyumba
kwa kuingiwa na uchu na tamaa ya fedha ambazo hata walengwa
wenyewe huwa haziwafikii kwani pesa ya mtoto mara nyingi
huitumia mama huku akijua kwamba si yake na “baba” kukataa
kutoa huduma akidai si wajibu wake tena kwani DSS ishamvua
jukumu hilo alilokabidhiwa na Allah(Subhaanahu Wataala).
MADHARA YAKE.
Baada ya kuona “maslahi” na athari ya ujanja huu basi ni
vyema na tuangalie madhara yake na hapo tunaweza na kuwa
picha halisi ya je ujanja huu unafaa kufanywa na muislam wa
kweli ambae amemridhia Allah(Subahaanahu Wataala) kuwa mola
wake na uislamu kuwa dini yake na Muhammad (Sallallahu
“Alayhi Wassallam) kuwa ni Mtume wake?
1 Watoto kukosa mwelekeo sahihi wa malezi kwenye nyumba
ambayo tayari haijasimama kwa misingi ya kisheria ya ndoa ya
kiislam.Tumeona athari hizi katika majumba ambapo tofauti
zinazojitokeza kwa wazazi watoto huziona .
2 Kuweza kula, kunywa, kuvaa kwa haramu kwani hatujui pesa
ipi ni halali kwetu na ipi ni haramu .
3 Kuharibika /kubatilika kwa ndoa kwani wengine wanaishi tu
bila ya kujijua kama ni mume na mke.
4 Uwezekano wa mtu kuwakosa watoto wake mwenyewe endapo mama
atafariki na watoto kutokuwa na “baba”(tayari tunayo mifano
hai kwani yashatukuta).
5 Hata ikitokezea watoto kuchukuliwa na DSS, jukumu la
kuwalea watoto bado lipo palepale kwa mzazi kwa lolote
atakalolifanya mtoto hata akiwa hayuko kwenye madaraka yake.
HITIMISHO
Baada ya maelezo na ufafanuzi huu ,turudi tena kwenye kadhia
yetu.Ifahamike kwamba Ujanja wa kutengana (Separation) kuwa:
1 Sio talaka wala haina sura wala maana ya talaka kwa
mtazamo wa sheria ya Kiislamu. Hata hivyo athari zake ni
mbaya zaidi hata kuliko talaka yenyewe kwani talaka inakuwa
imejulikana kama hakuna ndoa tena ,lakini sura yetu hii ya
kutengana ni balaa tupu hakueleweki kama ndoa ipo au laa.
Hawa watakuwa wanasema uongo na kudanganya ni moja katika
dhambi za ulimi.
Ndoa hata hivyo ipo kwani hakuna jambo lililofanyika
lililobatilisha ndoa hii ila uongo huu unaweza kuiathiri
ndoa kwa kukosa mwenye kuiangalia kwani Allah (Subhaanahu
Wataala) anasema mwishoni mwa aya ya kwanza Annisaa ya
kwamba “...hakika Allah ni mwenye kukuangalieni” Vipi Allah
Aiangalie ndoa ambayo haikusimama kwa misingi aliyoileta?
2 Matamshi yaliyotumika au yanayotumika katika kuji- declare
huko ndio muhimu kuyatafuta na kuyatazama, kama Mume
(mwanamke hawezi kujiacha, kwa maana ya talaka bali yeye
huwa na Khul’u) alitumia matamshi ambayo ni miongoni mwa
matamshi ya talaka basi hapa ndio patizamwe, je talaka
imepatikanwa/ imesibu au haijasibu? Muhammad (Sallallahu
‘Alayhi Wassallam) anasema katika hadithi “ mambo matatu
(ukiyafanya kwa ) utani (huwa)
ni kweli na (yakifanywa kwa) ukweli huwa ni kweli; ndoa,
talaka na kumrejea mke”
Imam Shafi na Abu Hanifa wanaona talaka haihitaji nia
ikitamkwa tu au kuashiriwa basi tayari ni talaka.
Imam Malik
anasema talaka haisibu mpaka iambatane na nia.
Baada ya ufafanuzi huu tunaweza kutoa tahadhari kwa wanandoa
hawa isije mpangilio wao huu ukaweza kuathiri ndoa ya
kiislamu na kuhesabika kuwa talaka japo hawakukusudia lakini
maneno yalitamkwa au kuandikwa na katika suala la talaka
kitachoangaliwa je! kulitamkwa talaka ? Bila kujali kama
matamshi hayo yalikusudiwa ndoa ya kiislamu au ya kiserikali
ambayo kwa mtazamo wa kiislamu si ndoa na wala haina athari
na hivyo matamshi pia hayatokuwa na athari kwa ndoa ya
kiserikali lakini yanaweza kuiathiri ndoa ya kiislamu.
3 Hata kama tunasema kuwa walikubaliana, bado jukumu kubwa
ni la Mume kwani yawezekana kuwa mwanamke hana budi kutokana
na vitisho / hila / mbinu za mumewe ndio akakubali, hivyo
mume ndio muhusika wa kwanza na wa mwisho katika hukumu ya
ujanja huu.Kwa sababu yeye ndie aliepewa jukumu la
kuisimamia familia yake na kuiongoza.
عن عبد الله رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال
: " كلكم راع فمسؤول عن رعيته فالأمير الذي على الناس راع وهو
مسؤول عنهم والرجل راع على أهل بيته وهو مسؤول عنهم والمرأة
راعية على بيت بعلها وولده وهي مسؤولة عنهم والعبد راع على مال
سيده وهو مسؤول عنه ألا فكلكم راع وكلكم مسؤول عن رعيته " رواه
البخاري ( 2416
) ومسلم ( 1829)
Kutoka kwa
Abdullah Allah amuwie radhi kwamba Mtume Muhammad (Sallallahu
‘Alayhi Wassallam) amesema :
“Nyote ni wachunga na nyote mtaulizwa juu ya mlivyovichunga.
Kiongozi anaewaongoza watu ni mchunga na ataulizwa juu
wachungwa wake. Mwanamume ni mchunga kwa watu wake wa
nyumbani na ataulizwa juu ya wachungwa wake. Na mwanamke ni
mchunga kwa nyumba ya mumewe na watoto wake nae ataulizwa
juu ya wachungwa wake .Mtumwa ni mchunga katika mali ya
bwana wake na anawajibika juu ya mali hiyo. Hakika nyote ni
wachunga na na kila mmoja wenu anawajibika juu ya wachungwa
wake”
Imesimuliwa na Bukhari na Muslim
WITO
Ujanja huu madhara yake ni makubwa mno katika dini na hata
dunia yetu kushinda hata “faida” zinazoonekana kupatikana
kihali na mali na Allah Subhaanahu Wataala anatuonya kwa
ukali kuchunga nafsi zetu pamoja na familia zetu kama
anavyosema katika Suuratu Tahreem/6
يأَيُّهَا الَّذِينَ ءَامَنُواْ قُواْ أَنفُسَكُمْ
وَأَهْلِيكُمْ نَاراً وَقُودُهَا النَّاسُ وَالْحِجَارَةُ
عَلَيْهَا مَلَـئِكَةٌ غِلاَظٌ شِدَادٌ لاَّ يَعْصُونَ اللَّهَ
مَآ أَمَرَهُمْ وَيَفْعَلُونَ مَا يُؤْمَرُونَ
Enyi mlio amini! Jilindeni(jiokoeni) nafsi
zenu na ahli(familia) zenu na Moto ambao kuni zake ni watu
na mawe. Wanausimamia Malaika wakali, wenye nguvu, hawamuasi
Allah kwa anayo waamrisha, na wanatenda wanayo amrishwa.
Hivyo tunawaasa kwa nia njema kabisa wahusika waliofanya
janja hizi kwa kukusudia,au kwa bahati mbaya au kwa
kutokuelewa, kutubia mara moja kwa mola wao na kuondokana na
kila aina ya maasi na kuzidi kurudi kwake Subhaanahu Wataala
kwa maghfira na toba .
Tumuombe Allah Subhaanahu Wata’aala atupe nguvu na uwezo wa
kuweza kuyaacha yote aliyoyakataza na kufanya kila
aliloliamrisha. Amin
Wallahu A’alamu
Abu Ammaar
yasihali@hotmail.com
|